Jumapili, 12 Novemba 2023

TAASISI YA MAFUNZO INAYOANDAA MAJAJI KAZAKHSTAN YAONESHA NIA YA KUSHIRIKIANA NA 'IJA'

Na Tiganya Vincent, Astana-Kazakhstan

Taasisi ya Mafunzo kwa ajili ya kuwaanda Majaji ya nchini Kazakhstan imesema iko tayari kushiriana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) nchini Tanzania kwa lengo la kubadilishana uzoefu utakaosaidia kuimarisha utendaji na kuwaendeleza Maafisa hao wa Mahakama. 

Hatua hiyo ilifikiwa tarehe 10 Novemba, 2023 katika Mji Mkuu wa Kazakhstan wa Astana wakati wa mkutano kati ya ujumbe wa Mahakama ya Tanzania uliongozwa na Mtendaji Mkuu Prof. Elisante Ole Gabriel pamoja na wa Taasisi ya Majaji  ya Mahakama ya Upeo ya Kazakhstan.

Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Majaji ya Kazakhstan iliyopo chini ya Mahakama ya Upeo, Bi. Baimoldina Zauresh Hamitovna alisema kuwa wao wako tayari kuingia makubaliano na Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto Tanzania kwa lengo  la kubadilishana uzoefu kitaaluma na kuboresha Sekta ya utoaji haki kwa pande zote.

Alisema kwa muundo wao kabla ya mtu kuwa Jaji anatakiwa kushiriki mafunzo ya Shahada ya Uzamili (Master Degree) ya Sheria katika Taasisi hiyo na ili apate udahili  anapaswa kuwa na miaka 28 na kuendelea, Stashahada (Diploma) katika fani ya Sheria na uzoefu usiopungua miaka mitano.

Zauresh aliongeza kuwa katika Nchi hiyo kuna njia mbili za kuwa Jaji  ya kwanza ikiwa ni lazima mtu awe amesoma Stashahada (Diploma) ya Sheria katika Chuo Kikuu cha Nchi hiyo na ya pili ni lazima mtu asome katika Taasisi ya Mafunzo kwa ajili ya kuwaanda Majaji na kufaulu mitihani yote.

Alisema mtu anayepitia katika Taasisi ya Mafunzo ya kuwaandaa Majaji anakuwa na nafasi kubwa ya kufaulu wakati wa ushindani wa kuwatafuta watu wanaostahili kuteuliwa kuwa Majaji nchini humo.

Awali, Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel aliuomba Uongozi wa Taasisi hiyo kuangalia namna ya kuingia makubaliano ya kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto nchini Tanzania katika kubadiliana uzoefu wa kuwaendeleza Maafisa Mahakama na Watumishi wengine.

Alisema kuwa, Chuo cha Uongozi wa Mahakama cha Lushoto (IJA) kimekuwa na utaratibu wa kuwapa mafunzo elekezi Majaji, Mahakimu na Watumishi wengine wasio Maafisa wa Mahakama kabla ya kuanza majukumu yao mapya jambo ambalo limesaidia kufanya kazi kwa ufanisi ndani ya Mahakama ya Tanzania.

Prof. Ole Gabriel alisema wakikubaliana wanaweza kuandaa Programu ambazo zinaweza kufundishwa katika pande mbili kama sehemu ya kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo kwa watumishi na Maafisa wa Mahakama waliopo kazini na wale walioteuliwa kuingia kazini.

Aliongeza kuwa, endapo watakubaliana Uongozi wa Mahakama ya Tanzania utahakikisha unasimamia makubaliano yaliyofikiwa kwa manufaa ya pande zote mbili.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Angelo Rumisha alisema kwa Tanzania Majaji wanaandaliwa kutoka Vyuo Vikuu mbalimbali kwa kupata Shahada ya Sheria na kupita katika Shule ya Sheria (Law School of Tanzania) na wanapoteuliwa wanapata mafunzo elekezi katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.  

Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Majaji ya Kazakhstan iliyopo chini ya Mahakama ya Upeo, Bi. Baimoldina Zauresh Hamitovna (katikati) akitoa maelezo kwa ujumbe wa Mahakama ya Tanzania uliokwenda kujifunza jinsi wanavyowaandaa Majaji kabla ya kuteuliwa. Ujumbe huo ulikutana na Viongozi wa Taasisi hiyo tarehe 10 Novemba, 2023.
Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akizungumza na Uongozi wa Taasisi ya Mafunzo ya Kuwandaa Majaji ya Nchini Kazakhstan wakati wa ujumbe aliouongoza ulipokwenda kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo wanavyotoa mafunzo mnamo tarehe 10 Novemba, 2023.
Jaji Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama  ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (wa pili kutoka kulia) akitoa ufafanuzi kwa Uongozi wa Taasisi ya Mafunzo ya Kuwaandaa Majaji ya Kazakhstan wakati wa ziara ya mafunzo katika Taasisi hiyo.
Ujumbe wa Mahakama ya Tanzania (kulia) ukiwa na Uongozi wa Taasisi ya Mafunzo ya Majaji ya Kazakhstan (kushoto) wakati wa kikao cha kubadilishana uzoefu kuhusu mafunzo kwa Majaji watarajiwa na waliopo madarakani.
Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Kuwaandaa Majaji cha Nchini Kazakhstan  Baimoldina Zauresh Hamitovna (kulia) mara baada ya mkutano wa pande mbili wa kubadilishana uzoefu juu ya kuwaendeleza Majaji na kuwaandaa Majaji wapya.
Picha ya pamoja kati ya Viongozi wa Taasisi ya Mafunzo kwa ajili ya kuwaanda Majaji ya nchini Kazakhstan na Ujumbe kutoka Mahakama ya Tanzania. Katikati ni Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresha cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (wa saba kutoka kulia ), Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya kuwaandaa Majaji ya Kazakhstan iliyopo chini ya Mahakama ya Upeo, Bi. Baimoldina Zauresh Hamitovna (kulia kwa Prof. Ole Gabriel) pamoja na Wajumbe wengine walioshiriki katika Mkutano huo wa kubadilishana uzoefu. 
Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Kuwaandaa Majaji ya Kazakhstan Baimoldina Zauresh Hamitovna (wa pili kushoto) akitoa maelezo kwa ujumbe wa Mahakama ya Tanzania uliotembelea Taasisi hiyo jana kwa lengo ya kujifunza na kubadlishana uzoefu.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof Elisante Ole Gabriel (wa pili kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo kwa Majaji ya Kazakhstan Baimoldina Zauresh Hamitovna (katikati ), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (wa kwanza kulia), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Omolo (wa pili kutoka kulia), Afisa Mwandimizi kutoka Benki ya Dunia-Tawi la Tanzania Benjamin Mtesigwa (wa kwanza kushoto) katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa kubadilishana uzoefu juu ya kuwaandaa na kuwaendeleza Majaji.

(Picha na Tiganya Vincent)

(Imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni