Jumamosi, 7 Oktoba 2023

MAHAKAMA KANDA YA MTWARA KWENDA KIDIJITALI KWA ASILIMIA 100

Na. Richard Matasha-Mahakama, Mtwara

Mahakama ya Tanzania Kanda ya Mtwara hivi karibuni imeendesha mafunzo kwa watumishi ili kuwajengea uelewa kuhusu mfumo wa usimamizi na uendeshaji mashauri.

Mafunzo hayo yaliyokuwa yanafanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Ebrahim alisema, “Tuhakikishe kila mmoja wetu anashiriki kwa kufungua akili na mawazo yake, tuwe tayari kujifunza muda wote na kuwafundisha wananchi.”

Alisema kuwa matumizi sahihi ya mfumo huo yataboresha huduma za kimahakama, hivyo akawasihi kutembea na ndoto ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ili kuhakikisha Mahakama ya Kidijitali inawezekana.

Mafunzo hayo ni mahsusi kwa ajili ya kujianda na ujio wa mfumo mpya wa kusimamia na kuendesha mashauri kidijitali ambao unatarajiwa kuanza kutumika mwanzoni mwa mwezi Novemba, 2023.

Mkufunzi Mkuu wa mafunzo hayo alikuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Fredrick Lukuna akishirikiana na Afisa Tehama wa Kanda hiyo, Bw. Richard Matasha.

Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi Mtwara na Lindi, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya katika Mikoa ya Lindi na Mtwara, baadhi ya Mahakimu Wakazi na watumishi wengine wa Mahakama walishiriki kwenye mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo hayo walipongeza uongozi wa Mahakama kwa hatua kubwa ya maboresho hayo na wameahidi kujitoa kwa hali na mali ili kuendana na kasi hiyo inayoendelea kufanyika ndani ya Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Bw. Richard Mbambe (aliyesimama) akitoa maelezo ya utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi kufungua mafunzo hayo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim akizungumza na washiriki wa mafunzo hayo.
Naibu Msajilii wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Fredrick Lukuna (mbele kulia) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava wakisikiliza kilichokuwa kinajiri wakati wa mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, Mhe. Consolatha Singano (wa kwanza kulia), akiwa na watumishi wenzake wa Mahakama Kanda ya Mtwara katika mafunzo hayo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni