Jumatano, 4 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS MPIRA WA MIGUU MAMBO SAFI

·Yatoshana nguvu na Kilimo

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu leo tarehe 4 Octoba, 2023 imetoshana nguvu kwa kutoka suluhu na timu ya Kilimo katika mchezo ambao ndiyo ulikuwa wa ufunguzi rasmi wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea mkoani hapa.

Mchezo huo uliochezwa majira ya mchana katika Uwanja wa Samora ulikuwa ni wa upinzani mkali, huku timu zote zikishambuliana zamu kwa zamu. Katika mchezo huo, Mahakama Sports ilicheza kandanda safi kwa pasi fupi fupi, lakini wapinzani wao walikuwa imara katika kuzuia mashambulizi.

Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, hakuna timu iliyokuwa imeliona lango la mwenzie. Katika kipindi cha pili timu zote zilikuwa zikishambuliana kwa zamu, lakini kabumbu lilichezwa zaidi katikati, hivyo kuzuia hatari yoyote kwenda kwenye lango la timu pinzani.

Katika kipindi hicho cha pili, mchezaji mmoja wa Kilimo alizawadiwa kadi ya njano kwa kumchezea mchezaji wa Mahakama Sports rafu. Hadi mwamuzi anamaliza mtanange huo, timu zote mbili zilitoka uwanjani bila kufungana.

Kwa matokeo hayo, Mahakama Sports inakwea kileleni mwa kundi A na kushika nafasi ya kwanza kwa kushinda mechi mbili, kutoka sale mchezo mmoja na kupewa ushindi mchezo mmoja baada ya  timu ya Maji kuchezesha mamluki.

Wachezaji walioiwakilisha Mahakama ni Micheal Turuka, Nasoro Mwampamba, Akida Mzee, Kelvin Muhagama, Frank Obadia, Gabriel Mwita, Martin Mpanduzi na Seleman Magawa, Abdi Sasamalo, Mbura Minja, Iman Zumbwe, Rashid Hamis, Devis Munubi na Gisbert Chentro.

Wengine walikuwa Seif Shamte, Nkuruma Katagira, Emmanuel Mwamole Fahamu Kibona na Ramadhani Seif. Benchi la ufundi liliongozwa na Kocha Mkuu Spear Mbwembe na Kocha Msaidizi Said Albea, Timu Meneja Shaibu Kanyachole, Meneja wa Vifaa Eliya Ngule na Daktari Janeth Mapunda.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko akimkabidhi mpira Nahodha Msaidizi wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Seleman Magawa (kulia) kama ishara ya uzinduzi rasmi wa Mashindano ya SHIMIWI.


Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu (juu) iliyotoshana nguvu na Kilimo(chini).


Manahodha wa timu zote mbili wakiwa katika picha ya pamoja na waamuzi kabla ya mchezo.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu (juu na chini) wakimiliki mpira.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu wakilisakama lango la wapinzani.
Sehemu ya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu (juu na picha mbili chini) iliyokaguliwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko kabla ya ufunguzi rasmi wa mashindano ya SHIMIWI.



Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Sports, Makocha na Daktari nao walikuwepo wakati wa ukaguzi wa timu uliofanywa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko (hayupo kwenye picha).




























































 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni