Jumatano, 8 Novemba 2023

WATUMISHI MAHAKAMA YA KAZI WAELIMISHWA UTOAJI WA HUDUMA YA KWANZA

Na Mwanaidi Msekwa-Mahakama, Kazi

Wahenga wanasema, “Elimu ni bahari, Elimu haina mwisho.” Kamati ya Elimu ya Ndani Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi imekuwa ikiwapatia watumishi mafunzo mbalimbali ya uhalisia katika mazingira yote.

Hili limejitokeza hivi karibuni pale Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina alipoongoza Viongozi na watumishi wa Mahakama hiyo kujifunza namna bora ya uokoaji wa maisha ya binadamu katika hali hatarishi.

Mtaalamu kutoka Ofisi ya Msalaba Mwekundu, Bw. Bonaventure Minja alifafanua wakati wa mafunzo hayo maana ya huduma ya kwanza, kuwa ni msaada wa awali anaopatiwa mtu aliyejeruhiwa au kuugua ghafla na mara nyingi huduma hiyo hutolewa na mtu wa kawaida kwa mtu aliyepata jeraha au ugonjwa.

Watumishi walijifunza kanuni zinazotumika wakati wa kutoa huduma ya kwanza huku Bw. Minja akielezea umuhimu wa kutoa huduma ya kwanza kwa muarithika aliyepatawa na majanga. Kwa msisitizo, aliwaasa wanapotoa huduma ya kwanza wajiepushe na vitendo vitakavyopelekea kumsababishia mgonjwa matatizo makubwa.

Akiendelea kutoa mafunzo hayo, Bw. Minja pamoja na Mratibu wa Mafunzo katika Ofisi ya Msalaba Mwekundu, Bw. Deus Almachius walishirikiana vema kutoa elimu kwa njia ya vitendo. Jambo hilo liliongeza hamasa kubwa kwa Viongozi na watumishi waliohudhuria darasa hilo na kutoa shauku ya kuendelea kujifunza zaidi.

Akiahirisha mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu ambaye ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo aliwashukuru wawezeshaji na kuwaomba kufika mahakamani hapo tena pale watakapoalikwa.

Naye Jaji Mfawidhi alimpongeza Bw. Bonaventure kwa umahili wake katika uwasilishaji wa mada. Mafunzo kwa watumishi wa Divisheni ya Kazi yanatolewa kila siku za Ijumaa kuanzia saa 1:30 hadi 2:45 asubuhi katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama na huwafikia wengi kwa kupitia njia ya mtandao.

Mtaalamu kutoka Ofisi ya Msalaba Mwekundu, Bw. Bonaventure Minja (kulia) alifafanua jambo wakati wa mafunzo hayo. Picha chini akiwa na mwenzake, Mratibu wa Mafunzo katika Ofisi ya Msalaba Mwekundu, Bw. Deus Almachius (ambaye amelala chini) akionyesha namna ya kutoa huduma ya kwanza.

Zoezi la utoaji elimu kwa vitendo likiendelea (juu na chini).

Wakufunzi wa mafunzo hayo wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni