Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa
Timu ya Mahakama ya
Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu imekwea kileleni katika kundi A
kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali
(SHIMIWI) yanayoendelea mkoani hapa baada ya kuikandamiza Viwanda na Biashara
magori 7:0 katika mchezo uliojaa ufundi wa kila aina.
Iliwachukua dakika saba
tu ya mchezo kwa vijana wa Mhimili wa utoaji haki nchini kupachika bao safi
kupitia kwa kiungo bamia Frank Obadia baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Seif Shamte na
kuiandikia timu yake bao la kwanza.
Baada ya kwenda kambani,
Mahakama Sports iliendelea kulisakama lango la wapinzani na kufanikiwa kupata
bao la pili katika dakika ya saba ya mchezo kupitia kwa huyo huyo Frank Obadia
baada ya kupokea pasi murua kutoka kwa Seif Shamte kwa mara nyingine.
Kosa kosa za kupachika
mabao ziliendelea na ilipofika dakika ya 11 ya mchezo, kiungo hatari
aliyeonekana kuwa nyota wa mchezo huo, Selemani Magawa aliachia shuti kali na
kujaa wavuni, hivyo kuiandikia timu yake bao la tatu.
Mahakama Sports
hawakuishia hapo, kwani walizidisha mashambulizi na ilipofika dakika ya 24 ya
mchezo, mshambuliaji hatari Martin Mpanduzi alipokea pasi safi kutoka kwa beki kisiki Nasoro
Mwampamba na kuachia shuti lililomshinda mlinda mlango wa Viwanda na Biashara
na kujaa kwenye nyavu.
Baada ya kuingia kwa bao
hilo, timu ya Viwanda na Biashara ilionekana kuingia kwenye mfumo wa Mahakama
Sports na kuchezewa nusu uwanja muda wote. Katika dakika ya 28 ya mchezo, kiungo
Seleman Magawa alipachika bao la tano baada ya kupokea pasi kutoka kwa kiungo
mwenzake Obadia, ambaye alikuwa mwiba kwa timu pinzani.
Hadi kipindi cha kwanza
kinamalizika, Mahakama Sports ilienda kwenye mapumziko ikiwa na magori matano
kibindoni. Kipindi cha pili kilitawaliwa na kosa kosa nyingi kwa Mahakama
Sports kutokana na upepo mkali uliokuwa unavuma kwenda lango la Kaskazini la
Viwanda na Biashara.
Hata hivyo, baada ya
kutulia na kuanza kutandaza kandanda safi la kitabuni, dakika ya 47 ya mchezo
Nahodha wa Timu aliyeingia kutokea benchi, Devis Munubi alipachika bao na kuipatia timu
yake bao la sita.
Baada ya kosa kosa nyingi
za hapa na pale, Nahodha Msaidizi Seleman Magawa aliachia shuti kali katika
dakika ya 59 ya mchezo na kuweka mpira kwenye kamba, hivyo kuiandikia timu yake
bao la saba na la ushindi mnono.
Kuingia kwa bao hilo
kulimfanya kiungo huyo tegemezi kuondoka na mpira baada ya kupachika kwenye nyavu
jumla ya mabao matatu katika mchezo huo. Hii ni mara ya pili kwa timu ya
Mahakama kuondoka na mpita. Mara ya kwanza, mshambuliaji Mpanduji alifunga bao tatu
katika kipute kilichopigwa na timu ya Ras Kigoma, ambayo iliogelea jumla ya
magori nane kwa nunge.
Matokeo hayo yanaiweka
Mahakama Sports katika nafasi nzuri ya kutinga 16 bora baada ya kuzoa pointi
tisa ambazo imejikusanyia kufuatia kushinda mechi mbili kwa idadi kubwa ya
magori na kupata pointi nyingine tatu baada ya timu ya Maji kupokonywa ushindi
walioupata kwa taaabu baada ya kuchezesha mamluki.
Mwalimu wa Timu Spear
Mbwembwe amewapongeza vijana wake kwa kucheza vizuri na kumiliki mpira muda
wote wa mchezo, hivyo kuwafanya timu pinzani wasipate nafasi yoyote ya
kutengeneza mabao.
“Ninawashukuru sana,
mmecheza vizuri. Sasa tujipange kwa mechi ya mwisho ili tuendeleze ushindi,
hatutaki kupoteza mechi hata moja. Ninawaamini, mtafanya vizuri, kazi iendelee,”
amesema.
Naye Mwenyekiti wa
Mahakama Sports Wilson Dede amesema hakuna kurudi nyuma mpaka kieleweke. “Hatujamaliza,
kazi iendelee. Mwaka huu watatuelewa tu, wakichezesha mamluki tutapambana nao,
tunataka mchezo wa haki na haki lazima itawale mashindano haya. Safari hii
hatutakubali Bundi azengee mashindano,” amesema.
Wachezaji walioiwakilisha Mahakama ni Micheal Turuka, Nasoro
Mwampamba, Akida Mzee, Kelvin Muhagama, Frank Obadia, Gabriel Mwita, Martin
Mpanduzi na Seleman Magawa, Abdi Sasamalo, Mbura Minja, Iman Zumbwe, Rashid
Hamis, Devis Munubi na Gisbert Chentro.
Wengine walikuwa Seif Shamte, Nkuruma Katagira, Emmanuel Mwamole Fahamu
Kibona na Ramadhani Seif. Benchi la ufundi liliongozwa na Kocha Mkuu Spear
Mbwembe na Kocha Msaidizi Said Albea, Timu Meneja Shaibu Kanyachole, Meneja wa
Vifaa Eliya Ngule na Daktari Janeth Mapunda.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, timu ya
Mahakama Mpira wa Miguu imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara,
Maji, RAS Kigoma na Kilimo katika kutafuta nafasi ya kutinga 16 bora.
Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu,
ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao,
Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.
Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini
Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka
washindi katika michezo mbalimbali.
Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba
Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa
kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya
pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi
wa tatu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni