Jumamosi, 27 Januari 2024

MAHAKAMA MOROGORO YAFANA UZINDUZI WIKI YA SHERIA

Na. Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro leo Tarehe 27 Januari, 2024 imefanya uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria kwa matembezi makubwa yaliyowajumuisha mamia ya wakazi wa Morogoro.

Sherehe ya Uzinduzi ilianzia kwa matembezi katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro hadi ilipo stendi ya zamani ya Dalala Morogoro Mjini. Matembezi hayo yaliongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Maliama sanjali na mwenyeji wake ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor ambaye aliambatana na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro Mhe. Devotha Kamzola na Mhe. Hadija Kinyaka.

Akizungumza wakati wa kufungua maazimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima alitoa pongezi kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuwa na kauli mbiu inayoendana na wakati wa sasa kwakuwa mfumo wa haki ni shirikishi kwa Mahakama na wadau.

“Kauli mbiu hii itasaidia kuleta taifa linalojali utu, usawa na haki na ikizingatiwa kuwa suala la haki limezungumzwa mahali pengi katika vitabu vitakatifu mmekuwa na jitihada nzuri sana katika kupeleka ujumbe kwa jamii kupitia kauli mbiu mbalimbali mnazozitoa katika vipindi vya wiki ya sheria, pia nimefurahishwa baada ya kupata taarifa kuwa mmeipandisha kauli mbiu hii ya wiki ya sheria kileleni, hongereni sana,” alisema Mgeni rasmi Mhe. Malima.

Alitoa rai yake kwa wananchi wa mkoa wa Morogoro kusogea katika mabanda ya maonesho ili waweze kujifunza mambo ambayo mahakama imeandaa kwa ajili yao katika mwaka huu wa 2024.

“Tuwasaidie wadau kupitia mifumo mbalimbali ya mahakama inatusaidia kujua mahakama zetu na huduma zinazotolewa na mahakama, kwahiyo niwapongeze sana kwa maboresho makubwa ya Mahakama upande wa TEHAMA kwakuwa mmeturahisishia huduma ya haki sanjari na kumtambua wakili na kishoka kwa kupitia mfumo wa E- wakili.

Akizungumza na vyombo vya Habari mara baada ya maadhimisho uzinduzi wa wiki ya sheria Mhe. Mansoor alisema kuwa huu ni uwanda wa wananchi kusogea katika mabanda ya kutolea elimu ili waweze kujifunza na kupata uelewa wa sheria na namna ambavyo Mahakama inafanya kazi ikishirikiana na wadau wake na pia namna matumizi ya TEHAMA yanaweza kuwasaidia kupunguza gharama za kutembea ili kuisogelea huduma ya Mahakama.

“Mwananchi afike hapa apewe elimu na atapata uelewa wa namna kesi inavyopokelewa mpaka kufika Mahakamani na hata inapomalizika

Aidha, katika ufunguzi huo wasanii mbalimbali waliburudisha akiwemo Afande Sele, Tabu Mtingita, Mau Fundi na Dulla Makabila Pamoja na watumishi wa Mahakama, wadau, wananchi na wanafunzi baada ya ufunguzi huo pia walipata nafasi ya kupanda miti katika mto Mindu ikiwa ni sehemu ya kuunga jitihada za serikali katika kutunza Mazingira ambapo miti zaidi ya mia tatu imepandwa.

Maadhimisho ya wiki ya sheria yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 30 Januari, 2024 na kilele chake kinatarajiwa kuwa tarehe 1 Februari,2024 na kauli mbiu yake ni “Umuhimu wa dhana ya haki kwa ustawi wa Taifa:Mahakama na Wadau katika kuboresha mfumo jumuishi wa haki Jinai”

Mgeni rasmi Mkuu wa Mko awa Morogoro Mhe. Adam Malima akizungumza wakati hafla akizindua wiki ya sheria leo tarehe 27 Januari, 2024.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor akizungumza wakati akimkaribisha Mgeni Rasmi kuzindua wiki ya sheria.

Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakiwa wameketi meza kuu kushoto ni Mhe. Devotha Kamzola na kulia ni Jaji Mhe. Hadijah Kinyaka wakifuatilia sherehe za uzinduzi wa wiki ya sheria

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro wakifuatilia matukio wakati wa uzinduzi wa wiki ya sheria
Matembezi wakati wa sherehe za uzinduzi wa wiki ya sheria
Matembezi wakati wa sherehe za uzinduzi wa wiki ya sheria

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor akitoa zawadi wa msanii afande Sele wakati akitumbuiza.

Kikundi cha scauti wakionesha ukakamavu
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni