Ijumaa, 6 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS NETIBOLI YAIFUMUA SHERIA

·Yaisasambua kwa vikapu 52 kwa 16

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli leo tarehe 6 Octoba, 2023 imeisasambua Sheria kwa vikapu 52 kwa 16 na kufanikiwa kutinga robo fainali kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Mchezo huo uliofanyika kwenye viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikristo Ruaha majira ya saa 4.00 asubuhi ulianza kwa Sheria kudhibiti mpira na kutangulia kutupia vikapu viwili vya haraka haraka katika dakika za mwanzo.

Hata hivyo, Mahakama Sports ilitulia na kuanza kutupa pasi mpenyezo zilizowachanganya wapinzani wao na kuanza kulisakama mara kwa mara lango la Sheria.

Baada ya kujibu mashambulizi, tupia tupia za hapa na pale zilizokuwa zinaongozwa na Tatu Mawazo na Philomena Haule ziliihakikishi timu hiyo kuondoka na ushindi. Hadi timu zote mbili zinaenda kwenye mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa inaongoza kwa vikapu 27 kwa 8.

Katika kipindi cha pili, Mahakama Sports waliendelea kulishambulia lango la wapinzani, huku wakitoa pasi za kuelewana, hatua iliyowawezesha kwenda kwenye lango la wapinzani mara wa mara. 

Kasi ya utupiaji vikapu iliongezeka katika kipindi hicho na kuwezesha Mahakama Sports kutumbukiza vikapu 25, huku Sheria wakiambulia vikapu 8 pekee. Hadi mwamuzi anapuliza kipenga kumaliza mchezo huo, Mahakama Sports ilikuwa imejizolea vikapu 52 kwa 16 walivyotupia Sheria. 

Akizungumza baada ya mchezo huo kumalizika, Mwalimu wa Timu Paul Mathias amesema ameridhishwa na juhudi zinazofanywa na wachezaji wake na anauhakika wataendeleza wimbi la ushindi katika hatua inayofuata.

“Tunaingia kwenye hatua muhimu katika mashindano. Kwetu sisi hatuna kitu kingine zaidi ya ushindi kwa kila mechi itakayokuja mbele yetu. Yoyote atakayejipendekeza tutashughulika naye, ninachowaomba vijana wangu waendelee kujituma na kucheza kwa ushirikiano,” amesema.  

Naye Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema hatua waliyofikia ya robo fainali ni nzuri kuelekea kutwaa kombe. “Safari hii tunakwenda kufanya maajabu, hawataamini kitakachowakuta. Uzuri ni kwamba timu yetu inabadilika kiuchezaji kulingana na mpinzani. Kwa hiyo, yoyote atakayekuja atapigwa,” amesema.

Wachezaji walioiwakilisha Mahakama katika mchezo huo ni ni Tatu Mawazo, Filomena Haule, Upendo Gustaf, Nyangi Kisangeta, Eunice Chengo, Sophia Songoro, Shan Ally na Agness Mwanyika.

Waliokuwa kwenye mbao ndefu ni Nuru Nchimbi, Malkia Nondo, Talita Kayuli na Ruth Kibona, huku benchi la ufundi likiongozwa na Mwalimu Paul Mathias na Naibu Katibu Mkuu wa Mahakama Sports Theodosia Mwangoka.

Katika hatua nyingine, kabumbu lililokuwa lichezwe leo tarehe 6 Octoba, 2023 katika uwanja wa Mkwawa kuwakutanisha Mahakama Sports Mpira wa Miguu na TARURA limeahirishwa kutokana fujo za wachezaji wa timu ya Ardhi ambayo imeondolewa kwenye mashindano kwa kuchezesha mamluki.

Mechi hiyo ambayo ilikuwa imepangwa kuchezwa majira ya saa 2:00 asubuhi ilishindwa kuendelea baada ya wachezaji hao wa Ardhi kukataa kutoka kwenye uwanja, huku Viongozi wao wakidai kuwa hawajapokea barua kutoka SHIMIWI kuhusu uamuzi wa kuondolewa kwenye mashindano.

Wakati fujo hizo zinatokea, tayari waamuzi walishafanya ukaguzi wa timu zote mbili ili kuruhusu mtanange huo ambao ungechezwa ili kumtafuta mshindi atakayetinga katika hatua ya robo fainali.

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli hii hapa, ni miamba kweli kweli wa kutupia vikapu.

Mashambuli ya kutupia kikapu huanzia hapa kwa Eunice Chengo.

Eunice anaitupa pasi ya mashambuli kwa Agness Mwanyika.

Agness anaitupa kwa Upendo Gustaf.

Upendo anatupa pasi kwa mtupiaji hatari Philomena Haule.

Philomena badala ya kutupia anairudisha kati kwa Nyangi Kisangeta, naye anautuliza mpira ili kuwapa nafasi watupiaji kujiweka sawa.

Nyangi anaitupa kwa mtupiaji kinara, Tatu Mawazo.
Mtupiaji Tatu anatupia mpira langoni.
Mpira huoooo unatumbukia.
Mashabiki wa Mahakama Sports wanamwagika uwanjani kwa shangwe kushangilia.

Bendera ya Mahakama inapepea baada ya mchezo kumalizika.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni