Jumanne, 31 Oktoba 2023

GEREZA LA MAHABUSU MPANDA LAUNGANISHWA NA MAHAKAMA KIMTANDAO

Na. James Kapele- Mahakama, Katavi

Kaimu Mkuu wa Gereza la Mahabusu Mkoa wa Katavi, Kamishina Msaidizi wa Magereza (ACP) Christopher Fungo ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kusimika mfumo mzuri na bora wa usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao.

Mfumo huo utawezesha kusikilizwa mashauri kwa njia ya mtandao bila kumtaka mshitakiwa kufika mahakamani, hivyo kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za gereza hilo.

Vifaa hivyo ambavyo ni TV na vifaa vingine wezeshi kutoka Mahakama ya Tanzania viliwasilisha gerezani hapo na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe. Gway Sumaye.

Akizungumza katika hafla hiyo, Kaimu Mkuu wa Gereza hilo ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuona umuhimu wa kuwapatia vifaa hivyo ambavyo vitawezesha na kuongeza ufanisi katika usikilizaji wa mashauri.

“Kwa hakika vifaa hivi vimeletwa kwa wakati ambao vinahitajika sana kwa kuwa Mkoa huu una gereza moja tu la mahabusu ambao huletwa hapa kutoka katika Wilaya zote. Hivyo niishukuru sana Mahakama kwa kuwa vifaa hivi vitasaidia kutupunguzia gharama za uendeshaji wa mashauri, hasa ukizingatia jiografia ya Mkoa wetu,” alisema.

Vifaa hivyo vimesimikwa na Afisa Tehama wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Bw. Innocent Mayanga ambaye amewapitisha baadhi ya askari magereza wanaosimamia gereza hilo matumiziya mfumo huo.

Awali, akikabidhi vifaa hivyo, Mhe Sumaye amewahimiza askali hao kuvitunza kwa kuwa vimepatikana kwa gharama kubwa na kwamba vitasaidia katika uendeshaji wa mashauri.

Upatikanaji wa vifaa hivyo kwa magereza ni moja katika ya mipango mahsusi ambayo Mahakama imejiwekea katika mpango mkakati wa kuboresha huduma ili kuhakikisha mashauri yote yanasikilizwa kwa wakati.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe, Gway Sumaye (wa tatu kutoka kulia) akikabidhi vifaa hivyo kwa Kaimu Mkuu wa Gereza la Mahabusu Mpanda. Wengine ni Mtendaji wa Mahakama Mkoa wa Katavi, Bw. Allan Mwella (wa pili kushoto) ambaye naye alishiriki shughuli hiyo.


Sehemu ya wafungwa wakiingiza vifaa hivyo gerezani kwa ajili ya kusimikwa rasmi.
Afisa Tehama wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Bw. Innocent Mayanga (wa pili kushoto) akionekana katika luninga maalumu baada ya kusimika mfumo huo.

 (Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni