·Yabeba kombe mshindi wa pili wanaume
Na Faustine
Kapama-Mahakama, Iringa
Timu ya Mahakama ya
Tanzania (Mahakama Sports) Mchezo wa Bao leo tarehe 10 Octoba, 2023 imepeperusha
vyema bendera ya Mahakama ya Tanzania kwenye mchezo wa bao baada ya kushika
nafasi ya pili kwa upande wa wanaume.
Mchezo huo uliochezwa
katika maeneo ya Chuo Kikuu cha Kikristo Ruaha kuanzia saa 2:00 asubuhi
umemuinua kijana machachari, Hashim Rashid na kushika nafasi hiyo baada ya kuwabwaga
wapinzani wake kutoka katika hatua ya makundi hadi fainali.
Kutokana na matokeo hayo,
Mahakama Sports inanyakua kombe la kwanza kwenye mashindano hayo, huku tayari
imeshaweka kibindoni medali tatu, mbili katika mchezo wa riadha na moja kwenye
kurusha tufe.
Wanawake pia walishiriki
katika mchezo huo kupitia Filomemna Haule ambaye alifanya vizuri kuanzia kwenye
makundi na kufanikiwa kuwakimbiza mchaka mchaka wapinzani hadi hatua ya robo
fainali alipoteleza.
Kitu cha kushangaza
katika mchezo huo, mshindi wa kwanza ambaye ni Ras Lindi alipata vipigo mara
mbili kutoka kwa Philomena, ambaye hakuwa na uzoefu wowote kwenye mchezo huo
kwani ni mara yake ya kwanza kushiriki.
Kwa upande wa wanaume, Rashid
alianza mashindano kwenye mchezo huo kuanzia makundi kwa kukabana koo na Madini
ambao walitokashana nguvu sawa na baadaye akakutana na Uchukuzi ambaye
alimgalagaza vibaya.
Kwenye mchezo wa mwisho
hatua ya makundi, Mahakama Sports ilikutana na Ras Kigoma ambapo Rashid
alimshikisha adabu mpinzani wake na kutinga katika hatua ya 16 bora.
Katika hatua hiyo, Mahakama Sports ilikutana na mwajiri wake, Tume ya Utumishi wa Mahakama. Mpambano kati ya Baba na Mwana ulikuwa mkali, lakini mwisho Baba akakubali yaishe na kufungashiwa vilago na Mwana kwenye mashindano.
Matokeo hayo yaliipeleka
Mahakama Sports robo fainali na kukutana na Ras Ruvuma, ambaye walikutana
kwenye mashindano ya Mei Mosi Morogoro katika hatua ya fainali na kuibuka
mshindi.
Katika mchuano wa leo,
Ras Ruvuma ameangukia pua na kutupwa nje ya mashindano, hivyo kuiwezesha
Mahakama Sports kutinga nusu fainali. Kwenye hatua hiyo, Mahakama Sports imechuana
na Kilimo ambao nao wakachemsha.
Baada ya kuingia hatua ya
fainali, Mahakama Sports ikacheza na Ujenzi ambao walikiona cha moto baada ya Rashid
kutembeza makoleo hapa na pale, ingawa bahati haikuwa yake na kuishia kushika
nafasi ya pili.
Akizungumza baada ya
mchezo huo kumalizika, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza wachezaji
wake kwa mchezo na ushindani mzuri waliouonesha kwa kipindi chote.
“Haya ni mafanikio
makubwa sana kwetu. Nampongeza sana Philomena, hii ni mara yeke ya kwanza
kushiriki na hakuwa na uzoefu wowote kwenye mashindano haya, lakini mmeona
alichokifanya. Ninaamini mwakani atafanya maajabu.
“Vile vile nampongeza
sana mchezaji wetu Hashimu, hatua aliyofikia mwaka huu ni kubwa sana ukilinganisha
na mwaka jana ambapo alishika nafasi ya kwanza. Kwa mwendo huu mwakani
tutashika nafasi ya kwanza. Hivyo, nawapongeza wote kwa kuiheshimisha Mahakama
ya Tanzania,” amesema.
Kesho tarehe 11 Octoba, 2023, Mahakama Sports inajitupa kwenye michezo minne kwenye hatua ya nusu fainali. Michezo hiyo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Netiboli na Mpira wa Miguu Wanaume.
Mwingine huyu hapa, Philomena Haule. Naye mambo safi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni