Ijumaa, 6 Oktoba 2023

Na. Stephen Kapiga-Mahakama Mwanza.

Mahakama zilizopo katika jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kanda ya Mwanza, leo tarehe 6 Oktoba, 2023, zimehitimisha wiki ya Huduma kwa Mteja kwa kukutana na wateja wote Mahakama kwa lengo la kuwaeleza kwa kina shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mahakama ya Tanzania ikiwemo Mkataba wa Huduma kwa Mteja.

Akizungumza na wateja pamoja na watumishi wanaofanya kazi katika Mahakama za kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini Mwanza, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Chiganga Tengwa amewashukuru watumishi kwa kutoa huduma nzuri kwa wateja kwa kipindi cha wiki zima ya kuadhimisha shughuli hiyo, akawataka kuendelea na ari hiyo ya kutoa huduma bora kwa wateja wote wafikiao katika kituo hicho kupata huduma za kimahakama.

“Ninawashukuru kwa namna ambavyo kwa wiki nzima hii mmependeza na kuwa wachangamfu kwa wateja wetu na kila mmoja amekuwa ni mwenye tabasamu iliyo wavutia wateja na kufurahia huduma kwa kwa wiki hii. Niwasihi tuendelee na moyo huu hata mara baada ya kumalizika kwa zoezi la huduma kwa mteja”. Alisema Mhe.Chinganga Tengwa.

Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Bw. Tutubi Mangazini amesema kuwa, Mahakama inathamini mchango wa wateja wote kwa kuwa wawazi hasa pale kulipotekea kutoelewana kimaelekezo na baadhi ya watumishi waliowapatia huduma na kuwasihi kuwa wasisite kutumia mifumo iliyopo Mahakamani na kufikisha malalamiko yao.

“Ndugu zangu, nikiwa kama Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza jukumu langu kubwa ni kusimamia maswala ya kiutawala na utendaji wa shughuli za watumishi za kila siku ikiwa ni pamoja na kuwawezesha watumishi hawa waliopendeza kuweza kuwahudumia nyinyi vizuri, na yule ambaye atakengeuka kumuwajibisha kulingana na taratibu za kiutumishi. na Naibu Msajili yeye anashughulikia maswala yote ya mashauri yanayohusu Mahakama Kuu”. amesema Bw. Mangazini.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mwanza Mhe. Monica Ndyekobora  amesema, mkataba wa huduma kwa wateja uliopo mahakamani ni kwa ajili ya kusaidia kuainisha wajibu wa watumishi wa Mahakama kwa wateja na pia kuelezea juu ya wajibu wa mteja kwa Mahakama anapofika kutafuta huduma.

“Lengo la mkataba huu ni kuwafahamisha nyinyi wateja huduma zilipo Mahakamani na viwango vya huduma tunazopaswa kuwapatia na utaraibu mnaopaswa kuufuata endapo utaona hujapaitiwa huduma inayoridhisha. Hivyo ni vizuri kama mteja ukatambua wajibu wako pindi unapokuja kupata huduma, mkataba huu unapatika katika tovuti ya TanzLII hivyo kila mmoja anaweza kuupata na kuusoma”. Alisema Mhe Monica Ndyekobora.

Katika siku ya kuhitimisha wiki ya huduma kwa wateja, wateja walielimishwa juu ya mifumo yote inayotumika mahakamani ikiwemo mfumo wa kieletroniki wa kusajili, kusimamia na kuratibu mashauri, mfumo wa kuendesha mashauri kwa njia ya video (Video Conference), Mfumo wa kupandisha maamuzi mtandaoni (TanzLII), mfumo wa malipo ya Serikali, mfumo wa kupokea na kushughulika malalamiko, mfumo wa ramani ilipo Mahakama(JMAP) na mifumo mingine ambata.

Juma la huduma kwa mteja lilianza siku ya juamatatu ya tarehe 2 Oktoba, 2023 na kuhitimishwa rasmi leo tarehe 6 Oktoba, 2023 kwa watumishi wote kukutana na wateja na kuelezea shughuli na majukumu mbalimbali ya Mahakama ya Tanzania ya kila jambo ambalo liliwafurahisha wateja.

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Chiganga Tengwa (aliyesimama mbele) akiwashukuru wateja pamoja na watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini Mwanza kwa kuhitimisha salama wiki ya huduma kwa mteja leo tarehe 6 Oktoba, 2023 walipokutana katika kituo hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Bw. Tutubi Mangazini (aliyesimama mbele) akifafanua jambo kwa wateja na watumishi wa Mahakama waliofika mahakamani katika kilele cha wiki ya huduma kwa mteja.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, Mhe. Monica Ndyekobora akilelezea juu ya Mkataba wa huduma kwa wateja katika kilele cha maadhimisho ya wiki ya huduma kwa mteja.

Mteja wa Mahakama wakiwasilisha maoni yake na kutoa shukrani zake kwa Mahakama baada ya kupata elimu katika kilele cha maadhimisho ya wiki ya huduma kwa mteja.

 

Sehemu ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini Mwanza wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kuanza kwa elimu ya  hitimisho ya wiki ya huduma kwa mteja

Picha ya pamoja kati ya watumishi wa Mahakama Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini  Mwanza wakiwa Pamoja na wateja waliofika mahakamani siku ya kilele cha huduma kwa mteja.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni