Jumapili, 8 Oktoba 2023

MAMBO YA NDANI YABURUTWA

·Waziri Mkuu Sera tabaani

· Mahakama Kamba Wanaume, Wanawake nusu fainali

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu za Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Kamba Wanawake zimetoa vipigo vikali leo tarehe 8 Octoba, 2023 kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa.

Mahakama Sports Kamba Wanaume waliwaburuta Mambo ya Ndani na kuwatupa kolokoloni, huku Wanawake ikiwabutua Waziri Mkuu Sera na kuwafungashia vilago kwenye mashaindano hayo.

Michezo yote miwili imechezwa majira ya jioni saa 11:00 katika viwanja vya Mkwawa na kushuhudiwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama, akiwemo Mkurugenzi wa Mipango wa Mahakama ya Tanzania, Erasmus Uisso. 

Ulikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza kuchezwa huku Waziri Mkuu Sera wakiingia uwanjani kwa kujiamini. Mchezo huo ulikuwa kama wa kisasi kwa kuzingatia kuwa katika mashindano ya SHIMIWI mwaka jana timu hizo ziliingia kwenye hatua kama hiyo na Waziri Mkuu Sera ikanyonyolewa. 

Baada wa waamuzi kuamuru mchezo kuanza, Mahakama Sports kama kawaida yao hawakuwa na subira na walitembeza kichapo kikali cha kufa mtu na kuwafanya timu pinzani wapoteane.

Hadi mivuto yote ilipokamilika, Mahakama Sports ikazoa pointi zote mbili na kuwaacha wapinzani wako hoi tabaani wakipumua juu juu kama paka aliyenasa kwenye matope, hivyo kutupwa nje ya mashindano.

Baada ya mchezo huo kukamilika, ulifuata mchezo wa Kamba Wanaume ambapo Mahakama Sports ilipangwa kupigishana kwata na timu ya Mambo ya Ndani. Mchezo huo pia ulikuwa ni wa kisasi kwa kuzingatia kuwa katika michezo ya Mei Mosi iliyopita, Mambo ya Ndani iliwapigisha chafya Mahakama.

Katika mchezo wa leo, Mahakama Sports walionekana tangu mwanzo kukamia na waamuzi walipoamuru ‘ngoma” iwekwe uwanjani, Mambo ya Ndani walikiona cha moto, kwani walipigwa kama ngoma na kusweka kolokoloni katika mvuto wa kwanza.

Ilipofika katika hatua ya pili, Mambo ya Ndani walijaribu kutumia mbinu ya kukaa chini ili kuwakata pumzi vijana wa professa. Hata hivyo, kilichowatokea hawakuamini macho yao.

Mambo ya Ndani waliburutwa vibaya na kujikuta wengine wanageukia kule walikotoka. Hadi mpambano unamalizika, Mahakama Sports ikazoa pointi zote mbili na kutinga katika hatua ya nusu fainali.

Timu ya Kamba Mambo ya Ndani ikiwa imesambaratika vibaya baada ya kuburutwa na Mahakama Sports. Picha chini Mambo ya Ndani wakiwa wamekaa chini ili kuwakata pumzi Mahakama Sports, lakini wamekiona cha moto.

Timu ya Mambo ya Ndani ikiwa haiamini kilichowakuta,  usicheze na Mahakama utaumia.
Miamba hiyo hapo, Mahakama Sports Kamba Wanaume. Ipo siku atakufa mtu.
Miamba mingine hiyo hapo, Mahakama Sports Kamba Wanawake. Waziri Mkuu Sera wameipatapata. Picha chini mmoja wa wanamichezo kutoka Waziri Mkuu Sera akiugulia kichapo baada ya kulambishwa mchanga.

Bendera ya Mahakama ikipepea baada ya Mahakama Sports kutembeza vichapo.
Shangwe kama lote, nginja nginja mpaka fainali na kuzoa makombe.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni