Ijumaa, 24 Novemba 2023

TAASISI ZA KIFEDHA ZANOLEWA MATUMIZI YA NJIA MBADALA YA UTATUZI WA MIGOGORO

Na. Innocent Kansha – Mahakama.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi kimeanzisha na kutekeleza programu ya kuzitembelea taasisi za kifedha mkoani Dar es salaam kwa lengo la kubadilishana uzoefu juu ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Akiongoza ujumbe wa Kituo cha Usuluhishi kuzitembelea taasisi hizo za kifedha ikiwemo ya Benki ya NMB na Benki ya CRDB ambao ni wadau wa nje wa Kituo hicho kwa nyakati tofaouti hivi karibuni, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Zahra Maruma alisema, Kituo cha Usuluhishi kwa kutambua umuhimu wa taasisi za kifedha katika kukuza uchumi endelevu ikiwa ni pamoja na kuyaishi maudhui ya kauli mbiu ya wiki na siku ya sheria nchini ya mwaka 2023.

“Kituo kinawajibu wa kusimamia na kutekeleza kauli mbiu hiyo isemayo Umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya Usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu: wajibu wa Mahakama na wadau, ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa nguzo ya tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama wa mwaka 2020/21 hadi 2024/25.

…ndiyo uliopelekea kuandaliwa kwa kikao cha wadau wa nje ili kupata uzoefu wa vitu gani vinakwamisha matumizi ya kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kutatua migogoro inayohusisha mabenki na wateja wao kiasi ikapelekea kesi kukaa mahakamani kwa muda mrefu na kufanya fedha zilizokopwa kutorudishwa kwa wakati na hivyo kuathiri uchumi kwa kiasi kikubwa ”, alisisitiza Mhe. Maruma.

Jaji Maruma alisema uzoefu wa ushughulikia migogoro ya Mabenki kwa njia ya usuluhishi ulitolewa na kubainisha maeneo yafuatayo kuwa ndiyo chanzo cha matatizo mathalani kutofuatwa kwa taratibu za ukopeshaji, kutopatikana kwa ridhaa ya mwenza au mwenye umiliki katika mali inayowekwa kama dhamana na matendo ya kijinai yanayohusika wakati wa taratibu za ukopeshaji fedha kupitia taasisi za kifedha.

Mhe. Maruma aliendelea kuangazia maeneo mengine yenye dosari kama kutorudisha hati baada ya mkopo kulipwa, kutoweka vizuri kumbukumbu za mikopo, kutopeana taarifa za hatua mbalimbali zinazotakiwa kuchukuliwa katika mikopo chechefu na kutoa mkopo wa pili kwa mtu bila uelewa na ridhaa ya mdhamini.

Jaji Maruma aliongeza kuwa, kutoa notice kwa anuani isiyo sahihi au tofauti na iliyotolewa wakati wa kusaini mkataba wa kukopa, kuuza mali bila kufuata hatua za kisheria na usimamizi mbovu wa utekelezaji wa maamuzi ya benki na pia madalali walioteuliwa kutosimamiwa ipasavyo chini ya kifungu cha 132 kifungu kidogo cha nne(4) cha Sheria ya Ardhi.

Mhe. Jaji Mfawidhi huyo, aliwasisitiza wadau hao wa nje juu ya faida za usuluhishi na  katika kuchambua faida hizo alisema mara nyingi zikiangaliwa asili za mahusiano ya kibenki, mikopo, muonekano wa wateja wafikapo mahakamani ni wazi kuwa mashauri  ya kibenki yana uwezekano mkubwa wa kumalizika ndani ya muda mfupi na hivyo kuokoa pato la taifa.

Kwa upande wa Maafisa wa Benki walibainisha changamoto wanazokutana nazo kutoka mahakamani kwamba, bado Mahakama inatoa nafasi kwa watu ambao wameshakubaliana kumaliza kesi, kurudi tena mahakamani kufungua mashauri tena Mahakama wakisikilizwa kwa viini au hoja zilezile.

“Hoja za kutopatikana bei stahiki ya kuuzwa mali, taratibu kutofautiana huibuliwa upya. Naiomba Mahakama kutoruhusu hii hali mara kwa mara tena madamu watu wameshamaliza kesi kwenye usuluhishi maana inaporuhusiwa hujikuta mashauri yanaenda tena mpaka Mahakama ya Rufani na kuchukua muda mrefu kutatua mgogoro”, aliongeza Afisa wa Benki.

Afisa huyo Benki, aliendelea kusema kuwa kesi zao nyingi sana zipo kwenye Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ambayo huwa yanatoa Zuio (Injunctions) mara nyingi sana. Akahoji ikiwa kama Mahakama kwa nafasi yake inaweza kuwasilisha hoja hiyo kwa Mabaraza, kwani ni eneo ambalo wateja wengi wanalitumia vibaya ili kukwamisha mabenki kurudisha fedha zilizokopwa kupitia dhamana zilizowekwa na kuongeza kuwa kitendo hicho kimekuwa kikikatisha tamaa sana.

Kwa nyakati tofauti wajumbe hao kutoka taasisi za kifedha waliongeza kuwa mkwamo mwingine unatokana na suala la uwakilishi (Representation) mara nyingine linakwamisha zoezi la usuluhishi kwa sababu muwakilishi huja na msimamo na hivyo juhudi zote za msuluhishi kuonesha faida ni hafifu na badala yake kutozaa matunda, mwakilishi utakuta bado husimama na alichotoka nacho nje ya chumba cha usuluhishi. Kwa hivyo hupelekea mteja kuamini kuwa ana nafasi ya kushinda kesi huko mbeleni badala ya kutumia vizuri nafasi ya usuluhishi.

Zoezi hilo la kuzitembelea taasisi za kifedha kwa mkoa wa Dar es salaam ni endelevu ili kujaribu kutafuta ushawishi wa kutatua migogoro baina ya wateja na mabenki ili kukuza uchumi na kupunguza migogoro inayochukua muda mrefu kwa njia ya kawaida mahakamani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Zahra Maruma (aliyevalia ushungi) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa nje wa Taasisi ya kifedha kutoka benki ya CRDB. Wengine Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Angela Bahati (mwenye koti la bluu)

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Zahra Maruma (wa tatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa nje wa Taasisi ya kifedha kutoka benki ya NMB, pamoja na Viongozi waandamiazi wa Kituo hicho. Mwingine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Angela Bahati (wa pili kulia).


Sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti kutoka Benki ya NMB walioshiriki katika majadiliano ya namna ya kuboresha taasisi za kifedha juu ya matumizi ya njia mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti kutoka Benki ya NMB walioshiriki katika majadiliano ya namna ya kuboresha taasisi za kifedha juu ya matumizi ya njia mbadala ya utatuzi wa migogoro wakifuatilia wasilisho kwa makini

Menejimenti ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo hicho Mhe. Zahra Maruma (wa kwanza kulia) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Angela Bahati (wa pili kulia) na pia Viongozi waandamizi wa Kituo hicho wakiwa kwenye majadilianao na taasisi hizo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi Mhe. Zahra Maruma (kulia) akifanya wasilisho kwa watumishi wa menejimenti ya Banki ya CRDB ya namna bora ya matumizi ya njia mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Mjumbe wa Menejimenti kutoka Benki ya CRDB akichangia kwenye mdahalo huo


Afisa Mtendaji Mkuu kutoka Benki ya NMB Bi. Ruth Zaipuna akitoa neno la ukaribisho kwa menejimenti kutoka Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi (hawapo pichani)

(Picha kwa hisani Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni