Jumapili, 8 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS MPIRA WA MIGUU, NETIBOLI ZATINGA NUSU FAINALI SHIMIWI

·Utumishi yaoga mabao 2:1

·Bunge Netiboli yabunguliwa vikapu 38:36

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu za Mahakama Sports Mpira wa Miguu na Netiboli leo tarehe 8 Octoba, 2023 zimetinga katika hatua ya nusu fainali katika Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa baada ya kuwasurubu Utumishi na Bunge.

Ulikuwa mchezo wa Netiboli ulioanza kuchezwa majira ya saa 7:0 katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikristo Ruaha ambapo Bunge ndiyo walioanza kulishambulia lango la Mahakama Sports na kufanikiwa kutupia vikapu vinne vya haraka haraka. 

Hata hivyo, vijana wa Mahakama walitulia na kuanza kuwathibiti wapinzani na kujibu mapigo. Walisimama imara na kulishabulia lango la wapinzani mara kwa mara. Hadi timu zote zinaenda kwenye mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa mbele kwa vikapu 18 kwa17 walizokuwa wametupia Bunge. 

Kipindi cha pili kilianza kwa kila timu kumkaba koo mwenzake kutokana na tupia tupia za hapa na pale. Bunge wakitupia na Mahakama nayo inatupia. Hadi mchezo unamalizika, Mahakama Sports ilikuwa imeshatupia vikapu 38 kwa 36 walivyotupia Bunge.

Wakati Mahakama Sports Netiboli ikiwapukutua Bunge, kaka zao timu ya mpira wa miguu imewachakaza Utumishi kwa mabao 2:1 katika mchezo mgumu uliochezwa kwenye Uwanja wa Samora. 

Ilikuwa Mahakama Sports walioanza kuliona lango la Utumishi katika dakika ya nne kupitia kwa kiungo punda Seif Shamte ambaye alipachika bao safi baada ya kumvika kanzu mlinda mlango baada ya kupokea pasi kutoka kwa Abdi Sasamalo, hivyo kuiandikia timu yake goli la kuongoza.

Baada ya kuingia kwa bao hilo, Mahakama Sports walianza kutandaza kabumbu safi kwa kupiga pasi fupi fupi na kufanikiwa kuumiriki mpira kwa kiasi kikubwa. Hata hivyo, katika dakika za mwisho za kipindi cha kwanza, Utumishi walipata faulo na kufanikiwa kusawazisha baada ya mabeki wa Mahakama Sports kushindwa kuelewana.

Katika kipindi cha pili, Mahakama Sports walizidisha mashambulizi na kuwachezea wapinzani nusu uwanja. Dakika ya 49, winga wa pembeni Frank Obadia aliachia shuti na mpira ukazama kwenye nyavu, baada ya kupokea pasi murua kutoka kwa Martin Peter, hivyo kuiandikia timu yake bao la pili. Hadi mchezo unamalizika, Mahakama Sports ilitoka kifua mbele na kutinga katika hatua ya nusu fainali.

Michezo yote miwili imeshuhudiwa na Mkurugenzi wa Mipango wa Mahakama ya Tanzania ambaye pia ni mlezi wa Mahakama Sports, Erasmus Uisso.

Akizungumza baada ya michezo hiyo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza wachezaji wote kwa kucheza vizuri, kwa kujituma na hatimaye kuibuka washindi, licha ya timu pinzani kutoa upinzani mkali. 

"Hizi timu za Utumishi na Bunge ni nzuri sana na zimetoa upinzani mkali. Lakini, kama nilivyokwisha kusema, sisi tupo vizuri kwenye kila idara na timu yoyote itakayojipendekeza kwetu itapigwa. Vipigo hivi vitaendelea hadi kuchukua makombe. Hatuna utani na mtu safari hii," amesema.

Hawa hapa Mahakama Sports Netiboli, ni miamba kweli kweli.

Wanaume wa shoka, Mahakama Sports Mpira wa Miguu. Anayefuata anapigwa kama ngoma. 
Kikapu hicho kinatumbukia kwenya lango la Bunge.
Mahakama Sports Mpira wa Miguu wakishangilia bao, huku timu pinzani wakiwa hawaelewi kilichotokea.


'Stopper' wa Mahakama Sports Netiboli akitibua mipango ya wapinzani. 


Kiungo mchezeshaji wa Mahakama Sports Netiboli akimiriki mpira. 
Hapa kazi ya kutafuta upenyo inaendelea.Picha chini upenyo umepatikana na mpira upo kwenye 'zone' ya mtupiaji hatari Tatu Mawazo.






Mchezaji wa Mahakama Sports (kulia) akimthibiti mpinzani. 


Mchezaji wa Mahakama Sports akimiriki mpira. 
Mwamuzi akimwonyesha mlinda mlango wa Utumishi kadi ya njano kwa kumwandama mwamuzi wa pembeni baada ya goli walilofunga kukataliwa kwa kumfanyia rafu mbaya mlinda mlango wa Mahakama Sports. 
Wachezaji wa Mahakama Sports wakifurahia ushindi baada ya mchezo kumalizika. Picha chini wakimbeba juu kwa juu Mkurugenzi wa Mipango, Erasmus Uisso. 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni