Na Naumi Shekilindi-Mahakama, Simiyu
Mahakama
ya Tanzania imekamilisha ahadi ya kuzipatia magari mapya Mahakama za Wilaya
Busega na Itilima katika Mkoa wa Simiyu.
Hakimu
Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Busega, Mhe. Christian Rugumila na Hakimu
Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Itilima, Mhe. Robert Kaanwa, wakiambatana na
watumishi wa Mahakama hizo wamepokea magari hayo kwa furaha kubwa.
Kukabidhiwa
kwa magari hayo kunajibu kilio cha muda mrefu katika Mahakama hizo cha
changamoto ya usafiri kwa Viongozi hao wa Mahakama katika ngazi ya Wilaya.
Mahakama
za Wilaya Busega na Itilima ni miongoni mwa Mahakama mpya 18 zilizojengwa kwa
ufadhili wa Benki ya Dunia ambazo zilizinduliwa kwa pamoja tarehe 25 Novemba,
2022 katika viwanja vya Mahakama ya Wilaya Busega.
Kwa
kipindi chote tangu kuzinduliwa kwa Mahakama hizo hakukuwa na usafiri wa wa
uhakika wa kuwahudumia Mahakimu Wafawidhi hao, hasa wanapokuwa katika
utekelezaji wa majukumu yao.
Akizungumza
baada ya kupokea gari la Mahakama yake, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Busega
alielezea kufurahishwa na hatua hiyo kwani amekuwa wakipitia changamoto nyingi,
hasa wakati wa ukaguzi wa robo mwaka kwa
Mahakama za Mwanzo, kuhudhuria vikao vya kanda na katika kutekeleza
majukumu ya ofisi kwa ujumla.
Naye
Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Itilima hakuwa nyuma katika kuelezea
furaha yake, kwani uwepo wa gari hilo unaenda kutatua changamoto nyingi zilizopo
katika Wilaya hiyo kwa urahisi zaidi.
Kabla
ya kupata magari hayo, Viongozi hao walikuwa wakiazima gari kutoka Mahakama ya
Wilaya Bariadi kwa ajili ya shughuli za ukaguzi na kuhudhuria vikao mbalimbali
vya kanda. Hatua hiyo ilipelekea wao kushindwa kukagua mara kwa mara maendeleo
ya Mahakama za Mwanzo.
Wameushukuru
uongozi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya
Wilaya Bariadi, Mhe. Caroline Kiliwa kwa kuwahudumia usafiri katika kipindi
chote walichokua hawana gari.
Wameahidi kuendelea kufanya kazi kwa ari zaidi kwani wameweza kurahisishiwa utekelezaji wa majukumu yao, hasa katika kuhakikisha wadaawa wa ndani na nje wanapata huduma bora.
Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Itilima,Mhe. Robert Kaanwa (kulia) akikabidhiwa funguo na Dereva aliyeleta gari hiyo, Bw. John Masunga mbele ya watumishi wa Mahakama.
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Itilima wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kupokea gari yao mpya.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni