Jumatano, 11 Oktoba 2023

IKULU NETIBOLI YANUSURIKA KICHAPO

·Mahakama Sports yashangaza wengi

·Hujuma, mbeleko zatawala mpira wa miguu

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Ikulu inayoundwa na wachezaji wa Timu ya Taifa ya Netiboli Tanzania leo tarehe 11 Octoba, 2023 imenusurika kichapo baada ya kukabwa koo na Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) katika mchezo wa nusu fainali  kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Mchezo uliofanyika kwenye viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikristo Ruaha kuanzia majira ya saa 10:00 jioni ulikuwa wa vuta ni kuvute huku Mahakama Sports ikitoa upinzani mkali kiasi cha kuwafanya Ikulu kutoamini kilichokuwa inatokea.

Mahakama Sports inayoundwa na vijana wadogo wadogo ambao hawana uzoefu mkubwa walionyesha mchezo mzuri uliowainua mashabiki mara kwa mara na kuwafanya Ikulu kufanya mabadiliko mara tatu.

Hadi mchezo unamalizika, Ikulu ikafanikiwa kutinga katika hatua ya nusu fainali kwa mbinde baada ya kutumbukiza vikapu 77 kwa 8 walivyopatya Mahakama Sports. Kwa matokeo hayo, Mahakama Sports itajitupa kesho tarehe 12 Octoba, 2023 kuwania katika nafasi ya tat una Hazina.

Wakati huo huo, hujuma za wazi zimetawala kwenye mchezo wa mpira wa miguu uliochezwa kwenye uwanja wa Samora saa 10:00 jioni, kuwakutanisha Mahakama Sports na Hazina, ambao wameibuka na ushindi kwa faida ya mwamuzi.

‘Man of the match’ kwenye mtanange huo alikuwa mwamuzi na dalili za upendeleo zilianza kuonekana mapema baada ya kuwazawadia Hazina tuta katika mazingira ya kutatanisha, dakika chache baada ya kuanza mchezo huo.

Hazina ambao ni vibonde na hawakuwa na lolote la maana zaidi ya kubebwa na mwamuzi walitumia nafasi hiyo na kufanikiwa kupata bao ambalo lilidumu hadi mwisho wa mchezo.

Mahakama Sports walionesha kandanda safi na kupata nafasi nyingi, lakini walikumbana na mchezo mbaya kwa kukanyagwa na kupigwa viwiko mara kwa mara na wachezaji wa Hazina, huku mwamuzi akiwa hachukui hatua yoyote.

Kadhalika, Mahakama Sports ilipata matuta ya wazi matatu katika kipindi cha kwanza na dakika za mwisho mwisho za mtanange huo, lakini mwamuzi akang’ata filimbi, jambo lililowashangaza wanamichezo waliofurika katika uwanja kushuhudia kabumbu hilo.

Kufuatia matokeo hayo, Mahakama Sports itamenyana na ndugu zao, Wizara ya Katiba na Sheria kesho tarehe 12 Octoba, 2023, ili kumtafuta mshindi wa tatu.

Mahakama Sports Mpira wa Miguu, ni vijana hatari wanaojua kusakata kabumbu. Mwamuzi kafanya yake kuwajeruhi vijana hawa. No fair play at all.
Mahakama Sports wakilisakama lango la Hazina mara kwa mara kama picha zinazoonyesha (juu na mbili chini). Hazina hawakufanya shambulio lolote zaidi ya tuta walilozawadiwa na mwamuzi.


Mwalimu wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe akiongea na vijana wake wakati wa mapumziko.
Hawa hapa Hazina, wamecheza mpira mbovu usio wa kiungwana.Mbeleko ya mwamuzi imewaokoa.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni