Jumatatu, 2 Oktoba 2023

MTAPIMWA NA WANANCHI KWA UWEZO WENU WA KUTENDA HAKI: JAJI MKUU

Na. Innocent Kansha – Mahakama, Lushoto

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewakumbusha Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania walioapishwa Septemba 14, 2023, kuwa wananchi watapima uwezo wao kwa kutenda haki na siyo vyeo walivyotunukiwa.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Majaji hao 24, ikiwemo wanne (4) wa Mahakama Rufani na 20 wa Mahakama Kuu , leo tarehe 2 Oktoba, 2023 katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mkoani Tanga ambapo mafuzo hayo yatafanyika kwa muda wa wiki tatu, Jaji Mkuu Mhe. Prof. Juma amesema, mwananchi hatajali Jaji husika ana uwezo gani wa elimu ama ana utaalam wa kiwango gani isipokuwa uwezo wako utapimwa kwa kiasi gani utaweza kutatua changamoto zao zinazowakabili wanapotafuta haki.

“Baadhi yenu mmesoma sana wengine shahada za uzamili, shahada za uzamivu kwa mwananchi anayetafuta haki hataangalia hizo shahada, yeye atafika kutafuta huduma tu, haangalii kama wewe ulikuwa ni profesa wa sheria, una udaktari wa sheria, haangalii kama kwenye hukumu yako utaandika we ni daktari au nani, yeye anachotaka tu ni hukumu inapotoka aisome aone kama inampa haki ili afanye uamuzi unaofuata”, amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma amesema, uwezo wa Jaji utapimwa kwa kiasi gani amejifunza katika mafunzo hayo elekezi, na namna gani atakavyokuwa anajitayarisha kila siku kusikiliza shauri lililo mbele yake, uwezo wa utoaji wa huduma wa Jaji utapimwa kila siku utakapokuwa unaingia mahakamani na kwa kila jalada utakalo kabidhiwa litatumika kukupima. Vilevile hata makarani utakaofanya nao kazi watakupima wakiona unaanza kulegalega huo ndiyo utakuwa ubuyu utakaokuwa unazungumzwa kwenye mabaraza na vijiweni

Mhe. Prof. Juma amewaambia Majaji hao kuwa wajitayarishe kufundiswa kazi na makarani, wao wote walifundishwa kazi na makarani hata maafisa wa jeshi wanafundishwa na wanajeshi wenye vyeo vya kawaida, sasa wale watu wa chini ndiyo wanafahamu taratibu zote za kila siku za mahakamani kuna mambo mengi sana mtajifunza kutoka kwao.

Kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Jaji Mkuu amesema, maboresho mengi ya muda mrefu hasa katika matumizi ya tehama. Mahakama inatumia sana mifumo ya tehama kuwajibishana, kupima utendaji na kuangalia kila hatua zinazofanywa na Maafisa wa Mahakama.

“Mimi siku zote huwa nawambia Majaji wapya kwamba, hakuna shimo unaloweza kijificha unapofanya kazi za kimahakama kwa sababu mifumo ya mtandao inaangalia mzigo wako wa mashauri kila siku, kama unaweka mashauri ya mlundikano utajulikana, kama wewe Jaji kazi yako ni kuhairisha mashauri utajulikana, kama wewe ni Jaji unayemaliza kusikiliza mashauri na husomi hukumu au unasoma hukumu hutoi nakala utajulikana na utafuatiliwa na ndiyo maana katika salamu zetu za Mahakama tunatumia sana uadilifu, weledi na uwajibikaji kwa sababu mfumo wetu mzima unahakikisha uwajibikaji”, amesisitiza Mhe. Prof. Juma.

Jaji Mkuu amesema, mfumo mpya wa kieletroniki wa kusajili, kusimamia na kuratibu mashauri ‘Advanced Case Management’ utaanza kufanyiwa majaribio leo tarehe 2 Oktoba, 2023 kwa kipindi cha mwezi mzima na utaziduliwa tarehe 1 novemba, 2023. Hivyo Mahakama inahama kutoka katika mfumo iliyokuwa ikiutumia kwa miaka kadhaa na kuanza kutumia mfumo wa kieletroniki wa kusajili na kusimamia mashauri ikiwa ni mfumo mama utakao tumika kuwafuatilia Maafisa wa Mahakama.

“Mfumo huu unatusaidia sisi kuhakikisha kwamba haki ambayo Katiba imewaahidi wananchi inapatikana ndani ya wakati, zama za matumizi ya majalada magumu, zama za majalada kupotea, zama za hukumu ambayo inasomwa lakini lakala hazipatikani itaisha kuanzia mfumo huu utakapo anza kufanya kazi”, ameongeza Jaji Mkuu

Kuhusu Maadili, Mhe. Prof. Juma amesema, ukisoma Kanuni za Maadili za Maafisa wa Mahakama ‘Code of Conduct for Judicial Officers’ zinasisitiza uwezo na ujuzi, kanuni hizo zinasema kwamba, uwezo ambao umewawezesha kuteuliwa kuwa Majaji au kuaminiwa kuwa Majaji wa Rufani na Majaji wa Mahakama Kuu, kanuni zinabainisha dkuendelea kuwa na uwezo huo huo bila kupungua.

“Kwa sababu uwezo ukipungua kanuni zinasema ni kigezo cha kuwaondoa kutoka katika kazi ya ujaji, kanuni hizo zimetamka kwamba hasa kanuni ya nne inaelekeza uwezo na umakini ‘Competence & Diligence’ uwezo mlionao mnapaswa kuendeleza”, amewambia Majaji hao.

Awali, Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Mhe Paul Kihwelo amesema, mafunzo kama hayo yanayoanza kutolewa kwa Majaji hao ni ya kundi la nane (8) na kwa upande wa Mahakama ya Rufani hilo ni kundi la nne (4) yakitolewa katika nyakati tofauti mara tu Mhe. Rais anapoteua kuwaapisha Majaji wapya toka kuanzia mwaka 2014 hadi sasa.

“Mhe. Jaji Mkuu ninaomba nikuhakikishie wewe binafsi pamoja na washiriki kwamba kama Chuo kwa kutumia uzoefu wa mafunzo yaliyotangulia tumejipanga vizuri uchaguzi wa wakufunzi pamoja na mada zitakazo tolewa zitakidhi kiu ya washiriki pamoja na kutimiza lengo la Mahakama na la Taifa, siku zote tunaamini Mahakama mafunzo yanatakiwa kujibu changamoto zilizopo na za baadaye”, amesema Jaji Kihwelo.

Mhe. Kihwelo amesema, mafunzo hayo yanalenga kuwajenga Wahe. Majaji kwa ajili ya Mahakama ya leo na Mahakama ya kesho. Mafunzo kwa yatakayo tolewa kwa washiriki wa Mahakama Kuu yatajumisha jumla ya mada 38 na wawezeshaji 41 watashiriki zoezi hilo kwa muda wa wiki tatu (3). Kwa upande wa washriki wa Mahakama ya Rufani kutatolewa mada tisa (9) na wawezeshaji sita (6) kwa muda wa wiki moja.

“Siku zote mafunzo ya Mahakama yanajikita katika maeneo matatu yaani mtazamo ama huluka, ujuzi na maarifa ‘ASK Attitude, Skills and knowledge’ ndiyo lengo la wawezeshaji wote waliopo na watakao kuja watagusa maeneo hayo”, amesema Jaji Kihwelo.

Naye, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akitoa neno la shukrani, amemshukuru Jaji Mkuu kwa kukubali kuwa mgeni rasmi na kufungua mafunzo hayo elekezi kwa Majaji hao.

“Mafunzo haya ya awamu hii ni ya kwanza na ya aina ya kipekee kwani kwa mara ya kwanza yamewajumuisha kwa pamoja Majaji wote wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu.”, amesema Mhe. Siyani.

Mhe. Siyani amesema mafunzo hayo yanaakisi sera ya mafunzo ya Mahakama na mpango wa utekelezaji wake na hivyo kuwa utamaduni kwa Chuo na Uongozi wa Mahakama kutoa mafunzo elekezi kwa watumishi wa kada mbalimbali ikiwemo Majaji wa ngazi zote.

“”Bila shaka uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani ni imani kubwa ambayo mamlaka ya uteuzi imeweka kwenu kwa niaba ya watanzania wapatao takribani milioni 61”, ameongeza Jaji Kiongozi.

Mhe. Siyani akatoa maelekezo kwa Majaji wa Mahakama kuu walioanza mafunzo elekezi mwaka 2021 jumla ya Majaji 21 walipatiwa mafunzo na wakapewa nafasi ya mafunzo kwa vitendo ambapo walipangiwa jumla ya mashauri 342 kati ya hayo mashauri 309 yalimalizika na ikumbukwe kuwa yale sio majaribio ya haki za watu, mtapaswa kwenda kutoa haki. Kiwango cha umalizaji mashauri kwa kwa mwaka huo ilikuwa asilimia 90.3 ufanisi huo ulitokana na kujengewa uwezo wa mafunzo kutokea Lushoto.

Mhe. Siyani ameongeza kuwa, mwaka 2022 kulikuwa na Majaji 22 wa Mahakama Kuu walioshiriki mafunzo elekezi na jumla ya mashauri 430 yalipangwa kwa Majaji hao na mashauri 402 sawa na asilimia 93 yalimalizika na asilimia 79 ya maamuzi hayo yalipandishwa kwenye Mfumo wa kielektroniki wa TanzLII

“Mwaka huu 2023 tumeandaa wastani wa mashauri mengine 400 yanayowasubiri Majaji wa Mahakama Kuu mara watakapo maliza mafunzo elekezi tuasubiri kuona kama mafanikio yaliyofikiwa na makundi yaliyopita yataendelezwa na Kundi hili lakini ni vema mkatambua baada ya kujengewa uwezo kuna matarajio ya matokeo makubwa mtakwenda kwenye vituo mtakavyopangiwa mkiwa mnakimbia kama askari wapya wenye nguvu”, amesisitiza Jaji Kiongozi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma  akifungua mafunzo elekezi ya Majaji hao 24, ikiwemo wanne (4) wa Mahakama Rufani na 20 wa Mahakama Kuu , leo tarehe 2 Oktoba, 2023 katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mkoani Tanga.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Majaji 24, ikiwemo wanne (4) wa Mahakama Rufani na 20 wa Mahakama Kuu , leo tarehe 2 Oktoba, 2023 katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mkoani Tanga.


Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Majaji 24, ikiwemo wanne (4) wa Mahakama Rufani na 20 wa Mahakama Kuu , leo tarehe 2 Oktoba, 2023 katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mkoani Tanga.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Mhe Paul Kihwelo akifafanua jambo wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo elekezi kwa Majaji
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akitoa neno la shukrani (Vote of Thanks) wakati wa hafla hiyo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na wanachama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA)


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na ambao awali kabla ya uteuzi na kuapishwa kuwa Majaji walikuwa Wasajili na Manaibu wasajili wa Mahakama Kuu. 


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania.


Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioanza mafunzo elekezi kwa muda wa wiki tatu chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya hafla hiyo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania walioanza mafunzo elekezi kwa muda wa wiki tatu chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni