Alhamisi, 30 Novemba 2023

MAHAKAMA KUIMARISHA UTOAJI HAKI KWA MASHAURI YANAYOHUSU MILIKI UBUNIFU

Na. Innocent Kansha – Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Mahakama ya Tanzana imeanzisha mkakati madhubuti wenye lengo la kuimarisha utoaji haki kwa mashauri yanayohusu miliki ubunifu.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo tarehe 30 Novemba 2023 Ofisini kwake jijini Dar es salaam Prof. Ole Gabriel amesema Miliki Ubunifu ni eneo nyeti linalogusa nyanja zote za maisha ya kila siku ya binadamu na ni chachu ya ukuaji wa biashara, teknolojia, uchumi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

“Mahakama ya Tanzania kwa kulitambua hilo na pia kwa kutambua kuwa ni mdau mkubwa katika kulinda miliki ubunifu imechukua hatua madhubuti za kuhakisha inaimarisha utoaji haki kwenye eneo hilo”, amesema Mtendaji Mkuu Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel amesema, kwa kipindi cha miaka mitano Mahakama ya Tanzania, imepiga hatua kubwa sana katika kuboresha utoaji haki eneo la mashauri yanayohusu miliki ubunifu kwa kushirikiana na Shirika la Miliki Bunifu Duniani ‘World Intellectual Property Organization’ (WIPO)

Mtendaji Mkuu huyo ametaja baadhi ya mafanikio hayo kuwa ni pamoja na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na WIPO wamekwisha andaa miongozo juu ya haki miliki(Copyright), alama za biashara (trademarks), hataza (patent) na maumbo bunifu (Industrial design). Miongozo hiyo inatumiwa na waheshimiwa Majaji na Mahakimu kama rejea pale wanapokuwa wanaendesha na mashauri yanayohusu miliki ubunifu.

Prof. Ole Gabriel amesema, kuanzia mwaka 2022 hadi 2023 Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) lilitoa ufadhili kwa Majaji na Mahakimu 250 kwa lengo la kusoma masomo hayo kwa njia ya masafa ‘Distance Learning Course’. Mafunzo hayo ya masafa yameongeza uelewa mkubwa kwa washiriki hususani katika eneo la miliki ubunifu.

“Jambo hili linadhihirisha kuwa Mahakama ya Tanzania hivi sasa ina Majaji na Mahakimu wengi waliobobea kwenye eneo hili na wameiva katika kutoa huduma bora kwa mashauri yanayohusu miliki ubunifu na imesaidia kutoa elimu hii kwa makundi mbalimbalimbali wakiwemo wabunifu, wafanyabiashara, makampuni, wamiliki wa viwanda”, ameongeza Prof. Ole Gabriel

Mtendaji Mkuu huyo akataja mafanikio kuwa, Mahakama kwa kushirikina na WIPO wamekuwa wakifanya makongamano ya miliki ubunifu. Mapema mwaka huu, mwezi Machi kwa kushirikiano na WIPO Mahakama ilifanikiwa kufanya kongamono kubwa la miliki ubunifu kwa njia ya mtandao. Mkutano huo ulihudhuriwa na Majaji na Mahakimu wa Tanzania zaidi ya 150, wataalamu kutoka WIPO na Majaji waliobobea kwenye eneo hili la Miliki Ubunifu kutoka Berkeley Judicial Institute, Chuo Kikuu cha London, Marekani, Ulaya, na Kenya.

Mtendaji Mkuu alisema, mafanikio mengi yaliyofikiwa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na WIPO ni kuandaa muhtasari wa maamuzi mbalimbali ya Mahakama ya Tanzania kwa lengo la kuwarahisishia Majaji na Mahakimu kufanya rejea ya maamuzi ya Mahakama kwa wepesi wakati wa kufanya tafiti za kisheria zinazohusiana na mashauri ya miliki ubunifu.

Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa, maamuzi ya Mahakama ya Tanzania yanachapishwa kwenye mtandao mkubwa dunia WIPO Lex. Uchapishwaji wa Maamuzi hayo kwenye mtandao huo umeitambulisha kazi nzuri inayofanywa na Majaji wa Tanzania duniani na umewawezesha Majaji wa nchi mbalimbali kupata maamuzi yanayotolewa na Mahakama ya Tanzania kwenye eneo hilo.

 

Majaji na Mahakimu wa Tanzania wameweza pia kupata kwa urahisi maamuzi ya Nchi zingine kupitia mtandao huo na hivi sasa Mahakama ipo mbioni kuunganisha mfumo wa WIPO Lex na tovuti ya Mahakama ili Majaji na Mahakimu waweze kupata kwa urahisi maamuzi mbalimbali ya nchi zingine kupitia mtandao huo utakaoukuwa unaonekana kwenye tovuti ya Mahakama ya Tanzania”, ameongeza Mtendaji Mkuu.

 

Shughuli mbalimbali zinazofanywa na WIPO kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania hivi sasa zimeshawanufaisha Majaji na Mahakimu takriban 815 na hii imeweka Mahakama ya Tanzania katika nafasi nzuri ya kushughulikia vema mashauri yanayohusu hakimiliki (copyrights), alama za Biashara (Trademarks), hataza (Patents) na maumbo bunifu (Industrial designs).

 

Matendaji Mkuu huyo akatoa wito kwa wadau kuwa Mahakama ya Tanzania imeshajenga uwezo wa ndani, inapenda kutoa wito kwa wadau wa Miliki Ubunifu nchini kushirikiana na Mahakama kutoa elimu kwa umma juu ya elimu ya hakimiliki, alama za biashara, hataza na maeneo mengine yanayohusu miliki ubunifu.

“Hapa nchini tunao wabunifu, wasanii na wafanyabiashara wengi ambao kazi zao hazilindwi kisheria kutokana na uelewa mdogo wa masuala yanayohusu miliki ubunifu na namna gani ya kupata haki zao pale zinapovunjwa”, amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel akahitimisha kwa kueleza kuwa, Mahakama ya Tanzania ina dhamira ya kuhakikisha kuwa wabunifu, wafanyabishara, makampuni na viwanda hawakutani na kikwazo chochote kwa mambo yanayohusu haki zao haswa zile ambazo Mahakama kwa namna moja au nyingine inashiriki kuzilinda. Mahakama ina dhamira kubwa ya kuweka mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji kwa ustawi wa Taifa letu.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo tarehe 30 Novemba 2023 Ofisini kwake jijini Dar es salaam akieleza mikakati ya Mahakama ya Tanzania kuimarisha mambo yanayohusu Miliki Bunifu na mafanikio ya WIPO Tanzania ndani ya kipindi cha miaka mitano.

Afisa Kiungo baina ya Mahakama ya Tanzania na Shirika la miliki bunifu Duniani (WIPO) Tanzania Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Upendo Ngitiri akifafanua jambo kwa waandishi wa habari kwenye mkutano huo 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (mbele) akizungumza katika mkutano huo na waandishi wa habari katika ni Afisa Kiungo baina ya Mahakama ya Tanzania na Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) Tanzania Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Upendo Ngitiri.

Sehemu ya waandishi wa habari walioshiriki katika mkutano huo ulieleza mafanikio ya WIPO Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano

Picha na Innocent Kansha - Mahakama 





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni