Jumatano, 8 Novemba 2023

TEHAMA TIBA YA VISINGIZIO VYA MAHABUSU, WAFUNGWA KUTOKUFIKA MAHAKAMANI

Na Hasani Haufi- Mahakama, Songea

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha amemkabidhi Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Tunduru, Mrakibu wa Magereza Uswege Yoran vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) vya kisasa vitakavyotumika kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao.

Vifaa hivyo vilivyokabidhiwa hivi karibuni vitawawezesha Mahabusu waliopo gerezani kusikiliza mashauri yao bila kufika mahakamani moja kwa moja.

Akizungumza wakati akikabidhi vifaa hivyo, Mhe. Karayemaha alisema kuwa Mahakama ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika matumizi ya TEHAMA na imeangalia changamoto nyingi zinazosababisha kuchelewa kwa huduma za kimahakama, hivyo ikaanzishe mifumo mingi inayoenda kutibu changamoto hiyo.

“Ni matarajio yetu kuwa vifaa hivi vitafanya kazi iliyokusudiwa ya usikilizaji wa mashauri na vitaenda kutibu kero na visingizio mbalimbali, ikiwemo kukosekana kwa mafuta na gari ya kupeleka mahabusu na wafungwa mahakamani. Vifaa hivi pia vitasaidia mahabusu wenye changamoto za kiafya ambazo zinawafanya kushindwa kutoka gerezani na kupelekea mashauri kuchelewa,’’ alisema.

Mhe. Karayemaha alisema kuwa, vifaa hivyo vilivyokabidhiwa kwa gereza hilo vitaenda kuongeza kasi ya upatikanaji wa haki kwa haraka na kupunguza au kuondoa kabisa malalamiko kwa mahabusu na wafungwa, kwani mashauri yanapokaa kwa muda mrefu ndivyo haki ya mahabusu waliopo gerezani inachelewa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Tunduru ameushukuru uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea kwa kusikia kilio cha muda mrefu na mwishowe kuwakabidhi vifaa hivyo vya kisasa kwa ajili ya kusiliza mashauri kwa njia ya mtandao, hivyo kuwapunguzia gharama ya kubeba mahabusu hao.

“Tuna furaha isiyo na kifani kwani tunapitia changamoto kubwa, ambazo tunashindwa kuzitatua kwa vile zipo nje ya uwezo wetu, hivyo vifaa hivi tutavitumia kwa matumizi yaliyokusudiwa kwa lengo la kupunguza gharama za usafiri na muda pia,” alisema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Julius Mtatiro kwa ujumla aliipongeza Mahakama ya Tanzania inayoongozwa na Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Ibrahimu Juma, kwa kupiga hatua kubwa katika upande wa TEHAMA na kuwa mfano bora wa kuigwa kwa taasisi zingine za kiserikali.

Alisema kuwa miongoni mwa malengo ya Mahakama ni kutoa haki kwa wakati, hivyo vifaa vilivyotolewa vitaenda kutibu matatizo ya mahabusu na akaahidi kuwa msimamizi katika vifaa hivyo.

“Mahakama ya Tananzania imekuwa ikikimbia katika upande wa utoaji haki kwa njia ya TEHAMA na kuwa ni sehemu moja wapo ya taasisi zingine za kiserikali kuiga kitu kizuri kama hicho siyo vibaya. Kutokana na jitihada hizi ninaahidi nikiwa kama Mkuu wa Ulinzi nitahakikisha vifaa vinakuwa salama siku zote kwa manufaa ya taifa letu,’’ alisema.

Katika tukio jingine, Jaji wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo, Mhe. Upendo Madeha naye amekabidhi vifaa kama hivyo juzi tarehe 06 Novemba, 2023 katika Gereza la Wilaya Mbinga. Alisema kuwa vifaa hivyo ni moja ya mageuzi ya kitaasisi katika kukamilisha na kuboresha mfumo wa uendeshaji wa mashauri mtandao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wilaya Mbinga, Mrakimu Mwandamizi wa Magereza Aloyce Mbongo ameushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea kwa kuwarahisishia huduma na kuwapunguzia gharama ya usafiri na muda.

“Zipo sababau nyingi, lakini kimsingi Mahakama imefanya maboresho na mageuzi makubwa sana ya kitaasisi ikiwemo mifumo kama JSDS, TANZLII, TAMS na mfumo wa kusikiliza mashauri kwa njia ya mtandao,” alisema.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Mhe. Aziza Mangosongo ameushukuru uongozi wa Mahakama kwa jitihada wanazozifanya za kuboresha huduma za Mahakama katika maeneo mbalimbali, ikiwa lengo ni kuhakikisha huduma za Mahakama zinapatikana kwa urahisi.

Aliomba wataalam wa mifumo wa Mahakama kutembelea na kutoa elimu ya matumizi ya vifaa hivyo mara kwa mara ili kuhakikisha changamoto za mifumo zinatotatuliwa.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha (wa pili kulia) akimkabidhi TV yenye ukubwa wa inchi 65 kwa Mkuu wa Gereza la Mahabusu Tunduru, Mrakibu Uswege Yoran kwa ajili ya matumizi ya usikilizaji wa mashauri ya kwa njia ya mtandao. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Mhe. Julius Mtatiro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha (kulia mwenye suti ya bluu) akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Mhe. Julius Mtatiro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha akitetea jambo na Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Julius Mtatiro (wa kwanza kutoka kulia).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha na wenzake kwenye luninga baada ya Afisa TEHAMA, Bi. Catherine Okumu kukamilisha zoezi la kufunga vifaa hivyo.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Upendo Madeha akisaini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Mbinga.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Upendo Madeha (wa pili kulia) akimkabidhi vifaa vya TEHAMA, Mkuu wa Gereza la Mahabusu Mbinga Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Aloyce Mbongo.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Songea, Mhe. Upendo Madeha (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Mhe. Aziza Mangosongo (kulia) na kushoto kwake ni Mkuu wa Gereza la Mbinga, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Aloyce Mbogo pamoja na wadau wengine wa Mahakama.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni