Jumamosi, 14 Oktoba 2023

MAFUNZO YA UENDESHAJI MASHAURI YA WANYAMAPORI, MALIASILI YAHITIMISHWA

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Mafunzo yaliyokuwa yanaendelea mjini hapa kuhusu uendeshaji wa mashauri ya makosa ya wanyamapori na maliasili yamehitimishwa jana tarahe 13 Oktoba, 2023.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba alisema wakati anahitimisha mafunzo hayo kuwa, mafunzo hayo yaliandaliwa ili kukabiliana na changamoto za ushahidi hafifu ambao   wakati mwingine unapelekea mshitakiwa kuachiwa huru.

Alisema kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuwajengea uwezo maafisa wa Mahakama, wapelelezi pamoja na waendesha mashtaka ili wote wawe na ufahamu wa kutosha kuhusiana na sheria husika.

Mhe. Chaba alisema pia kuwa mafunzo hayo yaliandaliwa ili washiriki kuwaongezea ujuzi na maarifa katika kuyashughulikia mashauri hayo kulingana na nafasi zao katika mnyororo wa utoaji haki hapa nchini.

Aidha, Jaji Chaba aliwaasa washiriki wa mafunzo hayo kufanya kazi kwa kuzingatia taaluma zao na kuhakikisha kwamba wanafanya kazi kwa weledi mkubwa katika utendaji wao wa kazi.

Aliwataka washiriki wote wajenge utamaduni wa kushirikiana na wadau wengine muhimu katika maeneo yao ya kazi na watumie nafasi walizonazo kujiendeleza kitaaluma ili kujifunza mambo mapya na kujiimarisha zaidi kiutendaji.

Kadhalika, Kaimu Jaji Mfawidhi aliwahimiza kuhakikisha wanazingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuboresha utendaji wa kazi zao.

“Katika mafunzo haya, nimejulishwa kuwa wamekuja wataalamu wabobezi na na wakufunzi mahiri ambao wametoa mafunzo mahsusi kuhusiana na uendeshaji wa mashauri ya makosa ya wanyamapori na maliasili. Ninaamini washiriki wote tumepata msingi mzuri wa upelezaji, uendeshaji na usikilizwaji wa mashauri ya wanyamapori.

“Mkumbuke kwamba, uendeshaji wa kesi yeyote ile hauna tofauti na ujenzi wa nyumba ambapo huhitaji msingi ulio madhubiti ili kuhimili misukosuko yoyote. Hivyo, mashauri yanayohusu wanyamapori yanahitaji wapelelezi kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa, umakini wa hali ya juu sambamba na kushirikiana na wadau muhimu,” alisema.

Mhe. Chaba alisema waendesha mashtaka nao wanapaswa kuhakikisha mashauri ya aina hiyo yanaendeshwa kitaalamu na kwa weledi mkubwa kwa kuwa ushahidi thabiti unaotolewa mahakamani ndiyo kitu pekee kinachoifanya Mahakama kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Hivyo, alisema suala la upelelezi na uendeshaji wa mashauri ya aina hiyo ni muhimu katika utendaji wa haki kwa nafasi ya wapelelezi na waendesha mashtaka.

“Endapo upelelezi utafanyika chini ya kiwango na kuwa dhaifu, ni vigumu zaidi kwa waendesha mashtaka kuthibitisha kosa pasi na shaka yeyote mahakamani na Mahakama kwa upande wake, haziwezi kutenda miujiza kutokana na shauri husika kupelelezwa na hatimaye kufikishwa mahakamani wakati ushahidi uliotolewa ni dhaifu au hafifu,” alisema Jaji Chaba.

Mhe. Chaba alisema kuwa anaamini mafunzo hayo yamewanoa ipasavyo washiriki wote ambao idadi yao ilikuwa 160 na sasa wanakwenda kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi zaidi ili kupunguza mauaji ya wanyamapori ambazo ni nyara za Taifa.

Alisema, anaamini pia kwamba, washiriki wote wamemaliza mafunzo yako kwa ufanisi mkubwa na kwamba wanaondoka wakiwa na ujuzi tofauti na walivyofika kuhudhuria mafunzo hayo. Aliwaeleza washiriki kuwa alivutiwa na mafunzo hayo kwa kuwa yalihusisha pia somo la maadili katika utumishi wa umma.

Aidha, alisema kuwa Mahakama ya Tanzania katika kutekeleza mpango mkakati kupitia nguzo ya tatu, imeweza kuandaa mafunzo hayo kwa kuwashirikisha wadau katika sekta ya upelelezi na waendesha mashtaka ikishirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na wadau wengine (PLMS Foundation) katika kuwanoa maafisa wa Mahakama na wadau wengine.

Naye Mratibu wa Mafunzo hayo, Mhe. Elimo Masawe alisema kuwa mafunzo hayo yamefanikiwa kuwakutanisha wadau wa haki jinai, kugawana uzoefu na kujadiliana changamoto wanazokutana nazo mara kwa mara katika utendaji kazi kuhusiana na mashauri ya wanyamapori.

Alisema mada 17 zimefundishwa ambazo ziligusia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupata taarifa ya uhalifu tangu siku inapotolewa mpaka siku ya mwisho ambapo adhabu hutolewa na Mahakama kwa mujibu wa sheria.  

Mhe. Masawe alisema kuwa, mafunzo hayo yamekidhi kiu ya washiriki pamoja na kuangalia njia sahihi za kutanzua changamoto kubwa zilizopo wakati wa upelelezi, uendeshaji na usikilizwaji wa mashauri ya wanyamapori.

Alisema anaamini ujuzi walioupata washiriki katika mafunzo hayo, yataongeza ari na kasi ya ushughulikiaji wa mashauri hayo na hasa ikizingatiwa kuwa uhalifu unabadilika mara kwa mara kulingana na teknolojia inavyobadilika.

“Hivyo wapelele lazima wawe na ujuzi wa namna ya kuchunguza uhalifu unaofanyika kwa kutumia teknolojia, jinsi ya kukusanya ushahidi kwa misingi ya sheria na jinsi ushahidi utakavyotolewa Mahakamani. Tusipopeana ujuzi wa kutosha waalifu watatuacha mbali,” alisema.

Alisema kuwa kesi ya uhalifu wa wanyamapori hata ikiwa moja ni tatizo kubwa kwani mhalifu anapokamatwa na sehemu yeyote ya kiungo cha mnyama ni ishara kuwa mnyama ameuwawa.

Mafunzo hayo yaliyofunguliwa tarehe 9 Oktoba, 2023 mjini hapa, yametolewa kwa washiriki 160 kutoka Mahakama ya Tanzania, Wapelelezi na Waendesha mashtaka wa Serikali na yanategemewa kutolewa kwa awamu nyingine.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.

Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la PAMS Foundation, Bw. Samson Kasala akizungumza wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo.

Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuhitimishwa kwa mafunzo ya mashauri ya wanyamapori na maliasili mjini Morogoro.

Mratibu wa Mafunzo hayo, Mhe. Ellimo Massawe akuzungumza wakati wa kufunga.

Washiriki wakikabidhiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo hayo (juu na chini).

Washiriki (juu na chini) wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa kufunga mafunzo hayo.

 (Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Iringa) 

 

 

 

 

  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni