Na Seth Kazimoto - Mahakama Kuu, Arusha
Wananchi mkoani hapa, wakiwemo
watumishi wa Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Arusha hivi
karibuni walipatiwa elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Kituo cha Huduma Bora kwa
Mteja (Call Centre) cha Mahakama ya Tanzania.
Katika maelezo ya ufunguzi
wa kipindi hicho, Msimamizi wa Kituo hicho, Bi. Evetha Mboya alisema huwa wanapokea mrejesho juu ya huduma zinazotolewa na
Mahakama katika Mikoa yote ya Tanzania.
“Mrejesho huu ni pamoja na
malalamiko, mapendekezo, maulizo na pongezi toka kwa wateja. Wateja ni pamoja
na watumishi wa Mahakama (wateja wa ndani) na wale wa nje (wananchi wanaopata
huduma za Mahakama),” alisema.
Bi. Evetha aliongeza kuwa
tangu kuanzishwa kwa Kituo hicho kumekuwa na manufaa mbalimbali ikiwemo,
wananchi ambao ndio wadau wakubwa kupata sehemu ya kutoa madukuduku yao juu ya
huduma za Mahakama.
Alisema pia kuwa Mahakama imeweza
kujitahimini juu ya ubora wa huduma inayotolewa na kuweza kupata taarifa ya
maeneo yanayolalamikiwa na kufanyiwa maboresho.
Aliyataja maeneo
yanayolalamikiwa zaidi kuwa ni pamoja na mirathi, utekelezaji wa hukumu,
dhamana na ufunguaji wa mashauri kwa njia ya mtandao.
Aidha, Bi. Evetha alizitaja
njia mbalimbali za kuwasilisha maoni, malalamiko, pongezi na mapendekezo,
ikiwemo kwa mteja kupiga simu au kutuma ujumbe mfupi (sms) kwenda namba 0752
500 400 na 0739 502 401.
Kadhalika, alisema mteja anaweza
kutumia email maoni@judiciary.go.tz, email
maalum ya kupokea mrejesho unaohusiana na mashauri ya mirathi ccamirathi@judiciary.go.tz na njia
ya tovuti ambayo ni www.judiciary.go.tz na mara baada ya kufungua tovuti hiyo,
kuna kisanduku cha kutoa maoni juu ya huduma za Mahakama.
Kwa upande wake, Hakimu
Mkazi Mwandamizi anayehudumu katika Kituo hicho, Mhe. Aden Kanje alieleza kuwa
kama mteja hataweza kuwasilisha lalamiko lake Call Centre anaweza kupeleka
lalamiko lake sehemu zingine.
Alizitaja sehemu hizo kama Kamari
za Maadili za Maafisa wa Mahakama ngazi ya Wilaya na Mkoa, kwa Hakimu Mfawidhi
wa Mahakama ya Wilaya, Mkoa au kwa Naibu Msajili na kwa kutumia mfumo wa
malalamiko wa Sema na Mahakama.
Alieleza kuwa Kituo cha
Huduma kwa Mteja kinazingatia mambo mbalimbali katika kuchakata malalamiko ya
wateja, ikiwemo usiri na muda na kusisitiza kuwa lalamiko la mteja ni siri na
lazima lichakatwe kwa usiri mkubwa kiasi kwamba hata afisa anayelalamikiwa
hawezi kujua kama kuna lalamiko dhidi yake.
Alisema suala la muda ni
muhimu, kwani lalamiko hushughulikiwa ndani ya siku saba na ikishindikana
hupelekwa katika ngazi ya juu zaidi ili lipatiwe ufumbuzi na mteja hupatiwa
mrejesho wa hatua iliyofikiwa katika kushughulikia lalamiko lake.
Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call
Centre) kilianzishwa na Mahakama ya Tanzania tarehe 01 Machi, 2022 chini ya
Kurugenzi ya Huduma za Kimahakama, Ukaguzi na Maadili kwa lengo la kupata
mrejesho toka kwa wateja wa Mahakama juu ya huduma zinazotolewa.
Kituo hiki ni sehemu ya
utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama, hasa nguzo ya tatu ambayo ni “ushirikishwaji
wa wadau na kujenga imani kwa wananchi.”
Tangu kuanzishwa kwa Kituo
hiki, Mahakama ya Tanzania imepata manufaa makubwa kwani hadi kufikia tarehe
30, Agosti 2023, kituo kimeweza kupokea jumla ya mirejesho 2,751 ikiwa ni
maoni, mapendekezo, maulizo, malalamiko na pongezi. Mirejesho 2740 tayari
imefanyiwa kazi na wateja kupatiwa mrejesho, sawa na asilimia 98.6 na
malalamiko 11 yanaendelea kushughulikiwa.
Baadhi ya wananchi waliopata elimu kuhusu huduma zitolewazo na Kituo cha Huduma kwa Mteja katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.
(Habari
hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni