Na. Mwinga Mpoli – Mahakama, Mbeya
Mawakili mkoani Mbeya wamekutanishwa na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya na kukumbushwa kuanza rasmi kwa majaribio ya mfumo wa kielektroniki wa kusajili, kusimamia, kuratibu mashauri maarufu kama ‘e- Advanced Case Management System’ (eCMS).
Akizungumza na mawakili hao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Dastan Ndunguru leo tarehe 10 Oktoba, 2023 amesema, alipokea ombi la mawakili hao kuomba kukumbushwa juu ya matumizi ya mfumo huo na kuwataka mawakili hao kuwa makini katika kufuata maelekezo yote wanayopewa.
“Muwe makini na maelekezo yote yatayotolewa ili tuweze kufanikisha zoezi ili kwani linaenda kuhitimishwa tarehe 31 Oktoba, 2023”, alisema Mhe. Ndunguru.
Naye,
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu
aliwataka mawakili kutoa ushirikiano ili wanapoelekea kuanza rasmi matumizi ya
mfumo huo kusiwe na mikwamo isiyo ya lazima kutoka upande wa wao.
“Niwaombe mawakili kuwasiliana na ofisi ya Naibu Msajili mara moja pale itakapojitokeza mkwamo ama changamoto ya aina yoyote hasa kipindi hiki cha majaribio ili tuweze kuziwasilisha mara moja kwenye jopo la ujenzi wa mfumo huu” alisisitiza Mhe. Temu
Aidha,
kwa upande wake Afisa Tehama wa Mahakama Kuu Mbeya Mhandisi. Sadati Kalungwana
aliwapitisha upya mawakili hao kwenye mchakato mzima wa uwasilishaji wa mashauri
Mahakamani pamoja na namna ya ulipaji katika mfumo wa eCMS na aliwasisitiza
kuwa yeye yupo tayari wakati wowote kuzipokea changamoto zote
zitakazowasilishwa na kuzifanyia kazi mapema iwezekanavyo ili kazi zisikwame.
Afisa Tehama
Mahakama Kuu Mbeya Mhandisi. Sadati Kalungwana akiulezea mfumo mpya wa Kielektroniki wa kusajili, kusimamia na kuratibu mashauri wa e- Advanced Case Mangaement System (e-CMS) kwa wadau wa Mahakama (hawapo pichani)
Naibu Msajili wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akifuatilia maelekezo yanayotolewa katika mafunzo hayo ya mfumo wa kielektroniki.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia kwa umakini mafunzo hayo yaliyotolewa na Afisa Tehama Mahakama Kuu Mbeya Mhandisi. Sadati Kalungwana (hayupo pichani).
Muonekano wa sura ya mfumo huo (Interface) katika picha ya Powerpoint
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni