Jumanne, 3 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS NETIBOLI YAIKALISHA RAS MTWARA

·Yagawa dozi ya vikapu 50 kwa 8

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ya Netiboli imeendelea kuonyesha makali yake kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa baada ya kuibugiza Ras Mtwara vikapu 50:8.

Matokeo hayo yanaifanya Mahakama Sports kutinga katika hatua ya 16 bora baada ya kushika nafasi ya pili kwenye kundi G lenye timu tano. Timu ya Mahakama imekamilisha michezo ya hatuà ya makundi kwa kushinda michezo mitatu, huku ikipoteza mchezo mmoja kwa taaabu sana.

Katika mchezo huo, Ardhi walionufaika na upendeleo wa mwamuzi walishinda kwa ushindi mwembambna wa vikapu 23:21. Mchezo wa mwisho uliofanyika jana tarehe 2 Octoba, 2023 kwenye viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikristo Ruaha dhidi ya Ras Mtwara ulichezwa majira ya saa 11:00 jioni.

Katika mchezo huo, Mahakama Sports ililisakama mara kwa mara lango la wapinzani na tupia tupia za hapa na pale, zikiongozwa na Tatu Mawazo na Philomena Haule, ziliihakikishi timu hiyo kuondoka na ushindi. 

Hadi timu zote mbili zinaenda kwenye mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa inaongoza kwa vikapu 22 kwa 5. Katika kipindi cha pili, Mahakama Sports waliendelea kukaza uzi na kumiliki mpira kwa kiasi kikubwa, hatua iliyowawezesha kwenda kwenye lango la wapinzani mara wa mara. 

Kasi ya utupiaji vikapu iliongezeka katika kipindi hicho na kuwezesha Mahakama Sports kutumbukiza vikapu 28, huku Ras Mtwara wakiambulia vikapu 3 pekee. Hadi mwamuzi anapuliza kipenga kumaliza mchezo huo, Mahakama Sports ilikuwa imejizolea vikapu 50 kwa 8 walivyopata Ras Mtwara. 

Akizungumza baada ya mchezo huo, Mwalimu wa Timu Paul Mathias amesema hatua waliyofikia ni nzuri kwani wameshajihakikishia kufika katika hatua ya 16 bora. Aliwaomba vijana wake kuendelea kupambana katika hatua inayofuata ili kusonga mbele katika mashindano. 

Naye Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema wameshakamilisha lengo la awali la kuvuka katika hatua ya 16 bora, hivyo nguvu kubwa kwa sasa wanaielekeza kwenye hatua inayofuata na anaamini vijana wake wataendeleza vipigo hadi kunyakua kombe.

Wachezaji wanaoiwakilisha Mahakama katika mchezo huo ni ni Tatu Mawazo, Filomena Haule, Upendo Gustaf, Nyangi Kisangeta, Veronica Rajab, Eunice Chengo na Sophia Songoro. Waliokuwa kwenye mbao ndefu ni Nuru Nchimbi, Shani Ally, Rhoida Makassi, Malkia Nondo na Agnes Joseph.

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ya Netiboli kabla ya mchezo.
Mtupiaji hatari wa Timu ya Mahakama Sports ya Netiboli Filomena Haule (GA) akitupia moja ya kikapu kwenye lango la Ras Mtwara, huku mchezaji mwenzake, Upendo Gustaf (kushoto) akishuhudia.
Wachezaji wa Mahakama Sports (juu na chini) wakimiriki mpira.

Mashabiki wa Mahakama Sports (juu na chini) wakishangilia baada ya mpira kumalizika.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni