Jumanne, 10 Oktoba 2023

WATUMISHI WA MAHAKAMA BUKOBA WAPONGEZWA KWA KASI YA MATUMIZI YA TEHAMA

Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama Bukoba

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewapongeza watumishi wa Mahakama kanda ya Bukoba kwa kutoa huduma bora na kuongeza kasi katika ya matumizi ya Tehama iliyowezesha kusajili mashauri kwa njia ya mtandao kwa zaidi ya asilimia 99.

Akizungumza na watumishi wa kanda hiyo wakati wa Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na watumishi hao jana mjini Bukoba, Jaji Mkuu amesema mafanikio hayo yanadhihirisha ni kwa jinsi gani Mahakama inahama kwenda kidigitali katika shughuli zake za utoaji haki.

Alisema Mahakama ya Tanzania imefanya mabadiliko makubwa katika mfumo wa Usimamizi na Uendeshaji wa Mashauri (E-Case Management) na hivi sasa mfumo huo uko katika hatua za mwisho za majaribio kabla ya kuanza kutumika rasmi Tarehe 1 Novemba mwaka huu.

Aidha, Jaji Mkuu amewataka watumishi wa Mahakama kote nchini kuupitia mfumo huo mpya na kutoa mapendekezo ya maeneo yenye changamoto yanayotakiwa kufanyiwa uboreshaji ili mfumo huo ufanye kazi vizuri kama ilivyokusudiwa.

”Mfumo huu utakapoanza kutumika utakuwa na faida nyingi zikiwemo kuongeza ufanisi, kuongeza uwazi na kupunguza malalamiko ya wananchi, kupunguza hisia za kuwepo kwa vvitendo vya rushwa kutokana na uwazi na kusaidia viongozi katika usimamizi”, alisema Jaji Mkuu.

Mwenyekiti huyo wa Tume pia amewataka watumishi wote wa Mahakama nchini kuisoma kwa kina taarifa ya utafiti ya mwaka 2023 uliofanywa na Taasisi ya Repoa kuhusu viwango vya wananchi kuridhika na huduma zinazotolewa na Mahakama ili waweze kujitathmini zaidi kuhusu utendahji kazi wao na kuyafanyia kazi baadhi ya maeneo yaliyoanishwa kwenye utafiti huo.

”Someni kwa kina taarifa ya utafiti uliofanywa na Repoa ya mwaka 2023 na ile ya mwaka 2015 iliyotusaidia kuandaa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Mahakama na pia someni taarifa ya utafiti ya mwaka 2019 iliyopima nusu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati huo, taarifa ya sasa inapima nusu ya utekelezaji wa mpango Mkakati wa awamu ya pili”, alisisitiza.

Aliwataka watumishi wa Mahakama kulipa uzito suala la uadilifu kwa kuwa taarifa ya utafiti uliofanyika mwaka 2023 inaonesha kuwa uadilifu umeimarika  mahakamani lakini bado kuna changamoro katika Mahakama za chini.   

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu kanda ya Bukoba jana mjini wakati wa Mkutano wa Tume na watumishi hao.   
Watumishi wa Mahakama Kuu kanda ya Bukoba wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania jana wakati wa Mkutano wa Tume na watumishi hao mjini Bukoba.   


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni