Jumatatu, 9 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS YANYAKUA MEDALI NYINGINE SHIMIWI

·Yafanyiwa figisufigisu mbio za kupokezana vijiti

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imenyakua medali nyingine kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea mkoani hapa baada ya kufanya vizuri kwenye mchezo wa riadha wanawake.

Katika mchezo huo uliochezwa majira ya saa 12:30 asubuhi leo tarehe 9 Octoba,2023, Mahakama Sports imeshika nafasi ya pili kwenye mita 400 baada ya mkimbiaji wake hatari Upendo Gustaf kuwatimulia vumbi wapinzani wake.

Mahakama pia ilishiriki kwenye mbio za kupokezana vijiti wanawake na mfukuza upepo Justa George aliyekamata kijiti kwa mara ya mwisho alifanikiwa kushika nafasi ya kwanza, lakini akaondolewa kwenye kinyang’anyiro kwenda fainali.

Waamuzi walidai kuwa wakati anakimbia, Justa alitoka kwenye mstari wake, jambo ambalo siyo kweli. Hata hivyo, Viongozi wa Mahakama Sports wameamua kuivalia njuga figisufigisu hiyo ili haki iweze kutendeka.

Kadhalika, wanaume pia walishiriki kwenye mbio hizo kufanikiwa kuingia nuzu fainali. Waliondolewa baadaye kwenye mashindano kuelekea fainali baada ya mchezaji wake wa kwanza kushika kijiti kuchelewa kuchomoka kwenye mstari.

Hii ni mara ya pili kwa Mahakama Sports kuzoa medali kwenye mashindano hayo. Medali zingine ambazo tayari imeshaweke kibindoni ni riadha mita 3,000 wanawake kupitia kwa Justa George aliyeshika nafasi ya pili na tufe kupitia kwa Martin Mushi ambaye naye alinyakua nafasi ya pili.

Mahakama pia imefanikiwa kuingia fainali kwenye mbio za mita 100, mchezo ambao unatarajiwa kuchezwa kesho tarehe 10 Octoba, 2023.

Akizungumza kufuatia matokeo hayo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza vijana wake kwa kupeperusha vyema bendera ya Mahakama ya Tanzania na anaamini watafanya vizuri kwenye mchezo uliobakia.

 Amesema wataendelea kupambana pia kwenye michezo mingine ili kuweza kufanya vizuri na kuchukua vikombe. Mahakama Sports imeshaingiza tayari michezo minne kwenye hatua ya nusu fainali. Michezo hiyo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Netiboli na Mpira wa Miguu Wanaume.


Mwamba huyu hapa, Upendo Gustaf. Ukimwangalia kwa umbo huwezi kudhania kama ni mfukuza upepo hatari duniani. Picha chini akitimua vumbi.



Mwanamichezo wa Mahakama Sports, Upendo Gustaf (wa pili kutoka kulia) akikabana koo na mpinzani wake wakati wa kumalizia mbio za mita 400.

Upendo Gustaf akiongozwa na mwamuzi baada ya kumaliza mbio za mita 400. Picha chini akiandikisha jina kwa waamuzi wengine.






Upendo Gustaf, wa nne kutoka kulia akijiandaa kutimka mbio.

Justa George akikamilisha mbio za kupokezana vijiti na kushika nafasi ya kwanza. Hata hivyo, aliondolewa kwenye mashindano kwa figisufigisu za waamuzi kuwa alitoka kwenye mstari. Picha chini inaonyesha wazi jinsi alivyowaacha kwa mbali na yupo kwenye mstari wake.

Justa George ( wa kwanza kulia) akiwa na wafukuza upepo wenzake kabla ya kuanza kutimua vumbi.

Mchezaji wa Mahakama Sports Juma Mbega (wa kwanza kulia) akikamilisha mbio za kupokezana vijiti na kushika nafasi ya pili kwenye nusu fainali. Hata hivyo, timu yake ilitolewa kwenda fainali baada ya kushika nafasi ya nne. Picha chini timu ya Mahakama Sports (mstari wa kwanza) ikijiandaa kuchomoka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni