Jumanne, 24 Oktoba 2023

MAJAJI WAKUU WATEMBELEA MABANDA YA MAONESHO ARUSHA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Arusha

Majaji Wakuu kutoka Umoja wa Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika wanaoendelea na Mkutano wa Mwaka jijini hapa leo tarehe 24 Octoba, 2023 wametembelea mabanda ya maonesho yaliyoandaliwa na wadau mbalimbali wa Mahakakama ya Tanzania kujionea shughuli wanazofanya katika muktadha mzima wa utoaji haki.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliwaongoza Majaji hao na wageni wengine kutembelea mabanda hayo pembezoni mwa Mkutano huo na wameonyesha kuvutiwa na maendeleo ya kisasa ya teknolojia na miundombinu yanayotukati katika shughuli za kimahakama.

Mabanda hayo yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Uhamiaji, Shirika la Maendeleo la Taifa, Shirika la Ndege la Taifa, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na wengine.

Wakiwa katika mabanda hayo, Majaji Wakuu hao walichukua muda mrefu katika banda la Mahakama ya Tanzania baada ya kuvutiwa na mambo kadhaa yanayofanywa  katika kutoa haki kwa wananchi.

Akizungumza akiwa katika banda hilo, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha amesema Majaji Wakuu wote wamewatembele na kujionea mambo makubwa yanayofanyika, hivyo kuelekeza wataalam wao kuja Tanzania kujifunza zaidi.

“Kuna nchi ambazo zimesema hazitatuma watu wao, zinataka wataalam wetu waende kule. Miaka yote Tanzania imekuwa kiongozi wa Nchi za Afrika katika masuala mbalimbali. Sisi tumekuwa Makao Makuu ya ukombozi wa Bara la Afrika.

“Hivyo, tukiwa Makao Makuu ya ukombozi kwa masuala ya utoaji haki, bado tunaona tunatekeleza wajibu wetu na sisi tumewaambia tupo tayari muda wowote ule, tutakwenda kuwashirikisha wenzetu,” amesema.

Ametaja baadhi ya maeneo ambayo Majaji hao wamefurahishwa walipotembelea banda la Mahakama, ikiwemo matumizi makubwa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania katika utoaji haki.

Mhe. Dkt. Rumisha ameeleza kuwa nchi zingine zilikuwa na mifumo ambayo wameinunua, hali ambayo ni tofauti kwa Tanzania. Amesema mifumo yote katika Mahakama ya Tanzania imejengwa na wataalam wa ndani, yaani watumishi wa Mahakama.

Amebainisha faida nyingi za kufanya hivyo, ikiwemo uwezo wa kuongeza au kupunguza kitu chochote kwenye mfumo bila kutafuta mtu mwingine, tofauti na nchi zingine ambazo zimenunua mifumo iliyotengenezwa ulaya ambayo hairuhusu kufanya chochote.

Faida nyingine ni kwamba Mahakama ya Tanzania hailipii chochote kwa mwaka kwa kuwa mfumo umetengenezwa na wataalam wa ndani, tofauti na nchi nyingine ambazo hutoa gharama za uendeshaji.

Jaji Rumisha ametaja jambo jingine lililopelekea mafanikio hayo kama matumizi bora ya rasimimali na katika jambo hilo Majaji Wakuu hao walitaka kujua fedha zilizotumika kufanya yote hayo ilitoka wapi na makisio yao yalikuwa ni mabillioni ya fedha.

Aliwaeleza kuwa fedha iliyotumika haifiki hata robo ya kile walichokuwa wanafikiria kwa sababu mambo yote yaliyofanyika yametumia fedha ambazo hazizidi Dola za Kimarekani millioni 60, ambazo ni sawa na dola millioni tisa kwa mwaka kwa kugawanya muda uliotumika.

“Nimewapa mfano wa ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita katika Mikoa ya Dar es Salaama, Mwanza, Arusha, Dodoma na Morogoro ambapo tulibakisha shillingi billioni 3.6 za Kitanzania baada ya kukamilisha ujenzi huo,” amesema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha amesema kuwa Majaji hao wamepata kufahamu mambo makubwa yanayofanywa mahakamani na wamevutiwa na mambo kadhaa, ikiwemo dhana hiyo ya uwepo wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki.

“Wamevutiwa namna gani ambapo unaweza kuwakusanya wadau wote wa haki katika jengo moja na kuwepo na ngazi zote za Mahakama. Hili ni jambo ambalo wamelipenda sana na wametamani kwenda kwenye majengo yetu hayo kujionea,” amesema.

Mhe. Kamugisha ametaja suala lingine ambalo Majaji Wakuu hao wamevutiwa ni maendeleo ya kusogeza huduma za Mahakama karibu na wananchi, hususani matumizi ya Mahakama zinazaotembea. Amesema wamewaeleza namna Mahakama hizo zinavyofanya kazi na mpango wa kuongeza Mahakama zingine sita ambazo zitaanza kufanya kazi kufikia Januari mwakani.

“Wamevutiwa kuona kwamba huduma hizi zinawalenga wananchi ambao hawana uwezo wa kusafiri muda mrefu, wanawake wajane na wale ambao wamedhurumiwa haki zao na wafanyabiashara wadogo, kwamba tunawafuata katika maeneo yao ya biashara,” amesema.

Matumizi ya TEHAMA pia ni eneo ambalo limeleta mvuto na wageni wengi wakataka kuendelea kukaa katika banda la Mahakama, japo muda ulikuwa umeisha. Mhe. Kamugisha amewaelezea mifumo ya kitehama, mpango wa menejimenti ya mashauri na mfumo mpya unaokuja ambao utaanza kufanya kazi mwanzoni mwa mwezi ujao wa Novemba.

“Wamevutiwa sana kuona namna gani Mahakama inaweza kufahamu kile kinachoendelea nchi nzima ndani ya muda huo huo, kwa maana hata Jaji Mkuu akiwa ofisini anaweza kuona kitu gani Jaji au Hakimu mmoja mmoja anafanya na hali ya mashauri katika Mahakama zote kwa wakati mmoja,” amesema.

Kiupekee, Mkurugenzi huyo aliwaelezea Majaji Wakuu teknolojia mpya inayokuja ya kunukuu na kutafsiri mienendo ya kimahakama na wamevutiwa namna itakavyosaidia kuwaondolea Majaji na Mahakimu jukuku la kuandika mwenendo kwa mkono na kutafsiri mwenendo au hukumu kwa njia za kawaida.

“Kama tulivyoeleza jana, tumesikiliza mashauri mengi katika kipindi cha Uviko-19, hivyo wakataka kujua namna gani tuliweza kufanya hivyo, tumewaonyesha teknolojia yetu na mfumo wa kusikiliza mashauri kwa njia ya mtadao, hivyo wakavutiwa namna gani mtu anaweza kuwa yupo nyumbani na Jaji yupo ofisini, lakini shauri likasikilizwa, hili nalo limeleta mvuto mkubwa,” amesema.

Majaji Wakuu hao wanaoshiriki kwenye Mkutano huo wanatoka katika nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Namibia, Zimbabwe, Eswatini, Msumbiji, Seychelles, Botswana, Angola, Zanzibar, Malawi, Lesotho, Mauritius, Zambia na Afrika ya Kusini.

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo kwenye picha) kwenye banda la Mahakama ya Tanzania baada ya Majaji Wakuu kutoka Umoja wa Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika kutembelea banda hilo pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa Viongozi hao jijini Arusha.

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha (kushoto) akitoa maelezo kwa sehemu ya Majaji Wakuu hao walipotembelea banda la Mahakama ya Tanzania.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliyeongoza Majaji Wakuu hao kwenye maonesho akiwa katika banda la Shirika la Maendeleo ya Taifa. Picha chini akitia saini kwenye kitabu cha wageni.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto) akiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel katika banda la Wakili Mkuu wa Serikali.


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel (kushoto) akitoa maelezo kwa mmoja wa Viongozi waliotembelea banda la chama hicho.
Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Deo Nangela (wa pili kulia) na Mhe. Joachim Tiganga wakifurahia jambo walipokuwa wanapata maelezo kutoka kwa mtumishi wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania walipokuwa kwenye banda hilo.
Sehemu ya Wanachama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TAWJA) wakiwa na Mwanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania, Mhe. Elimo Masawe (wa kwanza kushoto).
(Picha na Lydia Churi na Jeremia Lubango-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni