Jumanne, 3 Oktoba 2023

MAHAKAMA YAPEWA HESHIMA UFUNGUZI WA MASHINDANO SHIMIWI IRINGA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu imechaguliwa kucheza mechi ya ufunguzi wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa. 

Taarifa hiyo njema imetolewa na Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede katika kikao cha wanamichezo wa Mahakama kuwa ufunguzi rasmi wa mashindano hayo utafanyika kesho tarehe 4 Octoba, 2023 katika Uwanja wa Samora.

"Viongozi wa SHIMIWI wameipendekeza timu yetu kucheza mechi ya ufunguzi rasmi wa mashindano haya. Tutacheza na timu ya Kilimo majira ya mchana. Hii ni heshima kubwa kwetu na sisi Viongozi tumeipokea kwa mikono miwili," amesema.

Mwenyekiti amefafanua kuwa kuchaguliwa kwa Mahakama kucheza mechi hiyo kunatokana na nidhamu ya hali ya juu waliyoionesha katika michezo iliyopita. Hivyo akahimiza wachezaji kucheza kwa kuzingatia sheria zote ili watu wote watakaokuwa uwanjani waweze kufurahia mechi hiyo.

"Kutakuwa na watu wengi kwenye ufunguzi huu. Wanamichezo wote na watu wengine watakuwa wanatutazama sisi. Tuilinde heshima hii kwa kucheza vizuri na kuendelea kuonesha nidhamu...

“Viongozi wa SHIMIWI wameshaliona hilo na wanatupongeza sana kwa kudumisha nidhamu siyo tu kwenye kambi, lakini pia mahali pengine. Kadhalika, wametusifia kwa kuujulisha umma wa Wanairinga na Tanzania nzima uwepo wa mashindano haya," amesema. 

Hata hivyo, Dede amewahimiza vijana wake kwenda kupambana kwenye mchezo huo ili kupata ushindi, hatua itakayowawezesha kujiongezea pointi kwenye mashindano hayo.

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Sehemu ya Viongozi wakuu wa Mahakama Sports wanaosimamia maendeleo ya michezo katika Mahakama ya Tanzania.
Mwalimu Mkuu wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe (kulia) pamoja na Kocha Msaidizi wa Timu ya Mpira wa Miguu Said Albea ndio wanaowasaidia Viongozi wakuu katika michezo.
Nahodha wa Timu ya Mpira wa Miguu Devis Munubi (kushoto) na Nahodha Msaidizi Seleman Magawa wanaiongoza timu vizuri ili kupata ushindi kwa kila mchezo.
Miamba hiyo hapo ambayo imechaguliwa kusakata kabumbu kwenye ufunguzi rasmi wa mashindano.

Kuchaguliwa kwa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu kwenye ufunguzi huo ni heshima kwa Mahakama. Tuipeperusha vyema bendera hii kwa kuendeleza vichapo kwenye kila mchezo.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni