Jumatano, 25 Oktoba 2023

MAHAKAMA YATEKELEZA OMBI LA RAIS SAMIA KUHUSU UTALII

· Yapeleka Majaji, wageni 150 Ngorongoro

·Nao waahidi kurudi Tanzania kujionea vivutio zaidi

Na Faustine Kapama-Mahakama, Arusha

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe Prof Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 25 Octoba, 2023 amewaongoza Majaji Wakuu kutoka Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika kutembelea Hifadhi ya Ngorongoro mkoani Arusha.

Hatua hiyo ni mwitikio wa ombi la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokuwa anafungua Mkutano wa Jukwaa la Majaji Wakuu kutoka nchi hizo katika Hoteli ya Mount Meru jijini hapa hivi karibuni.

Safari kuelelea katika Hifadhi hiyo ilianza mapema asubuhi saa 12.00 katika Hoteli hiyo na msafara wa Majaji hao ulipokelewa na Viongozi wa Mamlaka ya Hifadhi katika lango kuu la kuingilia hifadhini.

Wakiwa katika Hifadhi hiyo, Majaji Wakuu kutoka nchi hizo, Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na wageni wengine mbalimbali wamejionea utajiri wa wanyama pori na misitu ya kupendeza.

Watalii hao wamefanikiwa kuwaona baadhi ya wanyama maarufu duniani wanaofahamika kama Big-5 wanaopatikana kwa urahisi katika Hifadhi hiyo kama Tembo, Simba, Nyati na Faru. Chui, ambaye ni miongoni mwa Wanyama hao maarufu hakuweza kuonekana. Kwa kawaida, Twiga hapatikani katika hifadhi hiyo kutokana na umbo lake.

Kadhalika, Majaji Wakuu hao pamoja na wageni wengine wamefanikiwa kuwaona wanyama wengine kama swala, pundamilia, mbuni, nyani, fisi, Kiboko na ndege wa aina mablimbali wakiwemo Filamingo.

Viongozi hao wameonesha kufurahishwa na utalii huo na wamefarijika kujionea kwa macho wanyama wanaowaona kwa picha kwenye vitabu na runinga. Wameahidi kuja tena Tanzania kwa ajili ya kufanya shughuli za utalii.

Akizungumza kwenye lango kuu la kuingilia na kutokea kwenye Hifadhi hiyo baada ya Viongozi hao kufanya utalii, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Watendaji Wakuu wa Mahakama kutoka nchi hizo, Prof Elisante Ole Gabriel amewaambia Waandishi wa Habari kuwa wageni takribani 150 wametembelea kivutio hicho cha Ngorongoro ambacho kipo umbali wa mita 610 kutoka juu hadi chini na wameona wanyama wengi, wamefurahi na wengi wameonesha nia ya kutaka tena kuja kwa mara nyingine.

“Leo wageni hawa kutoka nchi 16 wameona Tembo, Simba, Nyati na Faru na wengine wengi na baadhi yao wamesema walikuwa hawajawahi kuwaona. Hii tunaifanya Tanzania iheshimike na watu wanaona nchi yetu ni ya kipekee kwa sababu ya heshima hii,” Prof. Ole Gabriel amesema.

Amesema kuwa kila Taasisi, ikiwemo Mahakama inawajibu wa kuona jinsi gani ya kutangaza vivutio vyetu vya kitalii, ni utajiri na dhamana ambayo Tanzania Mungu ameiipa, hivyo ni vyema kuthamini hali hiyo.

Amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kufungua Mkutano huo cha Majaji Wakuu ambao wameonesha kukuguswa na kitendo hicho, wamefarijika na wameona wametendewa heshima ya hali ya juu.

“Sisi kama Watendaji Wakuu wa Mahakama tumejifunza mengi na wenzangu wameahidi kwamba katika ngazi ya familia nao watafanya jitihada za kuja kutembelea vivutio vyetu,” amesema.

Majaji Wakuu wanaoshiriki kwenye Mkutano huo wanatoka katika nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Namibia, Zimbabwe, Eswatini, Msumbiji, Seychelles, Botswana, Angola, Zanzibar, Malawi, Lesotho, Mauritius, Zambia na Afrika ya Kusini.

Majaji Wakuu kutoka Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika na wageni wengine wakiwa katika lango kuu la kuingilia kwenye Hifadhi ya Ngorongoro. Picha chini Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Watendaji Wakuu wa Mahakama kutoka Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika, Prof Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kulia) akiwa na Majaji hao.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Watendaji Wakuu wa Mahakama kutoka nchi za Kisini na Mashariki mwa Afrika, Prof. Elisante Ole Gabriel (mwenye hama) akizungumza na wageni hao (picha chini) kabla ya kuingia kwenye hifadhi.

Msafara wa magari ya kitalii kuelekea kwenye hifadhi ya Ngorongoro. Picha chini, watalii wakiwa ndani ya hifadhi kabla ya kugawanyika kwenye makundi mawili ili kutembelea hifadhi hiyo na kuwaona wanyama kwa urahisi.

Mfalme wa nyika, Simba akiwa amejipumzisha.
Tembo, kama Tembo wakiwa kwenye hifadhi.
Tazama makundi makubwa ya Nyati (juu na chini) ndani ya hifadhi.

Vifaru wawili wakionekana kwa mbali.
Pundamilia, wanyama wapole kuliko wote.
Swala hao, kitoweo hicho safi kabisa.
Viboko na ndege Filamingo ndani ya hifadhi hiyo.
Makundi ya Nyani yakizurula hifadhini.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Watendaji Wakuu wa Mahakama kutoka Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo katika picha) baada ya kufanya utalii kwenye hifadhi hiyo.

(Picha na Lydia Churi na Mary Gwera-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni