Jumatano, 11 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAUME, WANAWAKE ZATANGULIA FAINALI

·Viwanda wanaume naye aburutwa

·Ras Kagera wanawake ulimi nje

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu za Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Kamba Wanawake zimetangulia fainali kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Mahakama Sports Kamba Wanaume wamewabamiza Viwanda, huku Wanawake wakitoa kipigo kikali kwa Ras Kagera. Michezo yote miwili imechezwa saa 12:30 asubuhi katika viwanja vya Mkwawa.

Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Utawala wa Mahakama ya Tanzania, Stephen Magoha ameshuhudia michezo hiyo na kupongeza vijana wake kwa ushindi mnono walioupata. Amewatia moyo kuendelea kupambana ili kunyakua makombe yote. 

Ulikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza kuchezwa huku Ras Kagera wakijaribu kuonyesha upinzani katika sekunde za mwanzo na kujipa matumaini kuwa wangeweza kushinda mchezo huo.

Kumbe ilikuwa danganya toto bwana, kwani Mahakama Sports walikuja juu na kuwasambaratisha vibaya wapinzani hao katika mvuto wa kwanza, hivyo kujihakikishia pointi moja.

Katika mvuto wa pili, Ras Kagera walionekana kutepeta na baada ya kushushiwa kipigo kikali walipoteana na kupoteza mpambano huo. Hadi mwisho wa mchezo ambao haukuchukua muda mrefu, Mahakama Sports ikaondoka na pointi zote mbili.

Baada ya mchezo huo kukamilika, ilifuata Kamba Wanaume ambapo Mahakama Sports iliwapigisha chafya Viwanda baada ya kuwapelekea pumzi ya moto na kutoa kichapo cha mwizi wa bata, hivyo kupoteza mchezo katika mivuto yote miwili.

Katika mchezo huo, Viwanda waliingia uwanjani wakiwa wamejiamini kwa nia ya kuwaaibisha Mahakama Sports. Hata hivyo, baada ya mchezo kuanza walikumbana na upinzani mkali na kuburutwa walipojaribu kujitutumua.

Kufuatia matokeao hayo, Mahakama Sports Kamba Wanaume watakutana na pacha wake, watoto wa Baba mmoja, Ikulu ambao wametinga katika hatua hiyo baada ya kuwang’oa Uchukuzi, huku Wanawake wakikutana na Uchukuzi ambao wamewashinda Ras Iringa kwa taaabu.

Katika michezo ya leo, Kamba Wanaume iliundwa na Leonard Kazimzuri, Joseph Chokela, Cletus Yuda, Luyuga Luyuga, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Abdulmumin Mbaraka, John Charles, Kumbukeni Mtete na Martin Mushi.

‘Super Sub’ walikuwa Hemed Semith, Emmanuel Dasian, Ashel Chaula, Willy Mwaijibe, Mussa Komba na Marko Mochiwa.

Kwa upande wa Kamba Wanawake walikuwepo Judy Mwakyalabwe, Zahara Suleiman, Beatrice Dibogo, Melina Mwinuka, Rebeca Mwakabuba, Tumaini Kizito, Namweta Mcharo, Joyce Simba, Sarafina Mkumbo na Mariam Mayalla.

Waliosimama kwenye mbao ndefu walikuwa Winiel Mahumbuga, Witness Lyasato, Veronica Rajabu, Eunice Lugiana na Janeth Mapunda.

Timu zote zipo chini ya Viongozi wa Mahakama Sports ambao ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Robert Tende, Naibu Katibu Theodosia Mwangoka na Mweka Hazina Rajab Ally.

Wengine ni Meneja wa Timu Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile, Mjumbe Rajabu Mwaliko na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole.

Mkiambiwa msicheze na Mahakama mtaumia, muwe mnasikia. Viwanda walikuja kuidhalilisha Mahakama, wamedhalilika wao, wameburutwaah.
Jamaa wa timu ya Viwanda wakijikusanya kusanya baada ya kuburutwaah.
Miamba hii hapa, Mahakama Sports Kamba Wanaume. Hapa (juu) timu ikiwa chini kusikilizia. Picha chini timu imenyanyuka juu na ikinyanyuka na kushuka ujue mtu anaburutwa.

Miamba mingine hii hapa, Mahakama Sports Wanawake, wanahatari hao, we acha tu. Picha chini ni timu ya Ras Kagera wanawake wakiugulia maumivu baada ya kupata kichapo kikali.

Mwamuzi akijiandaa kuanzisha mchezo.
Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Utawala wa Mahakama ya Tanzania, Stephen Magoha (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja na timu ya Kamba Wanawake.
Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Utawala wa Mahakama ya Tanzania, Stephen Magoha (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja na timu ya Kamba Wanaume.

Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Utawala wa Mahakama ya Tanzania, Stephen Magoha (katikati) pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Sports wakiwa katika picha ya pamoja na timu ya Netiboli ambayo inajiandaa kuwapasua Ikulu leo majira ya jioni.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni