Jumatano, 4 Oktoba 2023

NAIBU WAZIRI MKUU AWATAKA VIONGOZI KUSHIRIKI KIKAMILIFU SHIMIWI

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe.Dkt. Dotto Biteko leo tarehe 4 Octoba, 2023 amefungua rasmi Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa na kuwahimiza Viongozi katika Wizara, Taasisi, Wakala zinazojitegemea na Mamlaka za Serikali za Mitaa kushiriki kimamilifu kwenye mashindano hayo wao wenyewe.

Akizungumza katika Uwanja wa Samora kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya kupokea maandamano ya wanamichezo kutoka Taasisi mbalimbali wanaoshiriki kwenye mashindano hayo, Waziri Biteko alieleza kuwa Viongozi wote wasichukulie mashindano hayo kama jambo dogo.

“Tusichukulia hili kama jambo dogo na wanaotakiwa kushiriki ni watu wa aina fulani na kwamba sisi tunayo makubwa zaidi kuliko haya. Ni imani yangu mwaka unaokuja sisi Viongozi tushiriki kikamilifu, hata kama tuna dharura, basi tupange vizuri ratiba zetu ili watumishi hawa waweze kufurahi kuwaona Viongozi wao wanashirikiana pamoja katika kuendeleza michezo,” amesema.

Amewakumbusha Viongozi wa Serikali kuwa watumishi wa umma ndiyo nyenzo kubwa ya maendeleo nchini Tanzania, hivyo inapotokea fursa ya kushiriki na wengine kwenye michezo ni muhimu kuwawezesha kikamilifu na kwa Viongozi kushiriki wao wenyewe, hatua itakayowafanya watambue kuwa michezo inathaminiwa.

“Tuwawezeshe kikamilifu wale wote ambao wanastahili kuja kwenye michezo. Haina maana yoyote watu hawa wametoka katika Mikoa mbalimbali kuja kushiriki katika michezo, halafu waishi kwa taabu kama watu waliopewa lift, hapana. Fedha mnazozitenga siyo hasara, bali zitakuwa faida na faida yenyewe mtaiona wakirudi kwenye ofisi zao,” amesema.

Kadhalika, Mhe, Dkt. Biteko amezihimiza Wizara, Mikoa, Taasisi na Idara na Wakala za Serikali kutokurudi nyuma katika kuwapa ruhusa watumishi wa umma ambao wapo tayari kushiriki katika mashindano hayo, hivyo wanapaswa kujitathmini ili kutambua umuhimu wa michezo hiyo kwa ajili ya maslahi makubwa na kuongeza tija mahala pa kazi.

Amerejea malengo ya mashindamo hayo ambayo, pamoja na mambo mengine, yanalenga siyo tu kuboresha afya na akili, bali pia kuboresha mahusiano mazuri ya kikazi pamoja na mtandao wa kiutumishi miongoni mwa washiriki wote. Hivyo, ameupongeza uongozi wa SHIMIWI na wanamichezo wote kwa kuhakikisha kuwa michezo hiyo inaendelea kuboreshwa mwaka hadi mwaka.

Awali, akimkaribisha Naibu Waziri Mkuu kuzungumza na wanamichezo wote, Mwenyekiti wa SHIMIWI Taifa Daniel Mwalusamba alieleza kuwa kwa mwaka huu wa 2023, mashindano hayo yanajumuisha jumla ya washiriki 2765 kutoka kwenye Wizara, Taasisi na Wakala za Serikali na kati ya hao wanaume ni 1570 na wanawake ni 1135 ambao wanaoshiriki katika michezo mbalimbali.

Alieleza kuwa wanamichezo hao wameanza kushiriki katika michezo mbalimbali kuanzia tarehe 29 Septemba, 2023 na michezo hiyo inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 14 Octoba, 2023. Mwenyekiti ametaja michezo ambayo watumishi wanashiriki ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Mpira wa Miguu, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha pamoja na vinyoya.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Tendegu amewakaribisha wanamichezo wote mkoani kwake na kuwahakikishia usalama wakati wote. Kadhalika, amewashukuru wananchi wa Mkoa huo kwa ukarimu wanaouonesha kwa wanamichezo hao na kuwaomba kuendeleza mahusiano mazuri yaliyopo.

Wanamichezo wa Mahakama Sports wakipita mbele ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe.Dkt. Dotto Biteko (picha chini) wakati wa maandamano kuashiria ufunguzi rasmi wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) mwaka 2023.
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe.Dkt. Dotto Biteko akizungumza na wanamichezo wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Tendegu akiwakaribisha wanamichezo mkoani kwake.

Mwenyekiti wa SHIMIWI Taifa Daniel Mwalusamba akizungumza katika shughuli hiyo ya ufunguzi.

Maandamano yakiendelea(juu na chini).


Wanamichezo (juu na chini) ndani ya Uwanja wa Samora.


Mahakama Sports wakiwa na ndugu zao Ikulu baada ya ufunguzi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni