Jumatano, 18 Oktoba 2023

WATUMISHI, WADAU MOSHI WANOLEWA MATUMIZI YA MFUMO MPYA KIELEKITRONIKI

Na. Paul Pascal – Mahakama, Moshi

Uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi umefanya mafunzo ya mfumo mpya wa kielekitroniki wa kuratibu na kusimamia mashauri “Advanced Electronic Case Management System (e-CMS)” ikijumuisha watumishi na wadau wapatao 69 ikiwa ni pamoja na Mahakimu, Wahasibu, Wasaidizi wa kumbukumbu, Mawakili wa Serikali na wa wakujitegemea.

Akifungua mafunzo hayo ya siku moja leo tarehe 18 Oktoba, 2023 katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Omari Kingwele amesema, moja ya mpango wa Mahakama, kupitia nguzo ya kwanza ya Mpango Mkakati wa miaka mitano wa 2020/21-2024/25 ukihusisha lengo la kimkakati namba tatu linaelekeza kuwa “Kuongeza ufanisi katika katika shughuli za kimahakama na kukuza matumizi ya TEHAMA”.

“Lengo hilo linaitaka Mahakama kuanzisha Mahakama Mtandao (e-judiciary) ili kazi zote za kimahakama na utawala pamoja na huduma zote zinazotolewa na Mahakama zitolewe ki-dijitali. Katika kutekeleza lengo hili muhimu, Mahakama kwa kutumia wataalam wake wa ndani imejenga mifumo ya kielektroniki itakayotumika kuratibu shughuli zote za kimahakama na zile za kiutawala”, amesema Naibu Msajili.

Mhe. Kingwele amesema, mifumo hiyo inarahisisha na kuboresha shughuli za utoaji haki kwa wateja wa Mahakama. Vilevile inatoa fursa ya upatikanaji wa taarifa mbalimbali za utendaji wa kazi za Mahakama kwa usahihi na kwa wakati.

Mahakama imekuwa na safari ndefu ya kufikia hatua iliyofikia na ikumbukwe kuanzia mwaka 2014 Mahakama ilianza matumizi ya mfumo wake maarufu wa JSDS toleo la kwanza hadi ilipofika mwaka 2018 ilihamia kwenye mfumo wa JSDS 2.0 mfumo ukitoa huduma za kusajili mashauri kwa njia ya kielektroniki (e-filing) na kufanya malipo kwa njia ya kielektroniki (e-payment), ameongeza Mhe. Kingwele.

“Watumishi wa Mahakama siyo wageni kwenye matumizi haya ya kielektroniki. Kazi iliyo mbele yetu ni kuhakikisha kwamba Mahakama inafikia viwango vya kimataifa kwenye matumizi ya TEHAMA na wanufaika wakubwa wawe wateja wetu wa ndani na nje ya Mahakama”, amesisitiza Naibu Msajili huyo

Aidha, katika ujenzi wa mifumo yote ya kieletroniki inayokwenda kufundishwa na wataalam wa Mahakama wamefuata miongozo, viwango na taratibu zote kama zinavyotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao. Hivyo Mifumo iliyojengwa imekidhi viwango vya kitaifa na kimataifa katika matumizi na usalama wa taarifa zitakazoingizwa na kuhifadhiwa, amesema Mhe. Kingwele

Mhe. kingwele amewambia washiriki kuwa, ipo tofauti kubwa kati ya mfumo wa “Judicial Statistical Dashboard Systema (JSDS 2.0)” na mfumo mpya wa kielekitroniki wa kuratibu na kusimamia mashauri “Advanced Electronic Case Management System (e-CMS)”. Mfumo wa JSDS 2.0 ulitumiwa zaidi na wasaidizi wa kumbukumbu kusajili taarifa mbalimbali za mashauri na kuziuhisha mara baada ya shughuli za usikilizaji wa mashauri kukamilika mahakamani.

Mhe. Kingwele anasema, kwa kiasi kidogo Wahe. Majaji wafawidhi na Mahakimu wafawidhi waliingia kwenye mfumo kupanga mashauri kwa Wahe. Majaji au Mahakimu.

Mfumo huo mpya wa kielektroniki wa “Advanced Electronic Case Management System (e-CMS)” siyo tena kwa ajili ya Makarani unakwenda kutumika kwa asilimia mia moja na Wahe. Majaji na Mahakimu wote, hao ndiyo walengwa wakuu katika kuratibu shughuli zote zitakazoendeshwa ndani ya mfumo huo na kwa lugha ya TEHAMA wanaitwa “ICT users”.

“Niwaase wote mnaoshiriki mafunzo haya mambo yafuatayo kuwa na mifumo mizuri ni jambo moja lakini kuitumia mifumo hiyo ni jambo jingine lakini cha msingi sana, kama mifumo tutakuwa nayo halafu hatuitumii kutatua matatizo yetu ama kurahisisha utendaji wetu kupitia mifumo hiyo ni sawa na kutokuwepo”, Naibu Msajili aliwambia washiriki.

Lengo la haya mafunzo ni kujua namna ya kuitumia mifumo hiyo kwa ufasaha, na kuwafundisha maafisa wengine na watumishi wote pamoja na wadau kutumia mifumo hiyo kwenye utendaji kazi wa kila siku ili kurahisha utoaji wa huduma.

“Ni matarajio ya viongozi wetu kuwa, tutakwenda kuyafanyia kazi mafunzo haya na kuwafundisha wengine ili kwa pamoja ifikapo tarehe Mosi Novemba, 2023 tuanze matumizi ya mfumo huu kama ilivyoelekezwa ya kuwa ndiyo siku rasmi yakuanza kutumika katika mahakama zetu”, amesisistiza Mhe. Kingwele.  

Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Omari Kingwele akizungumza na washiriki wa mafunzo ya mfumo mpya wa kielekitriniki wa kuratibu na kusimamia mashauri (hawapo pichani) leo tarehe 18 Oktoba, 2023 katika Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Same Mhe Mussa Hamza (kushoto) ambaye ni muwezeshaji katika mafunzo hayo akiwa pamoja na wezeshaji wenza Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Siha Mhe. Jasmine Abdul (kulia) wakifuatilia ufunguzi wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi Mhe. Omari Kingwele (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wahasibu kutoka Wilaya za moshi wanaoshiriki mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi Mhe. Omari Kingwele (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu kutoka Wilaya za moshi wanaoshiriki mafunzo hayo.

Afisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Bw. Lukio Mrutu akiwa tayari kuwapitisha washiriki wa mafunzo hayo kwenye mfumo mpya huo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni