Jumanne, 10 Oktoba 2023

MAAFISA WA MAHAKAMA WAPIGWA MSASA MASHAURI YA WANYAMA PORI

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Katika jitihada za kulinda na kuhifadhi rasilimali za wanyamapori nchini Tanzania, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la PAMS, kimetoa mafunzo kwa Maafisa wa Mahakama ya namna ya kushughulikia mashauri ya kesi za wanayamapori na maliasili kwa ufanisi zaidi.

Mafunzo hayo yaliyofunguliwa jana tarehe 9 Oktoba, 2023 mjini Morogoro yamelengwa kuwafikia maafisa 157.

Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapha Mohamed Siyani, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor alisema kuwa Mahakama imeweka jitihada za kuhakikisha Majaji na Mahakimu wanaondokana na makosa ya kiufundi yanayopelekea majangili kuachiwa huru au kutopewa adhabu stahiki.

Alisema Mahakama imekuwa ikiwashughulikia majangili wakiwemo majangili wa meno ya tembo na nyara za serikali ambao mara wanapofikishwa Mahakamani na kupatikana na kosa adhabu yake huwa ni kuhukumiwa na kifungo chake huwa ni miaka 20 na fidia kwa Serikali.

“Lakini kuna baadhi ya kesi ambazo hazijapelelezwa, vizuri hivyo unakuta jangili anatoka kwa ajili tu kuna makosa ya kiufundi katika upelelezi, sasa hilo ndio tunalipatia mwarobaini kupitia mafunzo haya” alisema Mhe. Mansoor.

Kadhalika alisema mafunzo hayo yatawapa uelewa wa kutosha na kufanya ustawi wa wanyamapori na misitu kushamiri huku Wafadhili Pams Foundation na Chuo cha uongozi wa mahakama (IJA) wakijitahidi kupeleka elimu kwa watendaji wanaotakiwa kulinda wanyamapori, misitu na mazingira waliyorithi kutoka kwa mababu zao.

Alisema kuna juhudi kubwa zinafanywa na Shirika la uhifadhi Tanzania (TANAPA) na Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA) kuhifadhi aina za wanyamapori zilizopo kwenye hatari ya kupotea ikiwemo Nyati.

Naye Mkurugenzi wa mafunzo ya kimahakama kutoka Chuo cha Uongozo wa mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Patricia Kisinda alisema wanatarajia kutoa mafunzo hayo kwa maafisa wa mahakama zaidi ya 757 kutoka mikoa mbalimbali nchini ambapo wameanza na mikoa mitano ukiwemo Morogoro, Mtwara, Lindi, Dar es salaam na Pwani.

Kisinda alisema wameamua kugusa wanyamapori na maliasili sababu ni eneo nyeti katika uchumi wa nchi sambamba na kuwepo kwa changamoto nyingi katika uendeshaji wa mashauri ya wanyamapori mahakamani na baada ya tathmini ya mafunzo yaliyopita wameona kuna tija.

Naye Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la PAMS Foundation Samson Kasala alisema katika kushirikiana na serikali na wananchi kuhamasisha kuelewa umuhimu wa maliasili wanafanya kazi kwa Pamoja kuhakikisha kwamba majangili, waporaji, wanaohusika katika kutenda makosa ya jinai wanashughulikiwa na mkono wa sheria.

Naye Wakili wa Serikali ofisi ya mashtaka taifa mkoa wa Pwani Clarence Mhoja anasema mafunzo hayo yatawasaidia kufikia hatua nzuri ya kupeleka jalada mahakamani pale wenzao wa ukamataji na upelelezi wanapotekeleza kazi zao kwa mujibu wa sheria.

Mafunzo hayo yaliyozinduliwa leo tarehe 9 Oktoba, 2023 yanatarajia kuhitimishwa tarehe 13 Oktoba, 2023 yamewashirikisha wahe. Majaji wa Mahakama kuu, Mahakimu, waendesha mashataka na wapelelezi ambao kwa Pamoja watajengewa uelewa wa namna ya kushughulikia mashauri hayo hii ikiwa ni kundi la awamu ya kwanza linalotegemea kuwafikia maafisa 157.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor akizungumza wakati akifungua mafunzo ya wanyamapori na maliasili.
Meza kuu wakati wa kufungua mafunzo ya namna ya kushughulikia mashauri ya wanayamapori aliyeketi wa pili kulia ni mgeni rasmi ambaye pia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor akifuatiwa kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe Rose Ibrahim,wa kwanza kushoto ni mratibu wa Mafunzo Mhe. Ellimo Masawe na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi wa mafunzo ya kimahakama kutoka Chuo cha Uongozo wa mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Patricia Kisinda.

Washiriki wa mafunzo wakifuatilia hotuba ya ufunguzi toka kwa mgeni rasmi Mhe. Latifa Mansoor Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro (hayupo pichani) waliokaa mbele ni majaji toka kanda mbalimbali za Mahakama ya Tanzania ambao pia ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo ya namna ya kushughulikia mashauri ya wanayamapori wakifuatilia wakati wa utambulisho.

Washiriki wa mafunzo.
Meza kuu ikiongozwa na Mgeni rasmi Mhe. Latifa Mansoor (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya Pamoja na waendesha mashtaka wa serikali ambao ni sehemu ya washiri wa mafunzo.
Meza kuu ikiongozwa na Mgeni rasmi Mhe. Latifa Mansoor (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya Pamoja na wahe. Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Meza kuu ikiongozwa na Mgeni rasmi Mhe. Latifa Mansoor (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya Pamoja na wahe. Mahakimu ambao ni sehemu ya washiriki wa mafunzo.

Meza kuu ikiongozwa na Mgeni rasmi Mhe. Latifa Mansoor (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya Pamoja na waendesha mashtaka wa Tanapa ambao pia ni washiriki wa mafunzo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni