Jumamosi, 27 Januari 2024

JAJI MAGHIMBI AFAFANUA CHIMBUKO LA KAULI MBIU YA WIKI, SIKU YA SHERIA

Na. Mwandishi Wetu- Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi amebainisha kuwa, chimbuko la Kauli Mbiu ya wiki na siku ya sheria nchini kwa mwaka 2024 inatokana na Tume ya Haki Jinai iliyoundwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na kupewa jukumu la kupitia mfumo mzima wa mnyororo wa utoaji haki.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa wiki ya sheria kwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam iliyoambatana na matembezi leo tarehe 27 Januari, 2024 katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini hapo Mhe. Maghimbi amebainisha kuwa Tume hiyo iliibua mambo 18 yanayogusa Mahakama ya Tanzania, kutokana na taarifa hiyo ndiyo kauli mbiu ya mwaka huu ilizaliwa ili kuakisi utekelezaji wa mapendekezo ya taarifa ya Tume hiyo.

Mhe. Maghimbi ameongeza kuwa, katika kutoa uamuzi wa mashauri ya madai na jinai, Mahakama itaongozwa na sheria na Kanuni mbalimbali ambazo zimewekwa. Kwa muktadha huo, Mahakama inatumika kama chombo cha utoaji haki kwa ajili ya kuboresha ustawi wa Taifa.

Mahakama inatakiwa kushirikiana na wadau kuboresha mfumo jumuishi wa haki jinai. Mfumo huo unatakiwa ufanye kazi kwa kushirikiana na kwa kusomana kwenye mifumo ya Kielekitroniki kwa lengo la kuhakikisha kuwa wananchi wanaohitaji kupata haki Mahakamani, basi wanatakiwa wapate haki zao kwa wakati bila kucheleweshwa kwa haki hiyo kwa sababu tu ya mdau mmoja wa haki jinai aidha kwa makusudi au kwa uzembe kushindwa kutekeleza majukumu yake kwa wakati, amesisitiza Jaji Maghimbi.

“Kwa hivyo basi, lengo la kauli mbiu tajwa ni kutoa elimu na hamasa kwa umma juu ya umuhimu wa dhana ya haki kwa ustawi wa Taifa, nafasi ya Mahakama na wadau katika kuboresha Mfumo Jumuishi wa Haki Jinai,” ameongeza Mhe. Maghimbi

Aidha, Mhe. Maghimbi amesema katika kutoa elimu kwa umma juu ya kauli mbiu hiyo, ni vema katika wiki ya sheria na siku ya kilele chake, mada za utoaji elimu zijikite katika kuelezea na kufafanua kwa uchache mambo ya msingi yayohusiana na maboresho yanayoendelea Mahakamani na vile vile ushirikishwaji wa wadau katika maboresho hayo kwa ajili ya kuboresha mfumo wa Haki Jinai kwa ujumla.

Mhe. Maghimbi amewahakikishia wananchi watakaofika kwenye viwanja vya kutolea elimu kuwa, mbali na elimu watakayoipata kuhusu maudhui ya wiki ya sheria ya mwaka huu, pamoja na elimu ya mambo mengine ya kisheria, watapata pia nafasi ya kutoa malalamiko, maoni na mapendekezo ya uboreshaji wa huduma za Mahakama.

“Nimatumaini yangu na ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kuwa, Taasisi zote zinazosimamia sheria na zinazohusika kwenye Haki Jinai, zitatumia fursa hii kuhakikisha kuwa wananchi wanaelewa vyema dhana nzima ya mfumo wa Haki Jinai inavyofanya kazi zake na pia kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa wakati bila kucheleweshwa,” amesisitiza Jaji Mfawidhi huyo.

Mhe. Maghimbi akawakumbusha wananchi huduma watakazo kutana nazo katika kipindi chote cha wiki ya sheria ikilenga elimu kuhusu taratibu za ufunguaji wa mashauri hasa kwa njia ya mtandao, uendeshaji wa mashauri kimtandao, sheria na taratibu zinazotumika katika kuendesha mashauri mbalimbali kama mashauri ya ndoa na talaka, ardhi, migogoro ya kazi pamoja na utekelezaji wa hukumu, sheria za watoto, taratibu za mashauri ya mirathi na sheria na taratibu zinazotumika katika kuendesha mashauri ya jinai.

Aidha, katika maonesho hayo elimu itatolewa na Waheshimiwa Majaji, Naibu Wasajili, Watendaji, Mahakimu pamoja na wadau wa Mahakama wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF),Afisa Mfawidhi Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wanasheria Wanawake (TAWLA), Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA), Ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam, Ofisi ya Mkuu wa Magereza Mkoa wa Dar es Salaam, Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Ofisi ya Huduma kwa Jamii Mkoa wa Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji Kituo cha Msaada wa Sheria kwa Wanawake na Watoto (WLAC), Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), na wadau wengine.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi akitoa hotuba wakati wa uzinduzi wa wiki ya sheria nchini katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es salaam leo tarehe 27 Januari, 2024.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (hayupo pichani)


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (wa kwanza kulia) akiwa kwenye matembezi yaliyoashiria uzinduzi wa wiki ya sheria nchini, wengini ni Mgeni rasmi wa hafla hiyo ya uzinduzi Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mhe. Albert Chalamila (wa pili kulia) akiwa na vingozi wengine wa mkoa.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam wakiwa kwenye matembezi


Sehemu ya watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa serikali Mkoa wa  Dar es Salaam wakiwa kwenye matembezi.
Sehemu ya Kikosi cha Blasibendi kikiongoza matembezi
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mhe. Albert Chalamila (wa tatu kulia) akiwa kwenye matembezi akiwaongoza Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu na vingozi wengine wa mkoa.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mhe. Albert Chalamila (wa tatu kushoto) akiwa kwenye matembezi akiwaongoza Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu na vingozi wengine wa mkoa.






Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania wakati wa uzinduzi wa wiki ya sheria kwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam iliyoambatana na matembezi leo tarehe 27 Januari, 2024 katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni