Ijumaa, 13 Oktoba 2023

MAFUNZO KESI ZA WANYAMAPORI, MALIASILI HAYAJAACHA KITU

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Mafunzo ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanayamapori, ikiwemo ujangili yanayoendelea mjini Morogoro yanazidi kupamba moto baada ya Majaji jana tarehe 12 Oktoba, 2023 kushika usukani na kutoa darasa la namna bora ya uandishi wa hukumu.

Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama kwa kushirikiana na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya PAMS Foundation yamezidi kuwajengea uwezo wadau wote katika myororo wa utoaji haki nchini.

Mbali na washiriki toka Mahakama ya Tanzania ambao ni  Majaji na Mahakimu lakini pia kuna waendesha mashtaka wa serikali pamoja na wapelelezi ambao wote kwa pamoja wamekutana ili kuongeza ujuzi katika utendaji kazi.

Akitoa elimu ya uandishi bora wa hukumu, mwezeshaji ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Mustafa Ismail alisema kuwa ni vyema wahakikishe kile wanachokiandika katika hukumu zao kinawabainisha wao ni nani, uelewa wao na hata namna ya kuchanganua mambo.

“Sio watu wote wamepewa mamlaka ya kuhukumu, hivyo basi sisi tuliokasimiwa mamlaka haya tufanye kazi kwa heshima kubwa na itubainishe ujuzi wetu,” alisema.

Washiriki wa mafunzo hayo yaliyowajumuisha wadau 157 waligawanywa katika makundi matatu ambapo kundi la kwanza lilipigwa msasa na Mhe. Ismail, kundi la pili lilinolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahimu wakati katika kundi la tatu, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Dkt Deo Nangela aliwafunda vyema washiriki hao.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwezile alifundisha washiriki hao kwa njia ya mtandao (Video Conference) akiwa kwenye kituo chake cha kazi na kueleza kwanini adhabu za vifungo zinatolewa, kanuni mbalimbali za adhabu na namna ya utoaji wa adhabu hizo.

Mwezeshaji ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Mustafa Ismail akitoa somo juu ya namna ya kuandika hukumu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahimu akiwanoa washiriki juu ya somo la namna ya kuandika hukumu.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Dkt Deo Nangela akiwafunda washiriki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akifundisha kwa njia ya mtandao (Video Conference) akiwa huko Kigoma huku washiriki wakifuatilia kama inavyoonekana pichani.

Naibu Msajili, Mhe. Ellimo Masawe ambaye pia ni mratibu wa mafunzo akiongea na washiriki kabla ya kuanza kwa darasa kwa njia ya video.

Washiriki wakifuatilia darasa kwa njia ya Video Conference (juu na chini).

  (Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni