Jumamosi, 7 Oktoba 2023

MTENDAJI MKUU ATAKA MABADILIKO CHANYA KAMATI YA UKAGUZI YA MAHAKAMA

Na Evelina Odemba – Mahakama Morogoro

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka wajumbe wa Kamati ya Ukaguzi ya Mahakama kutumia vyema nyenzo walizokabidhiwa ili kuondoa hoja za ukaguzi ndani ya Mhimili huo.

Prof. Ole Gabriel alitoa wito huo jana tarehe 6 Oktoba, 2023 wakati akifunga mafunzo ya Kamati ya Ukaguzi ya Mahakama ya Tanzania ambayo yaliendeshwa katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.

Alisema kuwa amefarijika mafunzo hayo kuwa shirikishi kwa wakuu wa idara na vitengo ambao sio wajumbe wa kamati ya ukaguzi.

“Nimefahamishwa mmekabidhiwa nyenzo zitakazowasaidia kutekeleza majukumu yenu vyema. Kupewa nyenzo ni jambo moja lakini kusoma, kuelewa na kutumia ni jambo jingine ambalo ni binafsi. Ombi langu kubwa kwenu ni kuhakikisha tunatumia nyenzo hizo vizuri ili kuleta mabadiliko chanya,” alisisitiza.

Kadhalika, Mtendaji Mkuu alitilia mkazo matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuondoa hoja za ukaguzi, “TEHAMA inatusaidia kufanya tracking na kupata kile tunachotaraji...

“...Tukiweza kuzuia hoja za ukaguzi tutakuwa tumefanikiwa, utamaduni wetu baada ya haya mafunzo mazuri uwe ni kuzuia hoja za kikaguzi, natamani ifike sehemu Mahakama iwe ya mfano kwa kukosa hoja za ukaguzi,” alisema.

Awali, akisoma taarifa fupi ya mafunzo hayo, Katibu wa ya Ukaguzi ya Mahakama ya Tanzania, Bi. Agnes Bulyota alisema kuwa katika kipindi walichokuwa hapo wamefundishwa mambo mbalimbali, ikiwemo namna ya kuandaa taarifa ya ukaguzi.

“Mafunzo haya adhimu yametolewa kwa wajumbe wa kamati, wakuu wa idara pamoja na vitengo vyote vya Mahakama ya Tanzania. Mafunzo haya yametuwezesha kujenga uelewa wa pamoja katika kumshauri afisa masuhuli na kuiwezesha Mahakama kutimiza malengo yake ya kimkakati katika utoaji haki kiufanisi,” alisema.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya Kamati ya Ukaguzi ya Mahakama.
Katibu wa Kamati ya Ukaguzi ya Mahakama ya Tanzania, Bi Agnes Bulyota akisoma taarifa fupi kwa mtendani Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani).
Wajumbe wa mafunzo ya Kamati ya Ukaguzi ya Mahakama (juu na chini) wakifuatilia mambo mbalimbali wakati wa ufungaji wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji wa mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa mafunzo hayo (juu na chini).

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa sekretarieti ya mafunzo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni