Jumanne, 7 Novemba 2023

WATAALAMU WA MAHAKAMA TANZANIA WAPO NCHINI KAZAKHASTAN

·Wabadilishana uzoefu na wenzao wa kituo cha kuchakata taarifa ya kimahakama

Na Tiganya Vincent-Kazakhstan 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Profesa Elisante Ole Gabriel jana tarehe 6 Novemba, 2023 amewaongoza Wataalamu wa Mahakama ya Tanzania katika ziara ya kubadishana uzoefu kuhusu uimarishaji wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuboresha shughuli za kila siku za utoaji wa haki nchini. 

Timu hiyo ambayo imeweze kutembelea Mahakama ya Juu ya Upeo (Supreme Court) ya Kazakhastan ambapo ilipata fursa ya  kutembelea chumba maalum cha kusimamia, kuendesha na kudhibiti mtandao na kituo   cha kuchakata taarifa za kimahakama kwa ajili ya kujifunza. 

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Ole Gabriel alimweleza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Kazakhstan Nail Akhetzakirov kuwa tukio hilo ni mwendelezo wa iliyofanyika mwaka 2018 ambapo watajifunza uendeshaji, usimamizi wa shughuli za Mahakama kwa kutumia TEHAMA. 

Alisema Nchi ya Kazakhastan imepiga hatua katika matumizi ya TEHAMA katika shughuli mbalimbali za Mahakama, hivyo nao watabadilishana uzoefu ili kuendeleza mapinduzi makubwa yanayoendelea ya Mahakama mtandao nchini Tanzania ikiwemo kupunguza matumizi ya karatasi katika uendeshaji wa shughuli zake. 

Aidha, Prof. Ole Gabriel alimuomba Mtendaji Mkuu mwenzake wa Mahakama ya Kazakhastan kuendelea kushirikiana kwa Maafisa TEHAMA wa pande zote kwa kukubalishana uzoefu kwa ajili ya kuwajengea uwezo  ili waweze kuendana na kasi ya mabadiliko ya Teknolojia hiyo yanayobadilika kila wakati duniania. 

Naye Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Kazakhastan aliishukuru timu ya Tanzania kwa ziara hiyo ya kubadilisha uzoefu na kuahidi kuendelea na ushirikiano utakaowezesha pande zote mbili kuimarisha zaidi matumizi ya TEHAMA mahakamani. 

Awali, Prof. Ole Elisante na timu yake walipata fursa ya kutembelea Ofisi za Benki ya Dunia na kukutana na Mwakilishi wa Kazakhstan Andrei Mikhnev. 

Viongozi wengine waliopo katika ziara hiyo ya mafunzo ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Jenifa Omolo, Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Angelo Rumisha na Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Alesia Mbuya. 

Sanamu ya Lady Justice katika Mahakama ya Upeo wa Juu ya Kazakhstan.

Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini Kazakhstan Andrei  Mikhenew akizungumza na ujumbe wa Mahakama ya Tanzania ulipomtembelea ofisini kwake tarehe 6 Novemba, 2023.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa na ujumbe wa Mahakama ya Tanzania uliotembelea Mahakama ya Upeo wa Juu ya Kazakhstan kwa ajili ya kubadilishana uzoefu wa usimamizi na uendeshaji wa mifumo ya kimahakama.

Mwakilishi wa Benki ya Dunia Andrei Mikhenew akiwa na ujumbe wa Mahakama ya Tanzania ambao uko nchini Kazakhstan kwa ajili ya kubadilishana uzoefu wa usimamizi na uendeshaji wa mifumo ya kimahakama.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akisalimiana na Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini Kazakhstan Andrei Mikhenew (kushoto) alipowasili na timu yake kwenye ofiosi za Benki za Dunia.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni