Jumatatu, 2 Oktoba 2023

MDOMO MREFU SHIMIWI IRINGA WAKATWA

·Usicheze na Mahakama utaumia

·TAKUKURU ulimi nje, hawaamini kilichowakuta

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Mtoto akililia wembe mpe. Hiki ndicho walichokifanya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume kwa TAKUKURU kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea mkoani hapa.

Yalipoanza mashidano, TAKUKURU walianza kutamba mitaani kuwa wamekuja kwa kazi moja tu, kuiondosha Mahakama, tena katika hatua za awali, hasa kwenye mchezo wa kamba.

Siku ya kupanga makundi wakaonyesha dhahiri nia yao na kuchagua kuwa kwenye kundi moja na Mahakama. Wakati huo wote Mahakama ilionesha nidhamu ya hali ya juu na kuchagua kukaa kimya.

Usiku wa deni haukawii kukucha, hatimaye siku ikafika TAKUKURU waliyokuwa wanaisubiri kwa hamu, ni leo tarehe 2 Octoba, 2023. Lakini kipigo walichokipata hawatasahau, kwani ukicheza na Mahakama, ambayo ni Mhimili wa Dola, utaumia.

Ilkuwa majira ya asubuhi saa 12. 30 wanamichezo wakipofurika kwenye Viwanja vya Mkwawa kushuhudia nginja ngija hiyo ambayo ilikuwa inasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa pande zote mbili.

Waamuzi walipouita mchezo huo, TAKUKURU, kama walivyokuwa wamedhamiria, waliingia uwanjani kwa mbwembwe, wakiwa wamejiamini huku wengine wakiwa wamevaa kininja ili kuwatisha vijana wa Professor, jambo lililovuta hisia kubwa na kushangiliwa kwa wingi kutoka kila kona na mashabiki.

Hata hivyo, ukimya ulitawala pale Mahakama ilipoanza kufanya mambo yake. Katika mvuto wa kwanza, TAKUKURU walijaribu kukaza kamba, lakini wakakutana na vyuma vikiwatazama kwa hasira kali.

Baada ya kukata pumzi na kushindwa kuhimili mziki mzito wa Mahakama, TAKUKURU wakakubali yaishe, hivyo wakaachia pointi moja kwenda kwa wapinzani wao katika hatua mvuto wa kwanza.

Kibao cha mashabiki kuwashangilia TAKUKURU kiligeuka katika kipindi cha pili baada ya Mahakama Sports kuonyesha umahiri na ukomavu wa hali ya juu katika mashindano hayo. TAKUKURU walijaribu kujitutumua, lakini wakakumbana na kibano kikaki na kuangukia pua, wakaamua kujisalimisha mahakamani ili kupata haki wanayostahili.

Baada ya mchezo huo, wachezaji wa TAKUKURU, huku wakipumua juu kwa juu kama samaki aliyekosa hewa mtoni, waliondoka kwenye Viwanja hivyo kila mmoja na njia yake na kutokomea kusikojulikana ili kukwepa aibu waliyoipata.

Ushindi huo walioupata Mahakama Sports unawafanya kujikita kileleni mwa kundi A na wanasubiri mchezo mmoja utakaochezwa kesho tarehe 3 Octoba, 2023 katika viwanja hivyo dhidi ya Ardhi ili kukamilisha hatua ya kutafuta 16 bora. Katika michezo yake miwili ya mwanzo, Mahakama ilitoa vipigo kwa RAS Kigoma na Mawasiliano.

Baada ya mchezo kumalizika, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema watavikata vidomodomo vya yoyote atakayejaribu kuwatunishia misuri, hasa wale wanaovamia mashindano bila kupata baraka za wazee.

"Hawa jamaa (TAKUKURU) walikuwa na mdomo sana, walidhani kukaa kwetu kimya wakaona watatufanya kama wanavyotaka. Haya ni mashindano, usivamie tu bila kwanza kupata baraka za wazee. Kila kitu kina taratibu zake sheikh.

“Hawa jamaa walikuwa wamejisahau sana kuwa kila mji haukosi wazee. Kipigo walichokipata nadhani sasa hawatarudia. Niwakumbushe pia kuwa usitukane Mamba kabla ya kuvuka mto, wasirudie tena kucheza cheza na haki za watu,” amesema.

Wachezaji wa TAKUKURU wakiwa hawaamini kilichowakuta walipakumbana na kibano kikali cha Mahakama na kulambishwa mchanga kwenye mchezo wa Kamba Wanaume.
Vyuma hivi hapa kutoka Mahakama Sports vikitembeza kichapo kwa TAKUKURU. Picha chini, vyuma vikijiandaa kukata vidomodomo vyao.

Shangwe la mashabiki wa Mahakama Sports (juu na chini) baada ya mchezo.

Bendera ya Mahakama ya Tanzania ikipepea kwenye mitaa mjini Iringa kusambaza haki kwa wakati na kwa wote. Picha chini vyuma vinaondoka katika Viwanja vya Mkwawa na kukata mitaa mjini Iringa kwa raha zao.

Wachezaji wa Mahakama Sports (juu na chini) wakifanya mazoezi ya mwisho mwisho kabla ya mchezo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni