Jumamosi, 11 Novemba 2023

MAHAKAMA KUU KANDA YA DAR ES SALAAM YATEGUA KITENDAWILI CHA WAFUNGWA, MAHABUSU

 Na. Innocent Kansha- Mahakama.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam imetimiza ahadi yake iliyoitoa ili kuhakikisha inatatua changamoto zinazowakabili wafungwa na mahabusu walioko magerezani kwa kuandaa na kutekeleza mpango maalum wa kuwawezesha Mawakili wa utetezi kupata muda wa kutosha wa kutembelea magerezani na kuzungumza na wateja wao kabla ya kuanza kwa usikilizwaji wa mashauri mbalimbali yanayowakabili.

Akizungumza kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-salaam, Mhe. Salma Maghimbi. Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Butamo Phillip aliwahakikishia wadau kuwa  zoezi la kuwatembelea Mahabusu litakuwa endelevu na litapewa muda wa kutosha kabla ya kuanza vikao ya Mahakama Kuu ili kuwapa wadau fursa ya kuweza kufanya mawasiliano na Mawakili wao.

“Mpango huu unalenga kuhakikisha kuwa Mawakili wa kujitegemea wanapata fursa ya kutosha ya kuonana na wateja wanaowawakilisha Mahakamani. Uwakilishi huu ni kwenye mashauri mbalimbali hususani ya Jinai kama vile mashauri ya Ugaidi, Mauaji na Madawa ya kulevya”, alisema Jaji Phillip.

Mhe. Phillip alisema kuwa, Mpango huo utakuwa endelevu na utakuwa ukifanyika kabla ya muda wa vikao maalum vya mashauri ya jinai (Criminal Sessions). Kanda ya Dar-es-salaam itaanda mazingira magerezani ya kuwawezesha Mawakili usafiri wa kwenda kwenye magereza hayo ili kuwatembelea wateja wao wanaowatetea kwa kupitia takwa la kisheria. Hii itaweza kurahisisha mawasiliano kati ya Mawakili na Wateja wao Pamoja na kuhakikisha haki inatendeka kwa washtakiwa kwa kupata haki ya utetezi wa mashtaka wanayokabiliwa nayo.

Nichukue fursa hii kuwashukuru kwa dhati Mawakili wote waliojitokeza kutoka Chama cha Mawakili wa Kujitegemea (TLS) kwa kukubali wito wa Mahakama na kujitokeza kwa ajili ya zoezi hili. Vile vile niwashukuru Jeshi la Magereza kwa kukubali na kuhirikiana nasi mara baada ya kuelezwa adhima ya Mahakama”, alisema Mhe Phillip.

Mhe. Phillip aliwambia Mawakili walioshiriki zoezi hilo kuwa, dhumuni la safari hiyo ya kutembelea Magereza yanayowahifadhi Mahabusu wenye Mashauri mahakamani ni kujenga msingi wa uelewa wa pamoja kati ya Mawakili na Mahabusu ili waweze kuzungumza nao ikiwa ni maandalizi ya vikao vya kusikiliza mashauri wanayokabiliwa nayo. Kwa kufanya hivyo Mahakama inatekeleza na kutimiza takwa la nguzo ya tatu ya Mpango Mkakati wa Ushirikishwaji wa Wadau.

Mhe. Phillip aliwambia Mawakili hao kuwa, kwa sasa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-salaam hivi karibuni imekwisha andaa vikao 10 ambavyo vitahusisha, vikao vine (4) vya mashauri ya mauaji, viako vitano (5) vya mashauri ya ugaidi, na kikao kimoja (1) cha shauri la madawa ya kulevya.

Kwa upande wao maafisa magereza wameshukuru jihitada za Mahakama za kufanya ukaguzi huo, kwakuwa unapunguza sana malalamiko ya mahabusu hao wanaosubiri kusikilizwa kwa mashauri yao. Wakaiomba Mahakama iendelee kudumisha ushirikiano huo, kwa hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Mahakama Kuu, Kanda ya Dar-es-salaam katika kusukuma mashauri kwani kumepunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya mahabusu waliopo magerezani ambapo imepungua kwa takribani asilimia 50 ya wale waliokuwepo mwaka jana.

Zoezi hilo limefanyika kutokana na ziara mbalimbali zaMahakama za ukaguzi wa Magereza. Katika ziara hizo Mahakama imekuwa ikipokea malalamiko na hoja mbalimbali kutoka kwa Mahabusu na Wafungwa waliopo magerezani.

Mhe. Phillip alifafanua kuwa, moja kati ya changamoto iliyoanishwa na mahabusu wanaosubiri vikao vya mashauri (Criminal Session) ilikuwa ni kutopatiwa haki yao ya utetezi kwa ufasaha. Mahabusu hao wamekuwa wakilalamikia uwakilishwaji wao kwenye vikao vya jinai, uwakilishi ambao hutolewa na Mahakama bila gharama.

“Mahabusu walilalamikia kutokupata fursa ya kutosha ya kuongea na mawakili wao na kuweza kujua masuala mbalimbali ya utetezi wao na hata wengine kuonana na Mawakili wa utetezi katika chumba cha Mahakama wakati shauri linaendelea hivyo kuhisi kuwa wananyimwa haki ya uwakilishi vema kwenye utetezi wao”, alisema Jaji Phillip.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Joseph Lwambano (wa nne kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mawakili na Maafisa wa Gereza la Keko wakati wa ziara ya kutembelea Magereza kwa lengo la kuzungumza na wafungwa na Mahabusu.



Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Joseph Lwambano (wa nne kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mawakili na Maafisa wa Gereza la Keko wakati wa ziara ya kutembelea Magereza kwa lengo la kuzungumza na wafungwa na Mahabusu.









Hakuna maoni:

Chapisha Maoni