Jumamosi, 7 Oktoba 2023

KING’ANG’ANIZI SHIMIWI IRINGA AKIONA CHA MOTO

· Mahakama Sports yawachapa mbili kwa karai

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu leo tarehe Octoba, 2023 imeikung’uta Ardhi mabao 2:0 na kutinga robo fainali kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Ardhi waliokuwa wanang’ang’ania kucheza na Mahakama Sports licha ya kuondolewa kwenye mashindano kwa kuchezesha mamluki imekiona cha mtema kuni baada ya kufungashiwa vilago kwenye mashindano hayo baada ya kupokea kichapo hicho.

Awali, Mahakama Sports ilikuwa icheze kabumbu hilo na TARURA jana tarehe 6 Octoba, 2023, lakini mtanange huo uliahirishwa kutokana na fujo zilizoletwa na Ardhi na kukataa kutoka uwanjani, huku Viongozi wao wakidai hawakuwa na barua kutoka SHIMIWI inayowatoa kwenye mashindano.

Kabumbu la leo lililochezwa majira ya saa 2:00 asubuhi kwenye Viwanja vya Mkwawa lilianza kwa timu zote kushambuliana kwa zamu, huku Mahakama Sports ikilisakama lango la wapinzani mara kwa mara.

Iliwachukua dakika ya kwanza ya mchezo Mahakama Sports kuukwamisha mpira kwenye nyavu kupitia kwa mshambuliaji wake hatari Martin Mpanduzi. Hata hivyo, mshika kibendera namba mbili alilikataa bao hilo kwa madai ya mfungaji kuwa aliotea, kitendo kilichozua zomea zomea kwa mashabiki kwa kukataa bao hilo halali.

Kukataliwa kwa bao hilo kuliwaamsha Mahakama Sports na kuzidisha mashambulizi. Katika dakika ya 11, beki wa kushoto Gisbert Chentro aliachia shuti kali lililomshinda mlinda mlango wa Ardhi na kujaa kwenye wavu, hivyo kuiandikia timu yake bao la kwanza.

Baada ya kuingia kwa bao hilo, Ardhi walionekana kuzidiwa hasa katika eneo la katikati, huku vijana wa Mahakama Sports wakisakata kandanda safi na kuutawala mchezo. Ilipofika katika dakika ya 24, Mpanduzi aliwatoka walinzi wa Ardhi na kupachika bao la pili na la ushindi kwa timu yake.

Hadi timu zinaenda kwenye mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa mbele kwa mabao 2:0. Katika kipindi cha pili, timu zote zilikuwa zinashambulia kwa kuviziana, lakini mabeki walikaa imara hadi mwisho wa mchezo hakuna timu iliyoweza kuliona lango la mwenzake.

Akizungumza baada ya mchezo huo kukamilika, Mwalimu Spear Mbwembe amewapongeza vijana wake kwa kucheza kwa tahadhari kubwa na kupata matokeo kwa kuzingatia ubora wa timu pinzani.

“Hawa jamaa (Ardhi) ni wazuri sana, lakini nashukuru vijana wangu wamezingatia maelekezo yangu na kuweza kuwadhibiti. Mchezo huu waliouonesha, itafungwa timu yoyote itakayokuja mbele yetu,” amesema.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema anauhakika timu yake itachukua kombe mwaka huu kutokana na ubora wa vijana alionao na hakuna yeyote atakayewazuia kwenye hatua zinazofuata.

“Hawa Ardhi ni wazuri sana. Ingawa kulikuwepo na mkanganyiko namna walivyorudishwa kwenye mashindano, sisi tulikubali kupambana nao na bahati nzuri wamekiona cha moto. Sasa tunaangalia mbele na tutaendelea kupambana hadi ushindi upatikane,” amesema.

Wachezaji wa Mahakama Sports waliosakata kambumbu ni Fahamu Kibona, Nasoro Mwampamba, Gisbert Chentro, Rashid Mbwana, Akida Mzee, Kelvin Muhagama, Frank Obadia, Seleman Magawa, Martin Mpanduzi, Seif Shamte na Abdi Sasamaro.

Walioanzia kuchoma mahindi ni Michael Turuka, Emmanuel Mwamole, Juma Mbega, Davis Munubi, Timoth Mwakisamba, Gabriel Tabana na Ramadhan Seif. Benchi la ufundi liliongozwa na Kocha Mkuu Spear Mbwembe na Kocha Msaidizi Said Albea.

Alikuwepo pia Timu Meneja Shaibu Kanyachole, Meneja wa Vifaa Eliya Ngule na Daktari Janeth Mapunda.

Miamba hiyo hapo, Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu.
Waamuzi wakiwa katika picha ya pamoja na Manahodha wa Timu zote mbili.
Wachezaji wa Mahakama Sports wakilisakama lango la wapinzani. Picha chini ni mlinda mlango wa timu ya Ardhi akilamba nyasi baada ya kuruhusu bao.

Mabeki wa Mahakama Sports walisimama imara kuondoa hatari yoyote kwenye lango lao.
Mwalimu wa Timu Spear Mbwembwe akiongea na vijana wake wakati wa mapumziko.
Mashabiki wa Mahakama Sports wakiwa wamembeba beki kisiki Gisbert Chentro baada ya mchezo kumalizika. Chentro alifunga bao la kwanza kwa shuti kali lililozua gumzo kwa watazamaji.

Mahabiki wa Mahakama Sports wakiwaimbia Ardhi wimbo wa "Mungu akipenda tutaonana tena."
Mwalimu wa Timu Spear Mbwembwe akiongoza mashabiki kushangilia ushindi.
Orodha kamili ya wachezaji wa Mahakama Sports Mpira wa Miguu wanaoiwakilisha vyema Mahakama ya Tanzania kwenye mashindano hayo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni