Alhamisi, 5 Oktoba 2023

MAHAKAMA SPORTS YATIMUA VUMBI SHIMIWI IRINGA

·Yanyayua makwapa mshindi wa pili Riadha, Tufe

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imeanza kunyayua makwapa katika Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea mkoani hapa baada ya kufanya vizuri kwenye michezo ya riadha wanawake na tufe wanaume.

Katika mchezo wa riadha, Mahakama Sports imeshika nafasi ya pili kwenye mita 3,000 baada ya mfukuza wake upepo Justa George, maarufu kama MMM kuwatimulia vumbi wapinzani wake. Justa pia aliipeleka Mahakama fainali kwenye mita 100.

Kadhalika, mfukuza upepo mwingine maarufu wa Mahakama Sports Upendo Gustaf aliipeperusha vyema bendera ya Mahakama kwenye mita 200 na 400 na kufanikiwa kutinga fainali baada ya kushika nafasi ya pili kwenye michezo hiyo.

Kwa upande wa wanaume, Martin Mpanduzi alipepetana na wapinzani wake kwenye mita 100 na kufanikiwa kutinga nusu fainali baada ya kukamata nafasi ya pili. Hata hivyo, aliondoshwa kwenye kinyang’anyiro wakati wa kwenda fainali baada ya kuteleza wakati anaanza kutimua mbio.

Katika upande wa mchezo wa tufe, Martin Mushi alifanya vizuri na kushika nafasi ya pili baada ya kuzoa pointi 9.05, akimfuatia mpinzani wake wa karibu aliyepata pointi 9.44. Kufuatia ushindi huo mnono, Mahakama Sports imejihakikishia hadi sasa kuweka kibindoni medali mbili.

Akizungumza kufuatia matokeo hayo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza vijana wake kwa kupeperusha vyema bendera ya Mahakama ya Tanzania kwenye michezo hiyo.

 Amesema hatua waliyofikia ni nzuri na wanatarajia kufanya vizuri pia kwenye michezo mingine. "Kama nilivyosema awali, huu ni mwanzo mzuri na tutaendelea kukusanya makombe na medali kwenye michezo mingine. Hatua tuliyofikia kwa sasa ni nzuri, "amesema.

Mahakama Sports imepeleka timu nne kwenye hatua ya 16 bora baada ya kufanya vizuri kwenye makundi. Michezo hiyo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Netiboli na Mpira wa Miguu Wanaume.

Mfukuza upepo wa Mahakama Sports Justa George akimaliza mbio za mita 3,000 na kushika nafasi ya pili katika Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI).

Mwamba huyu hapa, Martin Mushi, mrusha tufe hatari. Ameshika nafasi ya pili kwenye mchezo huo. Picha chini akirusha tufe wakati wa mashindano.




Justa George (kulia) akipongezwa na Naibu Katibu Mkuu wa Mahakama Sports, Theodosia Mwangoka baada ya mchezo.
Wanamichezo wakimpongeza Martin Mushi baada ya kuibuka mshindi wa pili kwenye mchezo wa tufe.
Justa George akiwatimulia vumbi wapinzani wake wakati wa mchezo. Picha chini akipongezwa na mwanamichezo mwenzie wa Mahakama.
 

Mfukuza upepo wa Mahakama Sports Upendo Gustaf (katikati) akichanja mbuga wakati wa mchezo huo. Picha chini akipongezwa na wanamichezo wenzie.


Mwanariadha Martin Mpanduzi (mwenye t-shirt ya summer blue) akipambana kwenye mbio za mita 100. Picha chini (kulia) akipongezwa na wanamichezo wenzie kwa kushika nafasi ya pili kwenye hatua na nusu fainali. Hata hivyo aliondoshwa kwenye mashindano baada ya kuteleza wakati anaanza kukimbia.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni