Ijumaa, 6 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAUME, WANAWAKE MOTO

·Zatinga robo fainali kibabe

·Tume ya Uchaguzi, Mifugo wasurubishwa, wafungasha virago

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu za Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Kamba Wanawake zimefanikiwa kuingia robo fainali kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI)yanayofanyika mkoani hapa baada ya kuzisurubisha timu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Mifugo.

Michezo yote mawili katika hatua ya mtoano ya 16 bora imechezwa leo tarahe 6 Octoba, 2023 katika viwanja vya Mkwawa. Ulikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza ambapo Mifugo walionekana kujiamini, hasa baada ya mashabiki kuwashangilia wakati wanaingia uwanjani. 

Hata hivyo, kibao kiliwageukia Mifugo wakati mchezo ulipoanza baada ya Mahakama Sports kuwasurubu na kupokea kichapo katika mvuto wa kwanza. Utoaji wa vichapo uliendelea pia katika hatua ya pili ambapo Mahakama Sports haikuwa na huruma na mtu na kufanikiwa kuwaondoa Mifugo kwenye mashindano baada ya kuzoa pointi zote mbili. 

Baada ya mchezo huo kukamilika ilifuata Kamba Wanaume ambapo Mahakama Sports ilipangwa kuchakachuana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Tume waliingia kwenye mchezo wakiwa hawana amani, hasa baada ya kuiona miamba ya Mahakama ikiwa imesimama imara. 

Katika mivuto yote miwili, Mahakama Sports iliwasambaratisha Tume na kujikuta wanalambishwa nyasi baada ya kujaribu kuleta upinzani kwa magwiji hao wa mchezo wa kamba nchini. 

Kufuatia matokeo, timu zote mbili za Mahakama Sports Kamba Wanaume na Kamba Wanawake zinatangulia robo fainali, hivyo kuzifanya timu pinzani Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Mifugo kuyaaga mashindano. 

Akizungumza baada ya michezo hiyo miwili, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema kazi ndiyo imeanza. Amesema kila timu watakayokutana nayo katika hatua ya mtoano itapokea kichapo kikali.

"Sisi ni watoa haki, hivyo hatupendelei mtu yoyote, hivyo kwetu sisi vichapo ni vya kila mtu. Kuna watu walikuja na vidomodomo, tayari tumeshavikata. Kwa hiyo, yoyote atakayekuja ajiandae kabisa kuchezea kichapo, tutambamiza mtu yoyote atakayejipendekeza," amesema. 

Mahakama Sports imepeleka timu nne kwenye hatua ya 16 bora baada ya kufanya vizuri kwenye makundi. Michezo hiyo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Netiboli na Mpira wa Miguu Wanaume.

Timu ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi wakilamba nyasi baada ya kupokea kichapo kutoka kwa timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume. Picha chini Mahakama Sports ikiwasambaratisha wapinzani. 

Wanawake wa shoka wakitoa dozi. 
Timu ya Mifugo Kamba Wanawake wakisurubishwa. Wako taabani.
Waamuzi wakiweka kamba sawa kabla ya mchezo. 
Wachezaji wa Mahakama Sports na Tume ya Taifa ya Uchaguzi wakipongezana baada ya mchezo. 
Timu za Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Kamba Wanawake pamoja na mashabiki wake (juu na chini) zikishangilia baada ya kutinga robo fainali.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni