Ijumaa, 2 Februari 2024

MKUU WA MKOA PWANI ATOA WITO KWA MAHAKAMA KUWAFUNDISHA VIONGOZI WA SERIKALI

Na. Eunice Lugiana – Mahakama, Pwani 

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge ametoa wito kwa Mahakama kuishirikisha Serikali kuelezea kuhusu maboresho yanayofanywa na Mahakama ili kurahisisha utoaji wa elimu kwa wananchi kwani Serikali ina mtandao mkubwa wa kuwafikia wanachi.


 Akizungumza katika hafla ya kuadhimisha Wiki na siku ya Sheria nchini jana tarehe Mosi Februari, 2024 mkoani Pwani alipokuwa akiwahutubia wananchi na wadau wa Mahakama Mhe. Kunenge alisema, bado wananchi wengi hawajui mipaka ya Serikali na Mahakama hivyo ni wajibu wa Viongozi wa Mahakama na Serikali tuwafahamishe mipaka hiyo ili kuepuka kuingilia utendaji kazi wa Muhimili.


Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Pwani Mhe. Joyce Mkhoi katika hotuba yake alisema kauli mbiu ya mwaka huu imekua  na malengo makuu mawili  kuhamasisha Mahakama na wadau juu ya umuhimu wa kufungamanisha na kuboresha mfumo jumuishi wa haki jinai unaosomana ili kusaidia katika  kubadilishana taarifa kuanzia hatua ya upelelezi, uendeshaji wa mashtaka na utoaji wa maamuzi.


“Kauli mbiu hii ina lengo la kuikumbusha Mahakama na Taasisi nyingine za haki jinai kuwa zinawajibika katika kufungamanisha na kuboresha mfumo jumuishi wa haki jinai. Hivyo nakuwataka wadau kuongeza juhudi ya kuwekeza kwenye eneo la miundo mbinu ya TEHAMA na usimikaji wa mifumo ya kidigitali”, alisisitiza Mhe. Mkhoi. 

Mhe. Mkhoi ameongeza kuwa, wadau wa Mahakama wanawajibika kuendana na kasi ya mabadiliko ya nchi kwa kufanya maboresho katika ujenzi wa mifumo kwa taasisi zote zinazoshirikiana na Mahakama katika Mnyororo wa haki jinai ili utendaji kazi uweze kuleta tija na uwe wa ufanisi mkubwa ambao utaweza  kukabiliana na changamoto ambazo zimekuwa zinaukabili mfumo wa haki jinai.


Akisikiliza kesi ya kwanza inayoashiria uzinduzi rasmi wa Mwaka wa kimahakama wakati wa maadhimisho ya siku ya sheria Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kibaha Mhe. Emmael Lukumai amesema Mahakama imepiga hatua katika kusikiliza mashauri kutoka kwenye nyaraka ngumu na sasa Mahakama inasikiliza kesi katika nyaraka laini na zama za nyaraka ngumu zimeisha.


Akionyesha jinsi haki jinai ilivyo rafiki ametoa masharti rahisi ya dhamani ya mshtakiwa aliyekua na kosa la kusafirsha kiwango kidogo cha madawa ya kulevya aina ya bhangi Mhe. Lukumai amesema masharti hayo ni wadhamini wawili walio na barua za utambulisho wa makazi na mali kauli ya shiligi milioni moja.


Kilele cha siku ya sheria kimeadhimishwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani na Mgeni wa Heshima alikua Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge aliye ambatana na kamati ya ulinzi  na usalama ya Mkoa, sherehe hizo pia zimehudhuriwa na viongozi wa dini taasisi za serikali na viongozi wa vyama vya siasa mawakili wa kujitegemea pamoja na wananchi wa Kibaha.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge akihutubia Wananchi na Wadau wa Mahakama (hawapo pichani) Katika Sherehe za Siku ya Sheria nchini katika Viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani

Hakimu Makazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani Mhe. Joyce Mkhoi akitoa Hotuba yake mbele ya Mgeni wa Heshima (hayupo pichani) katika Kilele cha Siku ya Sheria Nchini Mkoa Pwani

 

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge (katika) akiwa meza kuu na Viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Pwani (Kushoto) Ni Mkuu wa Mashtaka Mkoa wa Pwani Bi. Faraja Kiula, Hakimu Mkazi Mfawidhi Wa Mahakama Ya Hakimu Mkazi Kibaha Mhe, Joyce Mkhoi (wa pili kushoto), wengine ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mawakili Wakujitegemea Bi, Rita Ntagazwa (wa kwanza kulia) na  Hakimu Mkazi Mfawidhi Wa Mahakama Ya Wilaya Kibaha Mhe. Emmael Lukumai (wa pili kulia) .

 Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Makimu wa Mkoa wa Pwani

Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Mkoa wa Pwani
 Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mawakili wa Serikali Mkoa wa Pwani




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni