Jumatatu, 9 Oktoba 2023

JAJI MFAWIDHI MOROGORO AWAHIMIZA MAHAKIMU KUWAJIBIKA

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor hivi karibuni alikutana na kuzungumza na Mahakimu wote wa Mahakama katika Kanda yake kukumbushana uwajibikaji na kupeana mikakati ya utoaji huduma ya haki kwa wananchi.

Kikao hiko kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mkutano katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) kilihudhuriwa na Majaji, Naibu Msajili na Mtendaji ambao kwa nyakati tofauti walipata wasaa wa kuongea na Mahakimu hao.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mansoor alisema kuwa angependa Hakimu atambulike zaidi kupitia uwajibikaji mzuri na sio vinginevyo.

“Wote hapa tumekasimiwa mamlaka ya kutoa haki kwa wananchi na sio vinginevyo, ni rai yangu tufanye jukumu hilo kwa uadidilifu usio tia mashaka, weredi mkubwa na wote tuwajibike kwa usahihi” alisema Jaji Mfawidhi.

Naye Jaji Messe Chaba alizugumzia suala la mashauri ya mirathi na kuwataka Mahakimu kuweka mikakati bora ya namna ya kuwaelekeza wasimamizi wa mirathi mara shauri linapomalizika.

Aliongeza kuwa takwimu zinaonesha uwepo wa kiasi kikubwa cha fedha katika akaunti ya Mahakama Kanda ya Morogoro na zinasubiri kulipwa kwa wanufaika wa mirathi.

“Tuwasaidie wahusika kubainisha taarifa zao sahihi ili mafao yaweze kuwafikia wanufaika kwa wakati,” alieleza na kusisitiza wale waliopewa jukumu la kukagua nyaraka za mashauri ya mirathi kufanya kazi hiyo ipasavyo.

Kwa upande wake, Jaji Gabriel Malata aliwahimiza Mahakimu kuiishi salamu ya Mahakama ya Tanzania inayosema “Uadilifu, Weredi na Uwajibikaji” na kila mmoja kutambua mamlaka aliyopewa.

Aliwaeleza Mahakimu hao kutogeuza mafaili yaliyopo mezani kwao kuwa fulsa ya kupenyeza mianya ya rushwa.

Naibu Msajili, Mhe. Agustina Mmbando alipalilia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kusema hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati wa Mahakama, hivyo aliwataka maafisa hao kuishi kimkakati.

“JSDS sasa hivi imeboreshwa na sasa tunaenda kwenye mfumo mpya wa usajili wa mashauri wa CMS ambao tayari umefanyiwa majaribio na hii ni kwa Mahakimu wote nchi nzima,” alisema.

Katika kikao hicho, wajumbe walitumia nafasi hiyo kuwachagua Viongozi wa Chama cha Majaji na Mahakimu (JMAT) Kanda ya Morogoro na Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Kihonda, Mhe. Kisaka Ramadhani alichaguliwa kuwa Mwenyekiti.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor akizungumza wakati wa kikao. Kushoto kwake ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda hiyo, Mhe. Messe Chaba.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba akizungumza wakati wa kikao.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Gabriel Malata akizungumza wakati wa kikao.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Augustina Mmbando akifuatilia hoja wakati wa kikao.

Sehemu ya washiriki wa kikao.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mdawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (katikati) pamoja na Majaji Messe Chaba (kushoto) na Gabriel Malata (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao hicho.

Mwenyekiti wa JMAT Kanda ya Morogoro, Mhe. Kisaka Ramadhani akisoma taarifa fupi mara baada ya kuchaguliwa.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mdawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (katikati) pamoja na Majaji Messe Chaba (kushoto) na Gabriel Malata (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa JMAT Kanda ya Morogoro mara baada ya kuchaguliwa.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mdawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (katikati) pamoja na Majaji Messe Chaba (kushoto) na Gabriel Malata (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Kanda ya Morogoro katika mkutano mkuu wa JMAT unaotegemea kufanyika mwezi Desemba huko jijini Dodoma.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni