Jumamosi, 2 Desemba 2023

WAZIRI GWAJIMA AZINDUA MAHAKAMA YA MFANO KUPINGA UKATILI, ULAGHAI DHIDI YA WATOTO MTANDAONI

 Na. Innocent Kansha - Mahakama

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima amefungua rasmi mafunzo yanayoendeshwa kwa njia ya Mahakama ya Mfano yenye kauli mbiu isemayo “ukatili na ulaghai dhidi ya watoto mtandaoni” (Moot Court on Children Cyber Bullying and Online Grooming) ikiwa ni sehemu ya kauli mbiu ya kitaifa ya kampeni ya siku 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia ambayo ni ‘Wekeza: Kupinga Ukatili wa Kijinsia’.

Akifungua Mahakama hiyo ya Mfano iliyoandaliwa na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) iliyoendeshwa kwenye ukumbi wa mikutano wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam leo tarehe 2 Desemba, 2023, Waziri Gwajima amesema, kauli mbiu ya kitaifa ina lenga kuhamasisha kila Mtanzania, popote alipo na kwa nafasi aliyokuwa nayo anatakiwa kuchukua hatua kupinga ukatili wa kijinsia.

“Niwapongeze wanachama wa TAWJA ambao ni Majaji na Mahakimu, kwa kuchukua hatua katika nafasi walizonazo na kuamaua kupaza sauti kwa kuandaa Mahakama ya Mfano iliyojikita kwenye kesi ya mfano ya ukatili dhidi ya watoto mitandaoni kwani kutokana na ukuaji wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), kesi za aina hii zimeanza kufikishwa Mahakamani”, amesema Waziri Gwajima.

Mhe. Gwajima amesema, takwimu zilizotolewa mwezi wa Oktoba, 2023, na Waziri mwenye dhamana ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, wakati akifungua Kongamano la saba la TEHAMA, zinaonyesha kuwa matumizi ya TEHAMA yameongezeka kutoka watumiaji milioni 29.9 kwa mwezi Aprili 2022 hadi kufikia watu milioni 34.04 kwa mwezi Juni 2023 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 13. Pamoja na mafanikio mengi yaliyoletwa na TEHAMA, pamekuwepo pia changamoto ya uhalifu wa kimtandao ikiwemo uhalifu wa unyanyasaji wa kimtandao dhidi ya wanawake na watoto.

Vilevile, Mhe. Gwajima akatoa Taarifa ya Utafiti kuhusu Hali ya Ukatili wa Watoto Mtandaoni nchini, kwa mwaka 2022 (Disrupting Harm Report in Tanzania) inaeleza tathmini ya kina ya hali ya ukatili wa kijinsia nchini, athari za ukatili wa kingono, mitazamo ya watoto juu ya ukatili wa kingono mtandaoni na mwitikio wa kitaifa wa namna ya kupambana na aina hii ya ukatili.

Matokeo ya utafiti yanaonesha kuwa, asilimia 4 ya watumiaji wa mtandao wenye umri wa miaka 12-17 nchini Tanzania ni manusura wa ukatili wa mtandaoni. Watoto wengi hufanyiwa vitendo vya ukatili kupitia mitandao ya kijamii kama vile WhatsApp, Instagram, Facebook, Tik Tok pamoja na mitando mengine ya kijamii.

Mhe. Gwajima amebainisha athari zingine ikiwa ni wanaofanya vitendo vya ukatili ni watu wanaofahamika na watoto wakiwemo ndugu wa karibu na marafiki na pia watoto wanaofanyiwa ukatili hawajui namna na sehemu ya kutoa taarifa ili wapate msaada.

Aidha, Waziri Gwajima akafafanua kuhusu hatua mbalimbali ambazo Serikali pamoja na Wizara yake imezichukua ili kukabiliana na uwepo wa aina mpya ya Ukatili dhidi ya Watoto Mitandaoni unaosababishwa na kukua kwa maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Mhe. Waziri Gwajima akatanabaisha kuwa kufuatia kuanza kwa kushamiri kwa matukio haya ya ukatili wa kimtandao dhidi ya Watoto, Serikali imeunda kikosi kazi cha Taifa cha Ulinzi na Usalama wa Mtoto mtandaoni chenye lengo la kuhakikisha kuwa watoto wanalindwa dhidi ya ukatili wa mtandaoni na kuwasaidia kutumia vifaa vya kieletroniki kwa usahihi na usalama,

Vilevile, kuanza mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Mtoto ili iweze kuakisi mazingira ya sasa ikiwa ni pamoja na ukatili wa watoto mtandaoni (online child abuse) na Serikali inafanya mapitio ya Sera ya hali ya usalama katika mitandao ili kubaini maeneo ya kuboresha, amesisitiza Mhe. Waziri Gwajima.

“Elimu itakayotolewa leo na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi kuhusu namna Mahakama zetu zinavyoshughulikia kesi za ukatili wa kimtandao dhidi ya Watoto ambao ni Taifa la kesho, kuwapa uafahamu wa matendo ya ukatili yanayofanyika kwenye mitandao na changamoto zitokanazo na uhalifu wa unyanyasaji wa kimtandao hasa kwenye ukusanyaji wa ushahidi na itasaidia pia kutahadharisha vijana wetu kuwa makini na matumizi salama na bora ya huduma na bidhaa za TEHAMA’’, amefafanua Mhe. Gwajima.

Mhe. Waziri Gwajima amehitimisha kwa kutoa shukrani za kipekee kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji Mkuu wa Tanzania Zanzibar, Jaji Kiongozi, Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Uongozi mzima wa Mahakama ya Tanzania Bara na Visiwani. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nikiwasahau Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wametupatia ukumbi wa kufanya Mafunzo hayo. Pia niwashukuru Chuo cha Sheria kwa Vitendo na Chuo Kikuu cha Tumaini kwa kutoa taarifa na kuwaruhusu wanavyuo kushirki mafunzo hayo.

Naye Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel amesema Chama kimeandaa mkakati wa kuratibu mafunzo ya kupinga ukatili wa kijinsia kwa njia ya Mahakama ya Mfano katika mikoa 5 ya Tanzania Bara na Zanzibar katika mikoa ya Arusha, Dodoma, Mbeya, Mwanza na Zanzibar kwa tarehe tofauti tofauti ili wadau wengi waweze kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo.

Mhe. Sehel amesema kuwa tayari mafunzo kama hayo wamekwisha kutolewa katika Kanda 2 za Mahakama Kuu ambazo ni Dodoma na Arusha na yalikuwa ya mafanikio makubwa sana kutokana na mwitikio wa wadau wanaopinga ukatili wa kijinsia.

“Kama tunavyofahamu kuna sheria mbalimbali zilizotungwa na serikali yetu dhidi ya uhalifu wa kimtandao, hata hivyo maendeleo ya teknolojia yamekuwa yakikuwa na kusafiri kwa kasi ya mwanga na hata matumizi yake yanaendelea kukua kila siku. Hii inaleta kuibuka kwa makosa mapya ya kimtandao na hivyo kufanya baadhi ya sheria zetu kupitwa na wakati”, amesisitiza Mhe. Sehel

Mwenyekiti huyo wa TAWJA akatoa mfano wa sheria hizo kama sheria ya makosa ya kimtandao, unyanyasaji wa kimtandao (Cyber Bullying) ni kosa la kijinai na adhabu yake ni kifungo kisichopungua miaka 3 au faini isiyopungua shilingi milioni 5 au kutumikia kifungo na faini kutegemeana na mazingitra ya kesi.

“Hata hivyo sheria hii ya makosa ya kimtandao aihakisi mazingira na uhalisia, kwa sasa kumeibuka uhalifu wa kurusha moja kwa moja picha za unyanyasaji wa kijinsia mtandaoni (Live streaming of sexual abuse) uhalifu huu bado sheria haija itambua hivyo tunaomba Mhe. Waziri utambue hilo”, ameongeza Mhe. Sehel

…..Ni matumaini yetu kuwa sheria pamoja na sera za nchi zitarekebishwa mapema iwezekanavyo ili kukidhi matakwa ya karne ya sasa ya maendeleo ya viwanda na teknolojia na kesi ya Mahakama ya Mfano itakayosikilizwa hii leo inahusu unyanyasaji wa kijinsia wa kimtandao”, amefafanua Mhe. Sehel.  

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (kulia) akipokea zawadi ya Kitabu kilichoandaliwa na Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake kutoka kwa Mwenyekiti wa chama hicho Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel leo tarehe 2 Desemba, 2023 katika ukumbi wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam baada ya uzinduzi wa Mafunzo yanayoendeshwa kwa Mahakama ya Mfano.


Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima akitoa hotuba yake wakati wa uzinduzi wa mafumzo hayo


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti Wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel akitoa hotuba yake wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam na Mlezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) akitoa neno la utangulizi wakati wa mafunzo iliyoendeshwa kwa njia ya Mahakama ya Mfano kwenye ukumbi wa mikutano wa Nkrumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji na sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Sehemu ya wanafunzi kutoka vyuo vikuu walioshiriki mafunzo hayo.

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (wa pili kushoto) akiwa na sehemu ya Majaji na viongozi waandamizi wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania wakati wa hafla hiyo

Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi
Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi

Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima (wa pili kushoto) akiwa na sehemu ya Majaji na viongozi waandamizi wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania wakati wa hafla hiyo wakibadilisha mawazo.

Sehemu ya Mawakili walioendesha mafuzo kwa njia ya Mahakama ya Mfano wakiwasilisha hoja jazo mbele ya jopo la Majaji (hawapo pichani) na wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itakayo saidia kuelimisha wananchi unyanyasaji wa kijinsia mitandaoni


Sehemu ya wadau wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itasaidia sana kuelimisha wananchi

         Sehemu ya Mawakili walioendesha mafuzo kwa njia ya Mahakama ya Mfano           wakiwasilisha hoja jazo mbele ya jopo la Majaji (hawapo pichani) na wadau          wakifuatilia Elimu iliyotolewa  na TAWJA kupitia Mahakama ya Mfano itakayo saidia   kuelimisha wananchi unyanyasaji wa kijinsia mitandaoni

                                (Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni