Jumatano, 26 Machi 2025

JAJI MFAWIDHI MTWARA AONGOZA WATUMISHI KUTEMBELEA KITUO CHA KULELEA WATOTO

Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, hivi karibuni aliungana na Watumishi kutoka Kanda hiyo kutembelea Kituo cha Elimu ya Watoto wenye mahitaji maalumu na changamoto mbalimbali, ikiwemo usonji, kilichopo Mtwara mjini.

Watoto wa Kituo hicho kinachoitwa ‘Upendo Rehabilitation Day Center,’ wakiongozwa na Walezi wao, waliwapokea wageni wao kwa furaha na kuwakaribisha.

Baada ya hapo, Jaji Mfawidhi alizungumza machache na Msimamizi wa Kituo hicho kuhusu watoto na uendeshaji wake kwa ujumla. Mhe Kakolaki aliwashukuru Walezi wa watoto hao kwa kazi ya kipekee ya kuwalea na kuwafunza.

"Hawa ni watoto wetu na wanahitaji msaada na uangalifu maalumu, ninawaomba wasiwe na wasiwasi, bali waendelee kuwaongoza na kuwatunza. Endeleeni juhudi hii ya upendo kwani mnajaza moyo wa matumaini,’ alisema.

Jaji Mfawidhi aliwaeleza Walezi hao kuwa kila wanachokifanya kwa watoto hao ni kikubwa na dhamana kubwa ya kibinadamu ambayo Mungu atawabariki. Pia aliwasihi Watumishi wenzake kutokuishia hapo, bali waendelee kuwasaidia na kuwatia nguvu wenzao katika kuwalea watoto hao.

Vile vile, Mhe. Kakolaki alishirikiana na Watumishi wa Mahakama kuwawezesha watoto hao baadhi ya mahitaji kama vyakula na vifaa vya kuwasaidia, akitambua changamoto zinazowakabili.

Alihimiza jamii yote kushiriki katika kulinda na kuendeleza haki kwani ni Kituo kinachoendelea kukuza matumaini kwa watoto wenye mahitaji maalum na changamoto mbalimbali.

Baada ya shughuli hiyo matendo ya hisani, Watumishi wa Mahakama na Wadau mbalimbali walikutana katika Iftar ya pamoja iliyofanyika kwenye Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara. Iftar hiyo ilikuwa sehemu ya kukuza ukaribu na upendo, hasa katika kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramdhan na Kwaresma.

Wakati wa hafla hiyo, Jaji Mfawidhi aliwasihi Watumishi wote kuendelea kujisogeza kwa Mwenyezi Mungu na kufanya matendo mema.

Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Sheikh Jamaldin Chamwi, ambaye alikuwa miongoni mwa Viongozi wa Dini waliohudhuria, alisisitiza ibada na kukazia juu ya yale aliyoyataja Jaji Mfawidhi kabla ya kafunga kwa dua.  


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akiungana na Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mtwara kukabidhi kwa Msimamizi wa Kituo vyakula na vifaa mbalimbali kwa ajili ya watoto hao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto) baada ya kupokelewa kituoni pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Saidi Ding’hoi (katikati) na Naibu Msajilli wa Mahakama Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana (kulia).

Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mtwara wakishuhudia uchangamfu na ukarimu kutoka kwa watoto.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akizungumza na watoto, wakionyesha tabasamu na kumfurahia.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitoa neno katika Iftar iliofanyika kwenye Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara.

Majaji wakiwa kwenye meza moja na Viongozi wa Dini wakati wa Iftar.

Watumishi na Wadau mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo ya Iftar (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma


 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni