Jumatano, 16 Oktoba 2024

MAHAKIMU, MAWAKILI TABORA WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA TEHAMA, AKILI MNEMBA

Na AMANI MTINANGI, Mahakama - Tabora

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora kwa kushirikiana na Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea Mkoa wa Tabora imeandaa mafunzo kuhusu Sheria ya Mtandao na Akili Mnemba kwa Mawakili wa Kujitegemea na baadhi ya Mahakimu wa Kanda hiyo.

Akizungumza hivi karibuni wakati wa Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Tabora, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi alisema kuwa, katika maisha ya sasa shughuli nyingi kibinadamu zimeunganishwa na mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) sambamba na Akili Mnemba.

“Ninatambua kuwa siku hizi maisha ya sasa shughuli nyingi kibinadamu zimeunganishwa na mifumo ya TEHAMA na Akili Mnemba hivyo ni jukumu letu kama wanasheria kujua njia sahihi za kushughulika na mashauri na masuala yanahusisha akili mnemba na uwasilishaji wa vidhibiti vya kielekroniki mahakamani,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza kuwa, ni muhimu na ni jukumu la Wanasheria kufahamu njia sahihi za kushughulikia mashauri na masuala yanayohusisha akili mnemba pamoja na uwasilishaji wa vidhibiti vya kielekroniki pale vinapohitajika mahakamani.

Wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Wakili Kelvin Kayaga kutoka Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Tabora, alisema Chama hicho kimeandaa mafunzo jumuishi kwa ajili ya Mawakili na Mahakimu wa Kanda ya Tabora kwa lengo la kuongeza ujuzi na maarifa ya Mawakili katika eneo la ushahidi wa kimtandao na akili mnemba.

“Tunafurahi kuandaa mafunzo jumuishi ambapo washiriki wake ni Mawakili wa Kujitegemea na Mahakimu wa Kanda ya Tabora, tukilenga kuongeza ujuzi na maarifa ya Mawakili katika eneo la ushahidi wa kimtandao na akili mnemba,” alisema Wakili Kayaga.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya Sheria ya Mtandao na Akili Mnemba yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Mhe. Jaji Dkt. Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki.
 
Washiriki wa Mafunzo wakifuatilia kwa makini somo linalofundishwa.


Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea Tabora, Wakili Kelvin Kayaga akitoa neno la ufunguzi wa mafunzo ya Mawakili na Mahakimu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Mhe. Jaji Dkt. Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki wa mafunzo (hawapo katika picha).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)








Hakuna maoni:

Chapisha Maoni