Ijumaa, 1 Septemba 2023

WATUMISHI MAHAKAMA SINGIDA WAHIMIZWA KUDUMISHA UPENDO, USHIRIKIANO

Na Eva Leshange- Mahakama, Singida

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo amewahimiza watumishi wa Mahakama mkoani Singida kudumisha upendo, ushirikiano na mshikamano mahala pa kazi.

Mhe. Dkt. Masabo alitoa wito huo hivi karibuni alipokuwa anaongea na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama za Mwanzo kwenye ziara yake ya kikazi mkoani hapa. Alisema kuwa mambo hayo matatu yakitekelezwa yatafanya mahala pa kazi kuwa pazuri na rafiki kwakuwa watumishi hutumia muda mwingi wakiwa kazini.

“Watumishi wenzangu, nasisitiza tuimarishe upendo, ushirikiano na mshikamano mahala pa kazi kwani tunatumia muda mwingi kazini. Tushikamane, tubebeane mapungufu na tuinuane tunapo anguka,” alisema.

Aidha, Jaji Mfawidhi aliwapongeza Mahakimu na watumishi wa kada zingine kwa kazi nzuri wanayofanya, hasa katika usikilizaji wa mashauri. Aliwataka kuongeza kasi zaidi na kuhakikisha hakuna mlundikano wa mashauri.

Aliwakumbusha Mahakimu kufikia kipimo kilichowekwa na Mahakama chz kumaliza mashauri, hivyo kila mmoja anatakiwa kujitathmini kama amefikia malengo kwa kiasi gani.

Mhe. Dkt. Masabo aliwasisitiza Mahakimu kuwa waadilifu, kwani kazi ya kutoa maamuzi ni kazi ya kimungu ambayo haiwezi kufanyika pasipo uadilifu.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi alisisitiza malipo ya mirathi kufanyika ipasavyo kwa wanufaika na kuhimiza jitahada binafsi zifanyike kwa kufanya upekuzi kwenye majalada yote ambayo mirathi haijafungwa ili kubaini kama kuna wanufaika ambao hawajalipwa.

Katika ziara yake mkoani hapa, Mhe. Dkt. Masabo alipata fursa ya kutembelea Gereza la Wilaya Singida na kusikiliza kero za wafungwa na mahabusu.

 Aliwapongeza wadau wote wa haki jinai kwa kazi nzuri wanayofanya, kwani hali ya Gereza hilo inaonekana kuwa nzuri, hakuna msongamano na changamoto zote zilizoibuliwa zilitolewa majibu.

 


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyekaa mbelekatikati) akiongea na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida na Watumishi wa Mahakama za Mwanzo Singida(hawapo pichani).

Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Watumishi wa Mahakama za Mwanzo mkoani Singida wakisalimiana na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe Dkt. Juliana Masabo alipokua kwenye ziara ya kikazi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Singida, Mhe. Allu Nzowa akimkaribisha Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyeketi mbele kulia) akiwa ameambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu kanda ya Dodoma, Mhe. Sylivia Lushasi (aliyeketi kushoto)

Sehemu ya watumishi wakijitambulisha Mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (aliyekaa mbele katikati). Anaye jitambulisha ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Utemini, Mhe. Ferdnand Njau.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo akisalimiana na wajumbe wa haki jinai alipowasiri Gereza la Wilaya Singida kwa ajili ya ukaguzi.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni