Jumapili, 12 Novemba 2023

UJUMBE WA MAHAKAMA NCHINI WATEMBELEA MAHAKAMA YA BIASHARA NA KITUO CHA USULUHUSHI KAZAKHSTAN

Na Tiganya Vincent, ASTANA-Kazakhstan

Ujumbe wa Mahakama ya Tanzania ukiongozwa na Mtendaji Mkuu Prof. Elisante Ole Gabriel umetembelea Mahakama ya Kituo cha Kimataifa cha Biashara Astana na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi  kilichopo nchini Kazakhstan kwa lengo ya kubadilishana uzoefu kuhusu njia za usuluhishi katika utatuzi wa migogoro  ikiwemo ya kibiashara na uwekezaji katika sekta mbalimbali.

Akizungumza jana mjini Astana mara ya baada ya kupata maelezo  kutoka kwa Watendaji wa Mahakama hiyo na Kituo hicho, Prof. Ole Gabriel alisema kuwa ziara hiyo ilikuwa na lengo la kubadilishana uzoefu ambao utasaidia kuendelea kuboresha zaidi Kituo cha Usuluhishi cha Mahakama Kuu nchini Tanzania.

“Uzoefu tuliopata utasaidia kuweka mipango ambayo itakiwezesha Kituo cha Usuluhishi kutumika zaidi katika utatuzi wa migogoro mbalimbali ikiwemo ile ya kibiashara, ya sekta za ujenzi na uwekezaji kwa ajili ya kuimarisha uchumi kwa kupunguza mlolongo mrefu wa kesi unaotumia njia nyingine za Mahakama, alisema Prof. Ole Gabriel.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mahakama hiyo, Almat Igenbayev alisema Kituo cha Kimataifa ya Usuluhishi (IAC) kilianzishwa kwa lengo kutatua migogoro ya kimataifa inayohusu biashara na uwekezaji wa aina mbalimbali na imekuwa ikifanya kazi kwa saa 24.

Alisema, katika kutekeleza majukumu yake Mahakama hiyo imepata uzoefu mkubwa katika kujihusisha na usuluhishi wa migogoro katika maeneo mbalimbali ya uchumi, ikiwemo masuala ya kibenki, huduma za kifedha, viwanda na Kampuni za ujenzi, masuala ya mafuta na gesi kwa kuhusisha Kampuni ya Kazakhstan na nje ya Nchi hiyo kama vile Uingereza na Ireland ya Kaskazini, New Zealand, Jamhuri ya Korea, Uswisi, Urusi, Ukraine, China, Latvia, Uturuki, Misri, Tajikistan, Kyrgyz, Ushelisheli na nyingine.

Igenbayev alisema Mahakama ni huru haingiliwi na Serikali na hata usuluhishi unaofikiwa katika Mahakama hiyo hauwezi kuhojiwa na Mahakama yoyote.

Naye Mwanasheria kutoka Mahakama hiyo, Aidana Rassova alisema Mahakama ya Biashara na Kituo cha Kimatifa cha Usuluhishi vimekuwa vikitumia Majaji kutoka Mataifa mbalimbali katika usikilizaji na uendeshaji wa mashauri yake na kuongeza imekuwa ikipata msaada mkubwa kutoka Serikali ya Kazakhstan.

Aliongeza kuwa hadi kufikia Mwezi Aprili mwaka 2023, Mahakama hiyo ilikuwa haitozi ada yoyote kwa ajili kufungua shauri isipokuwa kwa mambo yaliyokuwa yakihusu usuluhishi ndio walitakiwa kulipa ada kwa ajili ya wasuluhishi.

Alisema baada ya Mwezi Aprili mwaka huu walianza kutoza ada ya kufungua shauri lakini ni kidogo ukilinganisha na Mahakama nyingine za nchini humo.

Ujumbe wa Mahakama ya Tanzania umemaliza ziara ya mafunzo nchini Kazakhstan baada ya kutembelea Mahakama ya Upeo (Supreme Court) na kujifunza matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari katika usimamizi wa shughuli mbalimbali, kisha kukutana na Naibu Waziri wa Sheria, Baraza la Juu linalosimamia Maadili ya Majaji na kutembelea Taasisi ya Mafunzo kwa Majaji.

Viongozi waliongozana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ni pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu na Mkuu wa Kituo cha Maboresho cha Mahakama Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Omolo, Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Bi. Alesia Mbuya na watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania.

Mkurugenzi Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi (IAC) iliyopo nchini Kazakhstan,  Almat Igenbayev (kushoto) akionesha ujumbe wa Mahakama ya Tanzania moja ya Maktaba ya kuhifadhia kumbukumbu mbalimbali wakati walipotembea Kituo hicho jana tarehe 11 Novemba, 2023  kwa ajili ya kupata uzoefu kuhusu usuluhishi.

 Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi (IAC) iliyopo nchini Kazakhstan,  Almat Igenbayev (katikati) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (kulia) mara baada ya kutembelea Mahakama hiyo jana tarehe 11 Novemba, 2023 kwa ajili ya kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya usuluhishi.

 Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mahakama ya Kimatifa ya Usuluhishi (IAC) iliyopo nchini Kazakhstan  Almat Igenbayev (kulia)  mara baada ya kutembelea Mahakama hiyo kwa ajili ya kubadilishana uzoefu kuhusu usuluhishi.

Mwanasheria kutoka Mahakama ya Kimatifa ya Usuluhishi (IAC) iliyopo nchini Kazakhstan (mwenye koti la Kaki kushoto) Aidana Rassova akitoa maelezo kwa ujumbe wa  Mahakama ya Tanzania ulioongozwa na Mtendaji Mkuu, Prof. Elisante Ole Gabriel katika  ziara ya mafunzo na kubadilishana uzoefu katika Mahakama hiyo kuhusu usuluhishi katika kutatua migogoro katika masuala ya biashara na uwekezaji.

Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wa Mahakama ya Tanzania baada ya kutembelea Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi iliyopo nchini Kazakhstan kwa ajili ya kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro ya kibiashara na uwekezaji.

(Picha na Tiganya Vincent)

(Imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni