Jumapili, 1 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAWAKE YAMALIZA KAZI

  • Yatangualia 16 bora
  • Tume ya Uchaguzi waula wa chuya

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake leo tarehe 1 Octoba, 2023 imefanikiwa kutinga kwenye hatua ya 16 bora kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa baada ya kuwatoa kamasi Tume ya Taifa ya Uchaguzi. 

Mchezo huo ambao umechezwa majira ya saa 12.30 asubuhi kwenye Viwanja vya Mkwawa ulianza kwa timu zote mbili kukamiana, huku Mahakama Sports ikithihirisha umahiri wake katika mivuto yote miwili.

Katika vipindi vyote viwili, Mahakama Sports haikuwa na huruma na mtu, hasa baada ya Tume ya Uchaguzi kujaribu kujitutumua, lakini walishindwa kuhimiri vishindo vya watoa haki nchini.

Hadi waamuzi wanamaliza mchezo huo, Tume ya uchaguzi walishatepeta, hivyo kuiwezesha Mahakama Sports kuzoa pointi zote mbili muhimu. Kufuatia matokeo hayo, timu ya Mahakama inakwenda moja kwa moja kwenye 16 bora.

Mahakama, ambayo ilikuwa katika kundi A imefikia hatua hiyo baada ya kushinda mechi zake zote ilizocheza na timu pinzani za Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ya pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Mahakama Sports Kamba Wanawake (juu) wakitoa kipigo kwa timu ya Tume ya Uchaguzi (chini).
Timu ya Tume ya Uchaguzi ikionja joto ya jiwe baada ya kujaribu kujitumua kupoambana na Mahakama Sports.
Timu ya Mahakama Sports Kamba Wanawake meno mje baada ya kuwanyonyoa wapinzani. Picha chini ikijiandaa kumchakaza mtu.

Mazoezi ya  mwisho mwisho kabla ya mchezo (juu na chini).


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni