Jumanne, 3 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAUME YATINGA 16 BORA KIBABE

·Yaitifua tifutifu Ardhi

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume imekamilisha kibabe michezo yake katika kundi A kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Katika mchezo wake wa mwisho, Mahakama Sports imeitifua Ardhi, hivyo kukwea kileleni mwa kundi hilo lililoshirikisha timu zingine nne, ambazo zote zimepokea vichapo vikali.

Mchezo huo ambao ulichezwa majira ya saa 12.30 asubuhi haukuwa na upinzani wowote kwani Ardhi waliingia uwanjani wakiwa na hofu, hasa baada ya kuiona mibuyu ya Mahakama ambayo haikuwa na utani na mtu.

Kabla ya mchezo kuanza, mashabiki waliofurika uwanjani waliwaombea Ardhi msamahaha kwa Mahakama ili nao wapate angalau hata pointi moja. Hata hivyo, waamuzi alipoamuru mchezo huo kuanza, Mahakama haikuwa na utani na mtu.

Ardhi alichezea vichapo vikali katika mivuto yote miwili, hivyo kuiwezesha Mahakama kuibuka kidedea na kushika nafasi ya kwanza kwenye kundi hilo. Mahakama imeshinda mechi zake zote katika kundi A. Mbali na Ardhi, timu nyingine zilizopokea vichapo ni Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo.

Akizunguza baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza wanamichezo wote kwa kuwezesha timu zote nne, yaani Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Netiboli na Mpira wa Miguu, ambayo ina mechi moja mkononi, kwa kutinga hatua ya 16 bora.

"Kwa sasa macho na nguvu yetu tunazielekeza kwenye hatua inayofuata. Tutahakikisha tunapambana ili timu zetu zote zifanye vizuri kwenye michezo inayofuata. Ninachoomba tuendeleze ushirikiano na kudumisha nidhamu wakati wote ili lengo letu litimie,"amesema.

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu. 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede kabla ya mchezo dhidi ya Ardhi.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikitoa kipigo kwa wapinzani bila hata wasiwasi wowote. Wenzao wanaumia, yaani timu ya Ardhi (picha chini) wao wanaona hiyo ndiyo haki yao kwa leo.

Ardhi wamepata tabu sana kama unavyowaona.


Wababe hao wakijiandaa kumshughulikia mtu.

Shangwe kama lote baada ya Ardhi kukiona cha moto.
Ukisikia kamati ya roho ngumu ndiyo hawa, kila timu inapoenda na wao wanafuata kujionea jinsi mtu anavyoshughulikiwa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni