Ijumaa, 20 Oktoba 2023

MAHAKAMA MOROGORO YAFUNGA VIFAA VYA MTANDAO KWENYE MAGEREZA

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Kufuatia maboresho katika upande wa matumizi ya Tekinolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yanayofanywa na Mahakama ya Tanzania, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro imefanikiwa kufunga vifaa vya kisasa vya mtandao kwenye Magereza ya Kilosa na Mahenge.

Vifaa hivyo vilifungwa na Kaimu Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro Tofiki Sumbuo ili kurahisisha usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (Video Conference) kupitia mfumo wa Mahakama wa http://virtualcourt.judiciary.go.tz.

Akipokea vifaa hivyo, Mkuu wa Gereza la Kilosa Deodatus Kazinga aliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuwarahisishia utoaji huduma na kuwapunguzia gharama za kumsafirisha Mahabusu toka Magereza hadi mahakamani.

“Tunashukuru kwa Mahakama ya Tanzania, hakika wameturahisishia shughuli ya utoaji huduma, wakati mwingine tulikuwa tunapitia katika mazingira magumu ya kumsafirisha Mahabusu, hususani katika mashauri ya ugaidi kutoka hapa Magereza kwenda mahakamani umbali wa kilomita saba,” alieleza.

Naye Afisa TEHAMA wa Kanda Said Tamimu alisema kwa upande wa Mahakama Morogoro tayari wamefanikiwa kufunga vifaa vya kusikilizia mashauri kwa njia ya mtandao katika Magereza manne ya Kibelege huko Ifakara, Gereza la Mahabusu lililoko Morogoro Mjini, Gereza la Kilosa na Gereza la Mahenge.

Alisema kuwa kufungwa kwa vifaa hivyo kutarahisisha usikilizaji wa mashauri, ikiwemo kuondoa hatari inayoweza kujitokeza wakati wa kumsafirisha mahabusu toka gerezani hadi mahakamani, mfano kwenye mashauri yanayohusisha mashtaka ya ugaidi.


Mkuu wa Gereza la Kilosa Deodatus Kazinja (kulia) akipokea kutoka kwa Kaimu Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Bw. Tofiki Sumbuo nyaraka za makabidhiano ya vifaa vya mtandao kwa ajili ya usikilizaji wa mashauri.

Majaribio ya matumizi ya Video Conference kutoka katika Gereza la Kilosa baada ya vifaa hivyo kufungwa.

Kaimu Afisa TEHAMA kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Bw. Tofiki Sumbuo (kulia) akikabidhi vifaa vya Video Conference kwa Askari wa Gereza la Mahenge.

Vifaa vya Video Conference vilipowasili katika Gereza la Kilosa na kupokelewa na Mkuu wa Gereza Deodatus Kazinja (kushoto). Kulia ni Kaimu Afisa TEHAMA kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Bw. Tofiki Sumbuo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni